Makala

Kibarua cha Ruto kupambana na unyanyasaji na mauaji ya wanawake

Na WINNIE ONYANDO June 29th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

JUHUDI za serikali ya Rais William Ruto kupambana na unyanyasaji wa kijinsia (GBV) na mauaji ya wanawake zinaonyesha mwelekeo usioridhisha siku 1000 akiwa madarakani.

Kenya imeshuhudia ongezeko kubwa la visa vya mauaji ya wanawake, huku mwaka wa 2024 ukirekodiwa kuwa mwaka mbaya zaidi katika historia ya taifa hili.

Kwa mujibu wa ripoti ya hivi karibuni  “Silencing Women” visa 170 vya mauaji ya wanawake viliorodheshwa katika kipindi cha miezi 12 kufikia Januari mwaka huu – ongezeko kubwa ikilinganishwa na miaka ya awali.

Licha ya ahadi kadhaa zilizotolewa na serikali yake, changamoto bado zinaonekana katika ufadhili, utekelezaji, na mageuzi ya mifumo.

Akizungumza na Taifa Leo, Rachael Omollo, mtaalamu wa sera za umma na utawala, anasema kuwa serikali imepanua vituo vya kushauri waathiriwa wa GBV na kuunda jopo kazi ya kushughulikia mauaji ya wanawake.

Hata hivyo, juhudi hizi zimekosa ufadhili wa kutosha na mwelekeo unaofaa.

“Hizi zote ni hatua nzuri, lakini ukosefu wa fedha na huduma duni kwa waathiriwa ni changamoto kubwa,” anasema Bi Omollo.

Kando na hayo, anasema kuwa Idara ya Mahakama iliunda korti maalum za kushughulikia kesi za GBV  mwaka wa 2023, lakini utekelezaji wake bado ni dhaifu.

Naye Amondi Aroko, mtaalamu wa jinsia na maendeleo aliambia Taifa Leo kuwa mpango huu haujaambatana na mafunzo ya kutosha kwani maafisa, wahudumu wa afya, na washauri walio katika nafasi hizi hawana tajriba ya kutosha.

“Mswada wa mauaji ya wanawake unaweza kuwa suluhu muhimu, lakini bila sheria hiyo, waathiriwa wataendelea kuathirika,” Bi Aroko anasisitiza.

Kwa upande mwingine, upatikanaji wa huduma za afya ya uzazi bado ni tatizo, hasa katika maeneo ya vijijini ambapo unyanyapaa wa kitamaduni na ukosefu wa miundombinu ya afya vimeenea.

“Wale wanaopata watoto wakiwa na umri mdogo mara nyingi hukosa msaada wanaohitaji, jambo linalowaathiri zaidi,” Bi Omollo alieleza.

Ingawa sera za kupambana na ukeketaji wa wasichana (FGM) zipo, utekelezaji wake hauridhishi, hasa katika maeneo ya mashinani.

Wanawake wa mashinani, ambao wanaathirika zaidi, hawajanufaika kwa kiasi kikubwa kutokana na ukosefu wa usambazaji mzuri wa rasilimali.

Wanawake wanaoishi na ulemavu na wale walioko katika maeneo kame au ya vijijini pia wameachwa nyuma.

 “Licha ya hotuba za ushirikishwaji, wanawake wa mashinani—hasa vijijini—wanahisi kutengwa,” Bi Aroko anasema.

Japo utawala wa Rais Ruto umeunda jopo kazi kushughulikia GBV na mauaji ya wanawake, Bi Omollo anasema kuwa vyombo hivi vinakosa mamlaka na rasilimali za kutekeleza majukumu yao kikamilifu na kwa ufanisi.

“Kuunda jopo kazi ni hatua muhimu sana lakini bila matokeo tunaviona kama vyombo visivyo na nguvu,” anaonya.

Wataalamu hao wanakubaliana kuwa mageuzi ya mifumo ni ya dharura. Bi Omollo anasisitiza kuwa kushughulikia GBV na mauaji ya wanawake kunahitaji mfumo thabiti na unaofadhiliwa ipasavyo.

“Ufadhili wa moja kwa moja kwa mipango ya GBV, huduma bora kwa waathiriwa, na mifumo madhubuti ya utekelezaji ni muhimu,” anasema.

Naye Bi Aroko anasisitiza umuhimu wa kupitisha mswada wa kina wa mauaji ya wanawake ili kulinda wanawake na wasichana.

“Ni lazima tuweke kipaumbele sheria zinazowawajibisha wahalifu huku tukiwasaidia waathiriwa kwa njia inayofaa,” anasema.

Kwa upande wake, Javas Bigambo, mtaalamu wa utawala, anatoa wito umma uelimishwe na ushirikiano wa kisiasa ili kuziba pengo la kijinsia.

“Mapambano dhidi ya GBV si suala la serikali pekee—yanahitaji ushirikiano kati ya vyama vya kisiasa, asasi za kiraia, na umma kwa jumla,” Bw Bigambo anasema.