KINAYA: Wamunyoro ana kupe wengi wanaomnyonya damu
SIKU ya kufa kwa nyani, miti yote huteleza. Na wakati huu inawatelezea wanasiasa kweli-kweli, hasa wanaotokea Mlima Kenya.
Na haijalishi wewe ni mwanasiasa wa mrengo gani, ndiwe nyani hasa, na kila tawi la mti unaloshika linakubwaga chini kishenzi!
Bila shaka ukiwa rafiki wa Kasongo, mambo yanakuendea vibaya haraka, na hata wewe unajua kumnadi huko ni sawa na kuchuuza mbuzi ulaya Saudia.
Lakini hata wanasiasa wazembe wanaotafuta kila fursa kwenda kukariri kiapo cha uaminifu kwa Wamunyoro hawana bahati.
Ninachowapendea wapigakura wa mlimani ni kwamba mara nyingi wanamdadisi mwanasiasa binafsi na kuamua anatosha mboga au la.
Ikiwa hatoshi, wanamtupa kwenye pipa la takataka na kumsahau. Hakuna wanasaisa mashuhuri huko, hasa ikiwa wanatelekeza kazi walizopewa na wananchi.
Tatizo ni kwamba wanasiasa wa eneo hilo hawaonekani kuelewa kuwa siasa za kujipendekeza kwa vigogo hazina mashiko huko; wameamua ni heri washinde Wamunyoro badala ya kutumikia wananchi.
Na bila shaka namuelewa mwana huyo wa Mau-Mau kwa sababu kikawaida huwezi kuwakataza watu kukutembelea. Hata wakija na umbea ni sawa tu, watakusaidia kusukuma siku usiione ndefu sana.
Mwanasiasa akitoka kwenye kikao kama hicho kisha arejee kwa wananchi anatamauka kwa kusikia kaulimbiu za kumkatisha tamaa kama vile ‘kazi ya mtu imtetee’, ‘endelea kulala tumekuzoea’, ‘utachaguliwa na bibi yako’ na kadhalika.
Kumbe tatizo ni kwamba alinata kwa Wamunyoro kama kupe anavyonata kwenye ngozi ya ng’ombe, akafyonza damu mpaka ng’ombe anapochinjwa na ngozi yenyewe kuanikwa juani!
Hatima sawa na hiyo inawasubiri wanaomfuata Kasongo kokote anakokwenda, lakini hao walijua tangu mwanzo kwamba bunge au majumba rasmi ya magavana watayaona paa baada ya Uchaguzi Mkuu ujao.
Watafyekwa wote kama nyasi, watupwe kwenye pipa la takataka na lifunikwe ili wasinuke kwa miaka mitano! Mlimani hakuna huruma ya siasa.
Mwanasiasa yeyote mwenye akili timamu, na ni wachache mno enzi hii, hana haja ya kutetea wadhifa wake ikiwa anauza sera za Kasongo Mlimani.
Huko ni kutupa pesa mtoni ambapo maji yanakwenda kasi! Yatazimeza tu, nawe ubaki hapo ukiduwaa. Na utachekwa kila mahali, hata ukienda baa kukamata moja au mbili unaambiwa uende ukanywe chai kwa mkeo!
Kasongo mwenyewe, mweledi wa siasa zetu, anajua mlimani hana lake, ndiyo maana hajali hata viongozi wa kitaifa wa chama cha Yuda wakitoleana makucha na kulana maini hadharani.
Wakifanya hivyo wanampa kisingizio cha kudai alijaribu kusaidia Mlima, lakini marafiki zake kutoka huko wakamwangusha.
Sasa, hata ingekuwa wewe, ungefanyaje ukiangushwa? Unasalimu amri na kumwacha nguruwe ajikaange kwa mafuta yake mwenyewe.
Katika uchaguzi ujao, kuchaguliwa tena mlimani kunapaswa kuorodheshwa miongoni mwa mambo magumu yanayotabirika kwa wepesi kama Mkenya kuingia Tanzania na kutoka bila kulawitiwa!