Makala

Kamati ya Bunge yaidhinisha uteuzi wa Erastus Edung na wenzake sita kusimamia IEBC

Na CHARLES WASONGA June 4th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MWENYEKITI mteule wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) Erustus Ethekon Edung na makamishna sita wateule wanakaribia kuteuliwa rasmi kushikilia nyadhifa hizo baada ya Kamati ya Bunge la Kitaifa kuhusu Sheria (JLAC) kuidhinisha uteuzi wao.

Akiwasilisha ripoti kuhusu shughuli ya kuwapiga msasa wateule hao saba, iliyofanyika Jumamosi Mei 31, 2025, mwenyekiti wa JLAC George Murugara alisema kamati yake iliridhika na ufaa wa watu hao kushikilia nyadhifa hizo.

“Kwa hivyo, kwa mujibu wa mahitaji ya Kipengele cha 252 (b) cha Katiba, kamati hii inaidhinisha uteuzi wa Erastus Ethekon Edung kuwa Mwenyekiti na Mary Njeri Nderitu, Moses Alutalala Mukhwana, Mary Karen Sorobit, Hassan Noor Hassan, Francis Odhiambo Oduol na Bi Fahima Arafat Abdallah kuwa wanachama wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC),” Bw Murugara, ambaye ni Mbunge wa Tharaka, akasema Jumanne alasiri.

Sasa kikao cha wabunge wote kinatarajiwa kujadili ripoti hiyo na kupiga kura kuunga mkono mapendekezo ya kamati ya JLAC au kuyakataa.

Endapo wabunge wataidhinisha ripoti hiyo, hatua hiyo itatoa nafasi kwa Rais William Ruto kuwateua rasmi Bw Edung na wenzake kisha waapishwe kuacha kazi rasmi.

Hata hivyo, wiki jana Jaji Mahakama Kuu Lawrence Mugambi aliamuru kwamba endapo bunge itaidhinisha uteuzi wa Bw Edung na wenzake sita, wasiapishwe hadi kesi iliyowasilishwa mbele yake kupinga uteuzi wao itakaposikizwa na kuamuliwa.

Majuma mawili yaliyopita Rais Ruto alipendekeza uteuzi wa Erastus Ethekon Edungu kuwa mwenyekiti wa IEBC kufuatia mapendekezo kutoka kwa jopo la uteuzi wa makamishna wa tume hiyo lililoongozwa na Kasisi Nelson Makanda.

Dkt Ruto pia alipendekeza uteuzi wa makamishna sita ambao ni; Ann Njeri Nderitu (kutoka kaunti ya Nyandarua), Moses Alutalala Mukhwana (Kakamega), Mary Karen Sorobit (Uasin Gishu), Hassan Noor Hassan (Mandera), Francis Odhiambo Aduol (Kisumu) na Fahima Arafat Abdallah kutoka kaunti ya Lamu.

Saba hao walipendekeza kwa uteuzi wakati ambapo presha ya uteuzi wa makamishna hao ilikuwa ikipanda ili waweze kuendesha chaguzi kadhaa ndogo, shughuli ya uanishaji wa mipaka ya maeneo wakilishi na usajili wa wapiga kuwa wapya.

Shughuli hizo muhimu zilikuwa zimekwama kutokana na ombwe la uongozi katika IEBC tangu Januari 17, 2023, muhula wa kuhudumu wa mwenyekiti wa zamani Wafula Chebukati na makamishna wa zamani Abdi Guliye na Boya Molu.

Awali, makamishna wengine wanne Juliana Cherera, Justus Nyang’aya, Francis Wanderi na Irene Masit walifutwa kazi kwa kupinga matokeo rasmi ya uchaguzi wa urais Agosti 14, 2022.