Jamvi La Siasa

KINAYA: ‘Ouru’ anaandaa Mlima kupiga kura ya hisia, hasira na dharau?

Na DOUGLAS MUTUA February 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HIVI umewahi kupiga kura ya chuki? Au dharau? Au ya hasira, ilimradi tu? Kura za aina zote hizo hupigwa kutokana na hisia kali, hasa nia ya kumuudhi na kumkasirisha usimyepigia.

Aghalabu, anayepigiwa huwa ama hatoshi mboga, au ni mtu mbaya zaidi akilinganishwa na anayenyimwa kura yenyewe, lakini ni njia ya kumwambia anayenyimwa kuwa ‘nakuchukia na kukudharau kuliko mpinzani wako, ambaye tayari sote tunajua hafai kitu!’

Ni kisa cha mwaka 2022 ambapo wakazi wa janibu za Mlima Kenya walimpigia Kasongo kura ili kumkasirisha na kumwonyesha Ouru kwamba hawatambui ufalme wake.

Ni kisa cha mwaka 2013 ambapo wafuasi wa Bwana Wiper walimhimiza aungane na RAO na wakampigia RAO kura ili kuwakasirisha Ouru na Samoei (sasa Kasongo) kwa sababu wawili hao walimnyima Bwana Wiper tiketi ya kuwania urais.

Nakumbuka hasira walizokuwa nazo Wakambodia siku zile! Huko nje vijiweni, na kwenye vikao vya ‘Bunge la Mwananchi’, wafuasi hao wa Wiper walifoka na kuapa kuwafunza adabu Ouru na Samoei kwa ‘kumsaliti mtoto wetu’.

Hakika, wafuasi wa Wiper walijaribu kuwafunza adabu kwa sababu walipiga kura kwa fujo kumchagua RAO, ila kura zao hizo hazikutosha kumpa urais.

Siasa zina vituko; yaani jina la mtu fulani linaweza kutumiwa kuwatishia watu. Ni sawa na ‘chokora’ kukutishia umpe pesa, lau sivyo akupake kinyesi. Na unajua si utani kwa kuwa kinyesi chenyewe anacho mkononi!

Mbinu hiyo ya kutishia watu kwa jina la mtu ilitumika sana nchini Amerika mnamo mwaka 2024 wakati wa kampeni za uchaguzi wa urais.

Omba-omba wakiandika kwenye mabango makubwa na kuketi kwenye njia-panda ili watu wawape hela: “Nipe hela au nimchague Trump!”

Nimekumbuka haya yote baada ya kumuona Ouru akijaribu kufufua Muungano wa Azimio la Umoja, tena akampa Bwana Wiper usukani.

Nimejiuliza jina ‘Azimio’ litachukuliwaje Mlimani, hasa ikikumbukwa kuwa walilikataa wakati wa uchaguzi wa mwaka 2022.

Labda hii ni fursa ya mkazi wa Mlimani kupiga kura ya hasira, kumuonyesha Kasongo kuwa, ‘hata ikiwa nilikataa Azimio nikakuchagua wewe, sasa niko radhi kula matapishi yangu kama mbwa badala ya kukuchagua tena’!

Nimesikia Ouru na marafiki zake wanataka kubadili jina hilo na kujiumba upya ili wamjumuishe Riggy G, ambaye bado anasikiliza ‘ground’, lakini hilo ni wazo baya.

Ikiwa wanataka kuwa na athari kubwa kisiasa, basi na wahakikishe hawaondoi jina ‘Azimio’; litatumika kama tusi la kumtukana Kasongo, yaani kulipenda kwa nia ya kumuudhi tu.

Nikikumbuka Riggy G alivyoutukana na kuuchafulia jina Muungano wa Azimio mwaka 2022, nitacheka nusra mbavu ziniteguke nikimuona akifoka, “Azimio! Azimio! Azimio!”

Kweli hakuna cha kudumu isipokuwa mabadiliko, hasa katika siasa za Kenya. Keti kitako tufurahie.

– Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika (mutua_muema@yahoo.com)