Jamvi La Siasa

Miradi ya Ruto Nyanza ikikamilika kabla ya 2027 Upinzani mashakani -Wadadisi

Na CECIL ODONGO March 23rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ZIARA ya siku tano ya Rais William Ruto na ile ya siku nne Luo Nyanza iliyojaa miradi huenda imesambaratisha juhudi za Upinzani na Linda Mwananchi kupata uungwaji mkono eneo hilo kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.

Kwa miaka kadhaa, maeneo ya Nyanza na Magharibi yamekuwa chini ya himaya ya aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga ambaye aliaga dunia mnamo Oktoba 15 mwaka jana.

Kutokana na kutokuwepo kwake, kumekuwa na hofu kwamba maeneo hayo mawili ambayo yamekuwa yakitawaliwa na ODM, yatakuwa mayatima kisiasa na kugawa kura zao.

Rais Ruto alitamatisha ziara yake ya siku nne Luo Nyanza mnamo Jumapili na atakuwa na ziara nyingine Gusii kuanzia Machi 29 hadi Machi 31 huku akilenga kulemaza upinzani kabisa.

Akiwa Magharibi mwa Nchi , Rais alizindua miradi ya mabilioni ya hela katika kaunti za Vihiga, Kakamega, Busia na Bungoma.

Mnamo Jumamosi Rais Ruto na mwenzake wa Uganda Yoweri Museveni walizindua ujenzi wa reli ya kisasa ya kilomita 107 kutoka Kisumu-Malaba.

Ujenzi huo utakamilisha ujenzi wa reli ya kilomita 1000 kutoka Mombasa-Malaba na kuunganisha ile ya Malaba hadi Kampala.

Ni akiwa Magharibi ndipo Rais Ruto aliwakashifu viongozi wa upinzani kwa matamshi makali na kuwalazimu baadhi yao kujitetea.

Wanasiasa hao walidai kuwa matamshi ya Rais yalidunisha na kushusha hadhi ya afisi yake.

“Tumeanza kuwaaibisha washindani wetu kwa kuonyesha miradi ya maendeleo kila upande wa Kenya. Tunataka kuhakikisha kuwa kuna usawa wa maendeleo kila sehemu ya nchi,” akasema Rais Ruto akiwa Kisumu.

“Nataka kuwaambia washindani wetu kuwa mabadiliko nchini yapo kwenye mizani tofauti. Ningependa kuwaambia tuko tayari, kadi zetu za kupiga kura ziko tayari na wakati ukifika, tutakuwa tayari,” akaongeza kiongozi wa nchi.

Mnamo Februari 21, Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna, Gavana wa Siaya James Orengo na Mbunge wa Embakasi Babu Owino, walihutubia mkutano mkubwa uwanja wa Amalemba. Mkutano huo ulikuwa wa kusawiri eneo hilo kama linalochangamkia eneo hilo kisiasa.

“Hili vuguvugu ni kubwa, ni tsunami. Halisimami na hakuna nguvu duniani ambazo zinaweza kusimama mbele yetu. Serikali ijiandae kwa vuguvugu hili la raia,” akasema wakati wa Mkutano wa Linda Mwananchi Busia.

Mwezi uliopita, kundi hilo liliongoza kampeni kali Busia na Siaya ambapo walidai utawala wa Rais Ruto haujasuluhisha changamoto za Wakenya.

Mbali na Linda Mwananchi, Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya ameonekana kuwa sura ya upinzani Magharibi kupitia vuguvugu lake la ‘Tawe’.

Kwa mujibu wa mchanganuzi wa Masuala ya Kisiasa Martin Andati, upinzani sasa una mlima wa kuukwea hasa iwapo miradi iliyozinduliwa itakuwa imekamilika au kufikia hatua ya muhimu 2027 ikikaribia.

“Miradi hii inatekelezeka lakini baadhi yake gharama ni ya juu mno. Hatuwezi kusherehekea sana ilhali kutakuwa na mzigo mkubwa wa deni hata kwa kizazi kijacho,” akasema Bw Andati.

“Upinzani unajua kuwa uchaguzi haushindi tu kwa miradi pekee bali pia propaganda. Sasa lazima watafute mbinu nyingine za kumlemaza Rais Ruto kwa sababu miradi hii ikifaulu, Nyanza na Magharibi ambazo zimebaguliwa kwa miaka mingi, zitamchagua tena,” akasema Bw Andati.