Timamy azua joto kutaka mwandani kumrithi 2027
SIASA za kumrithi Gavana wa Kaunti ya Lamu Issa Timamy zimepamba moto huku zaidi ya wagombea saba wakijitokeza wakiwemo waliowahi kuwa manaibu wa magavana na wanasiasa wengine tajika.
Gavana Timamy ambaye anachukua fursa ya kuwa kiongozi wa chama cha ANC ambacho kiko na mkataba na chama tawala UDA, anapata fursa hiyo kuanza kampeni za kumrithisha mwandani wake ili kuendeleza sera zake.
Ikizingatiwa kuwa chama cha ODM hakina wagombeaji shupavu ikilinganishwa na uchaguzi uliopita, Bw Timamy anategemea kuidhinishwa na Rais William Ruto kuongoza siasa eneo hilo jambo ambalo limepelekea kupinga amri ya mahakama iliyotolewa wiki jana kuwa ANC haiko kwa muungano wa UDA.
Bw Timamy amesistiza kuwa chama cha ANC kiko halali na yote yaliyotajwa mahakamani yalitatuliwa jambo ambalo litamweka kifua mbele kupigia debe wandani wake 2027.
Katika uchaguzi uliopita, chama cha ODM kilijidhihirisha kuwa kiko hafifu katika Kaunti hiyo hivyo kinampa Bw Timamy nguvu ya kuwa na usemi wa siasa za 2027.
Katika uchaguzi wa 2022, Timamy aliibuka mshindi kwa kura 24,198 kwa chama cha ANC akifuatwa na Fahim Twaha wa Jubilee kwa kura 16,054, Umra Omar wa Safina (7556) na Eric Mugo wa Narc-K kwa kura 2,151 huku mgombea wa ODM Omar Buno akirambishwa sakafu kwa kura chini ya kura 2000.
Huku mwaka wa 2027 unapowadia, na kipindi cha siasa kupamba moto, Kaunti ya Lamu inazidi kuvutia wanasiasa na wafanyibiashara kwa kiti cha ugavana wakiahidi kutekeleza yale magavana waliotangulia wameshindwa kutatua.
Bw Timamy ambaye anamaliza kipindi chake baada ya kuhudumu mihula miwili kikatiba, anaonekana kutaka kuendeleza uongozi wake kupitia kwa wandani wake.
Wiki hii, gavana Timamy baada ya kuchagua naibu wake kumpendekeza naibu wake, Dkt Mbarak Mohamed na aliyekuwa mbunge wa Lamu Magharibi Julius Ndegwa kumrithi ifikapo mwisho wa muhula wake.
Kuchagua viongozi hao kumezua tetesi mbalimbali kwani wawili hao ni wandani wake akiwa Bw Ndegwa kama mshauri katika ofisi ya Gavana Timamy.
Hata hivyo, Bw Timamy amesifiwa kwa kupendekeza wawili hao kwa kujaribu kuleta uwiano wa kidini na kikabila jambo ambalo limekuwa likisumbua wakazi wa kaunti hiyo.
“Lamu kumekuwa na mjadala wa uongozi kwa misingi ya dini na kabila, na jambo ambalo Timamy amefanya ni la msingi ili kuboresha umoja,” alisema Juma Shehe, mkazi wa Witu.
Licha ya yote, wakazi tayari wameweka vigezo vitakavyotumika kupiga msasa viongozi wakisema iko haja ya kutatua mambo ambayo yamekuwa yakikumba wakazi wa Lamu.
Bi Khadija Juma, katika mkutano wa uzinduzi wa kusajili wapigakura uliofanyika mapema Januari mwaka huu eneo la Mokowe, alisema sera ni mojawapo ya vigezo muhimu wakazi wataangalia wakati wa kupiga kura, sio dini, kabila au tabaka.
“Kiongozi ambaye ataleta suluhu la donda sugu la ardhi, uskwota, ukosefu wa hatimiliki za ardhi ataweza kupata uungwaji mkono mkubwa kwani hilo ni suala muhimu linaloathiri wakazi. Ukosefu wa ajira miongoni mwa vijana na njia za kupambana na dawa za kulevya ambazo zinaathiri vijana wengi Lamu nalo lazima liwe kwa sera ya wagombeaji,” alisema Bi Khadija.
Kinyang’anyiro hicho ambacho kimevutia zaidi ya wagombeaji saba kwa sasa; akiwemo mwanamke pekee Seneta mteule Shakila Abdalla akiwa mbioni kuchaguliwa gavana wa kwanza kwa kike Kaunti hiyo.
Kati ya waliojitangaza kugombea ni pamoja na aliyewahi kuwa gavana wa Lamu Fahim Twaha akiwaomba wakazi kumpa nafasi kukamilisha yale aliyoanza hapo awali kwa muhula 2017–2022 kabla ya kung’olewa na Bw Timamy.
Eric Mugo Kinyua, aliyewahi kuwa Naibu Gavana kati ya 2013–2017 wakati wa kipindi cha Bw Timamy cha kwanza, amejitangaza kama mgombea wa sera za maendeleo endelevu.
Wengine ambao wanatarajiwa kujitosa kwa kinyang’anyiro hicho ni katibu wa uekezaji Abubakar Hassan, aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa Tume ya Huduma ya Polisi ya Kitaifa Eliud Kinuthia ambaye alijikita katika haki, usalama na utawala bora pamoja na Stanley Muthama ambaye ni Mbunge wa sasa wa Lamu Magharibi.