• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 6:50 AM
Kufunga baa kwasambaratisha kazi 93,250 za mahasla

Kufunga baa kwasambaratisha kazi 93,250 za mahasla

NA MWANGI MUIRURI

WAMILIKI wa baa katika ukanda wa Mlima Kenya wamelalamika kwamba kufungwa kwa sehemu hizo kumepotezea mahasla wa eneo hilo takriban kazi 50,000.

Mwenyekiti wa muungano wa wamiliki hao Bw David Kiama alisema Jumatano kwamba huku taifa likisherehekea Leba Dei ambayo huhusishwa na uimarishaji wa mazingira ya wafanyakazi, Mlima Kenya ni kilio tu.

“Kati ya baa zote 18,650 ambazo zilifungwa kote nchini, baa 10,000 zilikuwa za eneo hili,” akasema Bw Kiama.

Aliongeza kwamba watu 93,250 walipoteza ajira kote nchini.

Alisema hitilafu kuu ya vita hivyo ni kwamba hakuna nafasi za kazi mbadala zilizoundwa ili kuwachukua waliokuwa wakifurushwa kutoka kwa baa hizo.

“Ukizingatia kwamba wahudumu wa baa waliokuwa wakifurushwa ni wasio na taaluma, ilihitaji kwanza kuwekwe viwanda vya kuwachukua kama vibarua,” akasema.

Bw Kiama alisema serikali ya Rais William Ruto iliingia mamlakani ikisema kwamba inazingatia masilahi ya wanyonge wa mashinani na kuwabandika jina mahasla.

“Sasa mahasla ndio hao wametimuliwa kazini pasipo kuonyeshwa njia nyingine ya kujinusuru. Wanawake walio na watoto hata shuleni walifurushwa hadi nje ya ajira halafu tunasema kuna sherehe za Leba Dei,” akasema.

Alisema kwamba kusema serikali inajenga nyumba za bei nafuu na pia kutoa fatalaiza sio suluhu ya waliofurushwa kutoka kazi za baa.

“Kazi ya mjengo sanasana huwafaa wanaume. Wahudumu wengi wa baa ni wanawake. Aidha, askari rungu wanaolinda baa hizo ni wazee ambao hawawezi kufanya mjengo. Nacho kilimo ni cha walio na mashamba na mtaji. Hakuna afueni kwa waliopoteza ajira ya baa,” akasema.

Mrengo wa Azimio La Umoja-One Kenya eneo la Mlima Kenya tayari umetoa taarifa kwamba serikali ya Rais Ruto haikuzingatia hali kwamba baa sio tu mahali pa kuuzia pombe, bali pia huwa ni soko kubwa linalowapa wengi riziki.

Aliyekuwa mbunge wa Ndaragwa Jeremiah Kioni alidai kwamba serikali inaenda kinyume na ahadi ambazo ilitoa.

“Walidai kwamba utawala wa Rais mstaafu Uhuru Kenyatta ulikuwa ukidhulumu watu wa chini katika biashara. Wakatuambia kwamba hakuna riziki ya mtu itawahi kufungwa lakini sasa wanapiga vita riziki za wengi,” akasema Bw Kioni.

Katibu huyo mkuu wa chama cha Jubilee alisema Naibu Rais Rigathi Gachagua ambaye amezindua vita dhidi ya pombe haramu na kulenga utundu wa wamiliki wa baadhi ya baa, anafaa kujifahamisha kwamba biashara ya baa huwa ni soko kwa wachuuzi chungu nzima na ambao sasa wanaumizwa kwa msingi wa kupambana na ulevi.

“Sisi watu wa Azimio tunaunga mkono vita dhidi ya pombe haramu lakini hatuungi mkono kufungwa hata kwa baa moja isipokuwa ile ambayo imedhihirisha ukosefu wa maadili kabisa hasa kwa kuuzia watoto pombe,” akasema.

Alimtaka Rais Ruto na Bw Gachagua wajumuike mashinani na wajifahamishe na hali halisi ya mahasla wakiwa ndani ya baa kuchuuza bidhaa zao wala sio kunywa pombe.

“Ile dhana ambayo serikali iko nayo kwamba pombe itaisha kupitia kufunga baa na kuwakamata walevi, ni mtazamo usio na mashiko. Kile ambacho inafaa kufanya ni kuweka mikakati ya kuhakikisha upishi wa pombe au utengenezaji wake unafanywa kwa kuzingatia usafi na ubora wa hali ya juu ili bidhaa inayofika sokoni iwe salama,” akasema.

Aliongeza kwamba mkakati mwingine ni serikali kuzima mianya ya baa kupata pombe haramu.

