Makosa ya kudondosha viambishi vya idadi ya nomino katika wingi
KATIKA Kiswahili, upatanisho wa kisarufi ni muhimu tunapotaja idadi.
Mojawapo ya makosa yaliyozoeleka ni kuhesabu miezi bila kutumia kiambishi cha nomino ambacho ni mi-.
Ni kawaida kukutana na sentensi kama vile:
*Msimu huo mvua ilinyesha kwa mwezi tatu. Sentensi hii si sahihi. Nomino mwezi inamaanisha kipindi cha siku ishirini na nane hadi thelathini na moja.
Kwa hivyo katika wingi itakuwa miezi. Vilevile, kivumishi cha idadi tatu kinafaa kichukue kiambishi mi-. Ili kuisahihisha tutasema: Msimu huo mvua ilinyesha kwa miezi mitatu.
Makosa mengine yaliyozoeleka katika kuhesabu nomino ni kuvipa vivumishi tasa viambishi vya idadi: sita, saba, tisa na kumi.
Kila mara utakumbana na sentensi kama vile: Nilipofika darasani niliwapata wanafunzi *wasita. Vikombe *visaba vimeoshwa na mpishi.
Magari *matisa yameegeshwa. Miti *mikumi ilipandwa jana. Sentensi hizi si sahihi kwani zimetumia viambishi vya nomino mwanzoni mwa vivumishi sita, saba, tisa na kumi.
Tunafaa kuzisahihisha kwa kusema: Nilipofika darasani niliwapata wanafunzi sita. Vikombe saba vimeoshwa na mpishi. Magari tisa yameegeshwa. Miti kumi ilipandwa jana.
Kosa jingine la kawaida tunapohesabu nomino ni kukosa kutumia viambishi vya nomino tunapotaja vivumishi vya idadi vinavyobadilika katika wingi.
Aghalabu utakumbana na sentensi kama: *Nilinunua vitabu kumi na moja. *Wageni tano wamewasili kwetu.
Tunafaa kusema: Nilinunua vitabu kumi na kimoja. Wageni watano wamewasili kwetu.
Mwanafunzi mwenye changamoto ya kuhesabu nomino kwa usahihi, afanye mazoezi ya kuhesabu nomino ainati katika umoja na wingi.