Seneta Lelegwe alazimika ‘kujiosha’ lawama za kuhujumu Seneta Hezena
SENETA wa Samburu, Lelegwe Ltumbesi, alilazimika kujitetea vikali dhidi ya madai yaliyotolewa na mwenzake, Seneta Maalum Hezena Lemaletian, kwamba anaongoza juhudi za kuhujumu wanawake katika siasa za kaunti hiyo.
Mnamo Ijumaa, Seneta Lelegwe alikanusha madai hayo akisema hayana msingi wowote, na kudai kuwa jina lake linatumiwa kisiasa na wanasiasa wanaotafuta umaarufu miongoni mwa wapiga kura.
“Napinga kwa nguvu simulizi yoyote, iwe ya wazi au ya imefichwa, inayojaribu kuonyesha kuwa Samburu ni kaunti inayowachukia wanawake katika uongozi. Tangu kuanzishwa kwa ugatuzi, Samburu imewapa wanawake fursa sawa. Wananchi wamechagua mbunge mwanamke katika eneo la uwakilishi kwa mihula miwili mfululizo. Hivi majuzi pia, mwanamke alichaguliwa katika uchaguzi mdogo wa wadi ya Angata Nanyekie,” alisema.
Seneta huyo, ambaye yuko katika muhula wake wa pili, alidai kuwa joto la kisiasa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027 limechochea wanasiasa wanaohangaika kupata umaarufu kutumia mitandao ya kijamii kuchafua majina ya viongozi waliokita mizizi kisiasa, hususan ili kuwavutia vijana.
“Seneta mteule huyu si wa kiwango changu cha kisiasa. Wapinzani wangu wa 2027 ni aliyekuwa gavana na maafisa wawili wa kaunti,” alisema.
Aliongeza kuwa alishtushwa na madai hayo akisema ni ya uzushi na yanamsawiri kama mtu anayeweza kupanga vurugu dhidi ya mbunge mwenzake.
Kwa upande wake, Seneta maalum wa ODM, Hezena Lemaletian, amekuwa akimtuhumu Seneta Lelegwe kwa madai ya kutumia wahuni kuvuruga azma yake ya kisiasa na kuhatarisha maisha yake.
Alidai kuwa aliambiwa asilenge nyadhifa za juu kama ugavana au useneta bali aridhike na kiti cha mwakilishi wa wanawake au MCA.
“Iwapo jambo lolote litanipata, familia moja Samburu na washirika wake wa kisiasa wanapaswa kulaumiwa,” alisema.
Alidai familia hiyo iliwahi kumtishia marehemu babake na sasa imelenga kumdhuru yeye, ikiwemo kuvuruga uchumba wake, kueneza madai ya uongo mitandaoni na kutoa vitisho.
Seneta huyo alisema amewasilisha ushahidi wa vitisho hivyo kwa mamlaka husika na ataendelea kutafuta haki.
Hivi majuzi, Bi Lemaletian alitangaza kuvunja uchumba wake na kurejesha mahari, akisema uamuzi huo ulitokana na mila za Wasamburu na uchunguzi wa kina wa historia ya aliyekuwa mchumba wake.
Alisisitiza kuwa hana nia ya kuolewa na mtu huyo.