“Waache kuja tu na kuamuru wafanyabiashara kufunga baa,” akasema.

Naye aliyekuwa Waziri Msaidizi (CAS) katika wizara za Spoti na Elimu Bw Zack Kinuthia alisema kwamba ukifunga baa, unamfungia riziki mwekezaji na wahudumu wake.

“Isitoshe, utakuwa umewafungia wengine wengi ambao hutegemea kufunguliwa kwa milango ya baa ndipo wapate chakula cha kila siku,” akasema.

Bw Kinuthia alisema baa moja ya kiwango cha chini kabisa hutoa nafasi tano za kazi, zikiwa ni mwekezaji, mhudumu wa kaunta, mhudumu wa wateja, soja na mtekelezaji usafi.

“Hii ina maana kwamba kila baa inayoamrishwa ifungwe kuna kazi zisizopungua tano ambazo serikali inaua,” akasema.

Mwenyekiti wa muungano wa baraza la wazee Wachira Kiago ameteta kwamba vita hivyo vya kufungisha baa zinaathiri uchumi mashinani kwa kiwango kikuu.

“Baa ikiwa haiko karibu na shule, hospitali au eneo la ibada, haifai kuambiwa ifungwe. Ukipokonya mhudumu wa baa leseni yake kwa msingi kwamba watu wanakunywa pombe haujasuluhisha lolote,” akasema.

Alisema wazee wanaunga mkono vita dhidi ya pombe ya mauti “na ni msimamo wetu kwamba taka hizo za kukera hazitengenezewi ndani ya baa”.

Bw Kiago aliteta kwamba wachuuzi wa mayai ‘boilo’, njugu, nguo, viatu, bidhaa vya ujumla, madalali wa kushirikisha dili, wauzaji kahawa, samosa, matunda, dawa za mitishamba, vitabu, mifugo kama sungura na kuku, samaki na kadhalika huwa wanategemea pakubwa biashara ya baa kujishindia wateja.

Wengine hasa katika baa zilizo na lojing’i huwa wanachuuza bidhaa muhimu za matumizi ndani ya baa.

Mwenyekiti wa muungano wa wasanii Mlima Kenya Epha Maina alisema Kuna baa ambazo zimefungwa na zilikuwa zinaandaa shoo ambazo huwapa wasanii husika riziki yao bila kusahau waandalizi wa nyama nje ya vilabu hivyo.

“Unafunga baa na kwa mpigo unamnyima msanii nafasi ya kuandaa shoo. Hivi vita vya pombe vinafaa vipigwe msasa na ieleweke kwamba kufunga baa sio kumaliza pombe ya mauti. Pombe hii hata inaweza ikaandaliwa kwa boma la mtu binafsi au kwa vichaka. Katika hali hiyo pia utasema tufunge maboma yetu na pia vichaka?” awaza msanii Ben Githae.

Bw Githae alisema kwamba “kila mtu aliyeenda shule anasema kwamba kuzima pombe ya mauti kutafaulu tu iwapo serikali itazima kupatikana kwa malighafi na viwanda haramu wala sio kupitia kufunga baa”.

Bw Maina alisema kwamba “sisi kama wasanii tunaenzi sheria na pia usalama wa watu katika hali zote na kamwe hatuungi mkono ulevi kiholela…lakini tutilie maanani kwamba biashara ya baa sio haramu nchini”.

Wahudumu wa bodaboda, teksi na tuk tuk pia wanasema kila baa huwa ni mwanya wa kupata wateja hasa kuanzia masaa ya usiku.

“Walevi wengi hutafuta huduma za uchukuzi kufika kwao nyumbani. Kufunga baa ni sawa na kumalizia watu wa bodaboda nafasi za kuhudumu. Ni kama hii serikali iko kwa vita na wanaojitafutia katika mitaa kama mahasola,” akasema Bw Kamande Ngoru, mhudumu wa teksi Mjini Murang’a.

Kwa upande wao, vibiritingoma mitaani walisema kwamba baa ndizo shamba lao la kuvuna wateja huku nao baadhi ya wachungaji wa kuhamahama wakisema huwa wanahubiri ndani ya baa kuponya nyoyo za wanaohangaika na mengi ya dunia na kupata sadaka.

Aidha, ombaomba walioongea na Taifa Leo walihofia kwamba vita vya baa ni sawa na kuwafungia milango ya kugongagonga wakisaka wahisani.

[email protected]

  • Tags

You can share this post!

Stephen Letoo aachana na kitimoto cha Men’s Conference

Vituo vya petroli vinavyoogelea maji ya mafuriko vifungwe...

T L