Jamvi La Siasa

WALIOBOBEA: Mwachai, mbunge wa kwanza wa kike ukanda wa Pwani

Na BENSON MATHEKA March 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KATIKA historia ya siasa za Pwani ya Kenya, jina la Marere Mwarapayo wa Mwachai linatajwa akiwa mwanamke wa kwanza aliyethubutu kuvunja mipaka katika uongozi wa kisiasa.

Alijipatia umaarufu baada ya kuwa mwanamke wa kwanza kutoka eneo la Pwani kuchaguliwa kuwa mbunge, akiwakilisha eneo bunge la Msambweni kati ya mwaka 1997 na 2002.

Alivunja vizingiti katika siasa za Kenya wakati ambapo ulingo huo ulikuwa ukitawaliwa zaidi na wanaume, hatua iliyomweka katika historia ya kisiasa ya Pwani.

Kabla ya kuingia katika siasa, Mwachai alikuwa mwalimu. Kazi hiyo ilimpa nafasi ya kukutana na wananchi wa tabaka mbalimbali na kumfanya aelewe changamoto zinazowakumba hasa katika maeneo ya vijijini.

Kupitia uzoefu wake katika sekta ya elimu, alijenga hamu ya kushiriki katika uongozi ili kusaidia kuboresha maisha ya jamii aliyokuwa akiishi nayo.

Safari yake ya kuingia katika siasa haikuwa rahisi.

Mwaka 1992 alijaribu kwa mara ya kwanza kuwania ubunge katika eneo bunge la Msambweni lakini akashindwa na aliyekuwa mbunge wakati huo, Kassim Bakari Mwamzandi.

Hata hivyo, kushindwa huko hakukumvunja moyo.

Aliendelea kujihusisha na shughuli za kisiasa na kuimarisha uhusiano wake na wapigakura wa eneo hilo.

Hatimaye juhudi zake zilizaa matunda katika uchaguzi mkuu wa 1997 alipoibuka mshindi na kuwa mbunge wa eneobunge la Msambweni.

Ushindi huo ulikuwa wa kihistoria kwani ulimfanya kuwa mmoja wa wanawake wachache sana waliokuwa wamefanikiwa kushinda ubunge katika eneo la Pwani wakati huo.

Wengi waliona ushindi wake kama ishara kwamba wanawake wanaweza kushindana na kushinda katika siasa ambazo kwa muda mrefu zilionekana kuwa ngome ya wanaume.

Baada ya kuchaguliwa kuwa mbunge, Mwachai aliteuliwa kuhudumu serikalini kama Waziri Msaidizi katika Wizara ya Jinsia, Utamaduni na Huduma za Jamii.

Katika wadhifa huo alihusika na juhudi za kuimarisha ustawi wa jamii, kukuza haki za wanawake na kuendeleza masuala ya kitamaduni.

Wakati wa utumishi wake, alijulikana kwa kusisitiza umuhimu wa kuwapa wanawake nafasi zaidi katika uongozi na katika mipango ya maendeleo ya kitaifa.

Hata hivyo, kama ilivyo kwa wanasiasa wengi, safari yake pia ilikumbwa na changamoto.

Katika uchaguzi mkuu wa 2002 alijaribu kutetea kiti chake cha ubunge lakini akashindwa na Abdalla Jumaa Ngozi.

Kushindwa huko kulihitimisha muhula wake wa kwanza bungeni, lakini hakukufuta mchango wake katika siasa za Pwani.

Kwa muda mrefu pia alijulikana kwa kuwa mwaminifu kwa chama cha Kenya African National Union (KANU), hasa katika kipindi ambacho chama hicho kilikuwa kinakabiliwa na ushindani mkali kutoka kwa vyama vingine vya kisiasa.

Uaminifu huo ulimfanya aendelee kuwa sauti muhimu katika siasa za eneo la Pwani hata baada ya kupoteza kiti cha ubunge.

Leo, jina la Marerere wa Mwachai linatajwa kama mfano wa mwanamke aliyethubutu kuingia katika siasa wakati ambapo wanawake wachache sana walikuwa wakijaribu kufanya hivyo.

Kwa wakazi wa Msambweni na Pwani kwa ujumla, historia yake ni simulizi ya ujasiri, uvumilivu na azma ya kuvunja vikwazo katika uongozi.

Urithi wake unaendelea kuwahamasisha wanawake wengi kuwania nyadhifa za uongozi nchini, huku wengi wakimkumbuka kama mmoja wa wanawake walioweka msingi wa ushiriki mpana wa wanawake katika siasa za Kenya.