Kosa la kudondosha irabu katika kuandika maneno ya Kiswahili
KISWAHILI ni lugha ya Kibantu ambapo aghalabu maneno huundwa kwa kutumia konsonanti na irabu.
Ili mwanafunzi aweze kutamka na kuandika maneno ya Kiswahili kwa usahihi, sharti atambue na kutamka ipasavyo silabi zilizoundwa kutokana na sauti za herufi mbalimbali za Kiswahili.
Wapo wanafunzi wanaokumbwa na changamoto ya kudondosha irabu wanapoandika baadhi ya maneno ya Kiswahili.
Kosa hili hasa hutokea katika maneno yenye irabu moja inayorudiwa.
Kwa mfano, kuandika neno *kitungu badala ya kitunguu. Mwandishi wa neno hili amedondosha irabu ya mwisho -u imbayo imerudiwa katika neno kitunguu.
Makosa ya kudondoa au kuondoa irabu moja katika neno hasa pale irabu hiyo inaporudiwa kwa mfuatano hubadilisha muundo wa sauti.
Pia hupotosha maana ya neno na kusababisha matamshi na maandishi yasiyo sahihi. Mfano: Ukanusho wa – Analia ni halii.
Iwapo mtu atakanusha kwa kudondosha -i moja, neno hilo litakuwa hali.
Hapa atakuwa amewasilisha maana tofauti na aliyokusudia.
Aghalabu utapata sentensi kama vile: Baba alinunua *motoka jana.
Mpishi huyo *alianda chakula kitamu. Shangazi yangu amefunga *kitamba kichwani.
Sentensi hizi zina makosa ya kudondoshwa kwa irabu moja katika baadhi ya maneno.
Maneno mengine ambayo baadhi ya wanafunzi hudondosha irabu inayorudiwa ni: *migu badala ya miguu.
Mwanafunzi mwenye changamoto ya kudondosha irabu afanye mazoezi ya kutamka na kuyaandika maneno yenye irabu hizo kwa usahihi.