Uhuru: Kazi yangu sasa ni kusikiliza wananchi, sina mambo mengi
RAIS mstaafu, Uhuru Kenyatta, amesema amerejea kijijini kwao Ichaweri na sasa anasikiliza maoni ya wananchi kama Wakenya wengine.
Bw Kenyatta alisema haya akikejeli wanaomhusisha na siasa alipohudhuria mazishi ya aliyekuwa seneta wa Kirinyaga marehemu Daniel Karaba.
“Mimo sina mengi ya kusema. Nilitoka kijiji chetu Ichaweri kuja hapa kumuaga rafiki yangu. Sikuvutiwa na mambo mengi, ni Karaba tu. Sitaki kusema mengi nisije nikaambiwa mimi ndiye niliwaleta watu hawa wote hapa,” alisema Uhuru.
Aliongeza: “Sijui Orengo alitoka wapi. Hata Kalonzo nilikuwa namuona tu kwenye televisheni kule Ukambani. Hata ndugu yangu Wamunyoro nilidhani angekuwa anaendelea na siasa zake mahali pengine. Nilidhani nitakuwa na dadangu Martha tu hapa, lakini tuko wote.”
Uhuru aliwataka Wakenya kuwasikiliza viongozi badala ya wanasiasa.
“Ni vyema watu wasikilize viongozi, si wanasiasa, kwa sababu wanasiasa wana ndimi tamu. Lakini niliwaambia msisahau,” alisema.
Alionya kuwa maneno matamu yanaweza kuwapotosha watu hata katika maamuzi muhimu ya maisha.
“Hata binti yako mdogo unayetarajia kuolewa na mtu msomi, unaweza kumuoza kwa sababu ya ndimi tamu,” aliongeza.
Alimsifu marehemu Karaba kwa kusimama kidete katika maamuzi yake licha ya misukosuko ya kisiasa.
“Karaba alisimama nami hata mawimbi ya siasa yalipokuwa yakielekea upande mwingine. Aliamua kusimama na uamuzi wake mwenyewe,” alisema.
Uhuru alisisitiza umuhimu wa uongozi kuwa wakweli na waadilifu.
“Njia bora ya kujenga taifa ni viongozi kusema ukweli na watu kuwa pamoja. Nchi yetu inahitaji viongozi waadilifu wanaowahudumia wananchi, si wanaojihudumia,” alisema.
Alisema kuwa amerudi kijijini kusikiliza sauti ya wananchi.
“Nilirudi Ichaweri, nasikiliza wananchi. Wanachotaka ni umoja,” alisema.
Uhuru aliongeza kuwa hana nia ya kuwania kiti chochote cha kisiasa.
“Mtakayemchagua, nitabaki Ichaweri. Sina shida. Mkikosea, ni juu yenu,” alisema.
Alionya dhidi ya siasa za kununua kura.
“Msikubali kuuza kura zenu. Pokea pesa ukitaka, lakini kura yako ujue utampa nani,” alisema.
Aidha, alikumbusha umuhimu wa umoja akisema alichotamani yeye na Raila Odinga ni kuona Kenya ikiwa pamoja.