Kenya na Australia kuimarisha ushirikiano wa biashara na uchimbaji madini
Kenya na Australia zinatarajiwa kuimarisha ushirikiano wa pande mbili kupitia diplomasia ya mabunge, huku juhudi zikielekezwa katika kupanua ushirikiano katika sekta ya uchimbaji madini, biashara na uwekezaji.
Akizungumza katika majengo ya Bunge Alhamisi, Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula alisema nchi hizo mbili zitaendelea kuimarisha uhusiano wao wa muda mrefu huku zikichunguza fursa mpya za ushirikiano.
Wetang’ula alitoa kauli hiyo alipomkaribisha balozi wa Australia nchini Kenya Jenny Da Rin katika mazungumzo yaliyolenga kuimarisha ushirikiano kati ya nchi hizo mbili, hasa katika sekta ya madini.
Spika alisema Australia ina teknolojia ya hali ya juu katika uchimbaji madini pamoja na mfumo thabiti wa sheria unaosimamia sekta hiyo, akiongeza kuwa Kenya inaweza kunufaika pakubwa kwa kuimarisha ushirikiano huo.
“Kenya imepiga hatua kubwa katika kuanzisha Sheria ya Madini, na ushirikiano wa karibu kati ya nchi hizi mbili katika sekta ya uchimbaji madini unahitajika sana,” alisema.
Aliongeza kuwa Bunge la Kitaifa limeanzisha Kundi la Urafiki la Bunge kati ya Kenya na Australia ili kukuza diplomasia ya mabunge na kuimarisha uhusiano na Bunge la Australia.
Wetang’ula pia alisema Kenya imenufaika na sera za Australia zinazowarahisishia wanafunzi kupata visa pamoja na programu za ufadhili wa masomo ambazo zimewezesha Wakenya wengi kusoma katika vyuo vikuu vya Australia.
“Katika mazungumzo yetu tulikubaliana kuendelea kuimarisha diplomasia ya mabunge kati ya nchi hizi mbili kupitia ushirikiano wa mara kwa mara kati ya makundi yetu ya urafiki ya mabunge,” alisema.
Aidha, alibainisha kuwa Tume ya Biashara na Uwekezaji ya Australia ilihamisha kitovu chake cha kikanda kutoka Afrika Kusini hadi Nairobi mwaka 2017, hatua iliyoashiria kuimarika kwa uhusiano wa kiuchumi kati ya nchi hizo.
Miradi kadhaa ya pamoja ya utafiti wa kilimo pia inaendelea. Kituo cha Australia cha Utafiti wa Kimataifa wa Kilimo kinashirikiana na taasisi za Kenya kukuza kilimo kinachostahimili mabadiliko ya tabianchi na kuongeza uzalishaji kupitia mbegu zinazostahimili ukame.
Mradi wa thamani ya Sh287 milioni uliozinduliwa Februari 2025 pia unalenga kusaidia kurejesha ardhi iliyoharibika na kuimarisha kilimo kinachostahimili
Kwa upande wake, Balozi Da Rin alisema uhusiano kati ya Kenya na Australia unaendelea kuwa mzuri, lakini akasisitiza haja ya kuimarisha ushirikiano zaidi.
“Nawahimiza maafisa wa nchi hizi mbili kuendelea kushirikiana kwa manufaa ya mataifa yetu. Hii itaimarisha diplomasia ya mabunge na kuongeza ushirikiano wa kiuchumi,” alisema.
Aliongeza kuwa Australia inaendelea kujitolea kusaidia wanafunzi wa Kenya wanaotaka kusoma katika vyuo vikuu vya Australia.
Kulingana na rekodi za Wizara ya Masuala ya Kigeni na pamoja na Wizara ya Uwekezaji, Biashara na Viwanda, Kenya ilisafirisha bidhaa zenye thamani ya takriban dola milioni 35.3 kwenda Australia mwaka 2023, huku ikiagiza bidhaa zenye thamani ya dola milioni 118 kutoka nchi hiyo.
Bidhaa kuu zinazouzwa kutoka Kenya ni chai, kahawa, bidhaa za samaki, maua yaliyokatwa na ngozi, huku bidhaa zinazoagizwa kutoka Australia zikijumuisha ngano, mtama, mashine maalum na vifaa vya mawasiliano.