Jamvi La Siasa

Mtihani kwa Babu mbio za ugavana Nairobi

Na CECIL ODONGO April 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

MBUNGE wa Embakasi Kusini, Babu Owino, anakabiliwa na maamuzi magumu katika azma yake ya kuwa gavana wa Nairobi 2027 huku hatua atakayochukua ikitarajiwa kumjenga au kumbomoa kisiasa.
Mwakilishi huyo anayefahamika zaidi kama Babu aliingia bungeni mnamo 2017 akimpiku aliyekuwa Mbunge Joseph Oguttu kupitia ODM.
Katika uchaguzi wa 2022 Babu alimbwaga Francis Mureithi wa chama cha UDA, japo ushindani mkali ulishuhudiwa na hata wafuasi wa wanasiasa hao walikabiliana vikali mara si moja.
Kabla kuingia bungeni Babu alikuwa kiongozi wa wanafunzi chuoni kwa miaka mingi na ni kati ya wanasiasa wasomi nchini, huku pia sasa akihudumu kama wakili.
Ni kati ya wabunge ambao walitegemewa na marehemu Raila Odinga kudhibiti na kuvumisha umaarufu wake katika jiji kuu Nairobi.
Mara si moja mbunge huyo amekuwa na utata na sheria, akikamatwa na kuzuiliwa. Lakini hilo limemzolea umaarufu mkubwa wa kisiasa hasa miongoni mwa vijana jijini Nairobi.
Ingawa hivyo, safari ya kisiasa ya Babu Owino ya kutwaa ugavana Nairobi huenda isiwe rahisi licha ya kampuni mbalimbali za utafiti kumweka mbele ya gavana wa sasa Johnson Sakaja na wagombeaji wengine.
Babu ni kati ya wanasiasa wanaoegemea mrengo wa Linda Mwananchi unaoongozwa na Katibu wa ODM, Edwin Sifuna, Gavana wa Siaya James Orengo na Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi.
Wanasiasa hawa wanapinga ule mrengo wa ODM unaoongozwa na kinara wa chama Dkt Oburu Oginga, ambaye ni nduguye marehemu Raila.
Aidha, alionekana kuwa na ukuruba wa karibu na chama cha Wiper chake Kalonzo Musyoka kabla ya kuchipuka kwa mrengo wa Linda Mwananchi.
“Sidhani kama uteuzi ODM utakuwa huru kwa sababu ya ushirikiano wa chama na Gavana Sakaja. Inashangaza kuwa wakati ODM ilikuwa na mtihani nilikuwa natafutwa lakini sasa mambo yamewanyonyokea napigwa vita,” akasema Bw Owino kwenye mahojiano na Radio Nam Lolwe mwezi uliopita.
Ukuruba wa Gavana Sakaja na ODM ulianza mapema 2025 wakati azma ya Raila ya kuwania uenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika (AUC).
Inaonekana tayari ODM inaendelea na maisha bila Bw Owino ambaye pia anapinga utawala wa Rais William Ruto kuchaguliwa tena na pia ushirikiano wa chama na UDA.
“Babu aliniambia kwenye afisi yangu kuwa hawezi kuwa upande wetu kwa sababu analenga kura za Mlima Kenya na Ukambani. Hata hivyo, nilimshauri kuwa hata hizi zetu atazipoteza kwa hivyo uamuzi ni wake ila namtakia kila la kheri,” akasema Dkt Oginga akijibu madai ya mbunge huyo kuwa ametalikiwa na ODM.
“Upande wa kisiasa ambao yupo pia ataponzwa kwa sababu hao hawapigi hesabu na yeye na wana watu wao,” akaongeza.
Huenda Bw Owino anahofia kusalia ODM na kushiriki mchujo kwa sababu duru zinaarifu kutakuwa na maelewano kati ya UDA na ODM kuhusu viti vya Ugavana, Useneta na Mbunge Mwakilishi wa Kike.
Aidha anahofia tukio ambalo hatapata tikiti jinsi ilivyomfanyikia Mbunge wa Westlands Tim Wanyonyi mnamo 2022 baada ya uongozi wa ODM kumshawishi ajiondoe na aunge mkono Polycarp Igathe licha ya umaarufu wake.
Ingawa hivyo, kambi ya upinzani nao pia inajipanga baada ya aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua kutangaza kuwa wataelewana na Wiper kuhusu kiti cha ugavana na viti vingine ili wawe na wawakilishi wengi kwenye uchaguzi wa 2027.
“Tuko na makubaliano na Kalonzo ambaye amekuwa akisaidia ODM Nairobi. Mkataba huo ni kuwa na Gavana, Seneta na Mbunge Mwakilishi wa kike kutoka DCP.
Pia tunalenga kuwa na wabunge 16 kati ya 17 kwenye muungano wetu,” akasema Bw Gachagua mnamo November 25 mwaka jana baada ya chama hicho kushinda udiwani Kariobangi.
Kauli hii ina maana kuwa iwapo Bw Owino ataamua kufanya kazi na upinzani basi lazima ajiunge na DCP na kupambana na Mbunge wa Embakasi Kaskazini James Gakuya ambaye anaungwa mkono na Bw Gachagua.
Bw Gakuya amehudumu kama mbunge wa eneo hilo tangu 2013 na analenga ugavana ambao umechenga jamii ya Mlima Kenya tangu 2013 licha ya idadi yao kubwa jijini.
Aidha, Babu Owino anaweza kutoegemea mrengo wowote kisiasa na kujivunia kura za vijana ambao wengi wao wanamuunga mkono.
“Tatizo ni kuwa siasa za jiji huwa na miegemeo ya kikabila na lazima atajitokeza hadharani kumtangaza anayempigia upato kuwania urais. Ni vigumu kushinda ugavana bila kuwa na mgombeaji wa urais unayemuunga mkono kwa sababu ya hadhi ya kiti cha ugavana na pia uchumi wa Nairobi,” akasema Mchanganuzi wa Masuala ya kisiasa Martin Andati.
Iwapo atagombea kama mwaniaji huru na kushinda basi atakuwa wa kwanza kufanya hivyo tangu 2013 baada ya Evans Kidero wa ODM, Mike Sonko wa Jubilee na Bw Sakaja ambaye sasa anagombea kupitia UDA.
Japo Mbunge wa Makadara George Aladwa ametangaza kuwa pia analenga ugavana wa Nairobi kupitia ODM, haonekani kuwa na uzito wa kisiasa kama Babu Owino.