Wito wa uwekezaji katika Kiswahili ili kisibaki nyuma kidijitali
ZAIDI ya wataalamu 200 wa lugha, wasomi, watengenezaji wa teknolojia na watunga sera kutoka kote Afrika Mashariki na Marekani (US) walikutana katika Chuo Kikuu cha Kisii wiki iliyopita kwa kongamano muhimu lililolenga kuhakikisha Kiswahili kinapata nafasi yake katika mustakabali wa kidijitali.
Kongamano hilo la Kimataifa la Chama cha Kiswahili Afrika Mashariki (CHAKAMA), lilijikita katika namna Akili Unde (AI), majukwaa ya kidijitali na teknolojia zinazoibuka zinaweza kutumiwa kukuza Kiswahili na kukiweka kama lugha yenye ushindani katika uchumi wa kidijitali duniani.
Waliohudhuria walijumuisha wasomi kutoka vyuo vikuu vya Afrika Mashariki na maafisa kutoka taasisi za lugha, wawakilishi wa mashirika ya serikali, mashirika ya kitamaduni, pamoja na wasomi kutoka vyuo vikuu vya Marekani.
Miongoni mwa wasomi mashuhuri waliohudhuria walikuwa Profesa Clara Momanyi wa Chuo Kikuu cha Kenyatta, mwandishi mashuhuri Profesa Kithaka Wa Mberia, mwandishi wa tamthilia na mtaalamu wa elimu Professa Chacha Nyaigoti Chacha, miongoni mwa wengine.
Akizungumza wakati wa kikao cha ufunguzi, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kisii, Profesa Nathan Ogechi, alisema mkutano huo ulikuwa umefanyika kwa wakati mwafaka, wakati ambapo Kiswahili kinapata kutambuliwa kimataifa kwa kiwango ambacho hakijawahi kushuhudiwa.
Mwaka 2021, shirika la UNESCO lilitangaza Julai 7 kuwa Siku ya Kiswahili Duniani, ikiwa ni mara ya kwanza kwa lugha ya Kiafrika kupewa hadhi hiyo ya kimataifa.
“Utambuzi huo haukutokea kwa bahati. Ulidhihirisha ukweli kwamba Kiswahili kimekua na kuvuka mipaka ya Afrika Mashariki na kuwa lugha ya diplomasia, biashara na utamaduni barani Afrika na hata nje ya bara,” alisema Profesa Ogechi.
Leo, zaidi ya watu milioni 200 huzungumza Kiswahili barani Afrika na katika jumuiya za watu wanaoishi ughaibuni. Lugha hiyo pia inafundishwa katika vyuo vikuu kote Ulaya, Asia na Amerika Kaskazini.
Ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Kiswahili ni lugha rasmi na ni kichocheo muhimu cha ushirikiano wa kikanda, biashara na diplomasia.
Hata hivyo, licha ya hadhi yake kuendelea kukua, wataalamu walionya kwamba Kiswahili kinaweza kuachwa nyuma katika ulimwengu wa kidijitali iwapo hatua za makusudi hazitachukuliwa.
Profesa Ogechi alieleza changamoto kadhaa zinazoikabili lugha hiyo katika enzi ya Akili Unde.
Changamoto hizo ni pamoja na ukosefu wa data ya kutosha kwa ajili ya kufundishia mifumo ya Akili Unde, rasilimali chache za kujifunzia kidijitali, ufadhili mdogo wa teknolojia ya lugha, pamoja na kuendelea kutawala kwa Kiingereza na lugha zingine za kigeni kwenye mitandao.
“Zana za kidijitali hazipaswi kututisha. Kwa kweli, ndizo fursa yetu kubwa zaidi ya kupanua Kiswahili. Lakini ili hilo litimie, ni lazima tuwekeze katika utafiti, data na majukwaa yanayozungumza lugha yetu,” aliongeza.
Mwandishi wa tamthilia na mtaalamu wa elimu kutoka Kenya, Profesa Chacha Nyaigoti Chacha, alisema Kiswahili kimebadilika kutoka kuwa lugha ya mawasiliano ya kikanda na kuwa mojawapo ya lugha zenye ushawishi mkubwa zaidi barani Afrika.
“Kiswahili kina utajiri mkubwa wa kimaana. Kina uwezo wa kusaidia utafiti wa kisayansi, ubunifu na uzalishaji wa maarifa. Kinachokosekana ni uwekezaji wa makusudi katika rasilimali za kidijitali ili kufungua uwezo huo,” alisema Profesa Chacha.
Alionya kwamba bila maudhui bora ya kidijitali, lugha hiyo itaendelea kutengwa katika ulimwengu wa mtandao, licha ya mamilioni ya vijana kutumia muda mwingi zaidi kwenye intaneti.
Kongamano hilo lilipata msukumo mkubwa siku ya Ijumaa wakati Waziri wa Elimu, Julius Ogamba, alipohudhuria kikao cha kufunga na kuahidi msaada wa serikali.
Bw Ogamba alisema Wizara ya Elimu itawasilisha pendekezo kwa Baraza la Mawaziri la kuanzishwa kwa Baraza la Kiswahili nchini Kenya.
Chombo hicho kinachopendekezwa kitakuwa na jukumu la kuratibu utafiti, sera na maendeleo ya teknolojia kwa ajili ya lugha hiyo.
“Hatuwezi kuruhusu lugha yetu ya kitaifa kuachwa nyuma katika mapinduzi ya kidijitali. Serikali iko tayari kushirikiana na vyuo vikuu, kampuni za teknolojia na taasisi za kikanda ili kuhakikisha Kiswahili kinaendelea kustawi mitandaoni,” alisema Waziri huyo.
Aliongeza kuwa kuunga mkono Kiswahili katika mazingira ya kidijitali pia ni suala la kuhifadhi utamaduni na kuunda fursa za kiuchumi kwa vijana.
Bingwa wa Kiswahili na Ushirikiano wa Kikanda barani Afrika, Dkt Caroline Asiimwe, alisema ushirikiano wa kikanda utakuwa muhimu iwapo Kiswahili kitastawi katika enzi ya kidijitali.
“Kusherehekea Siku ya Kiswahili ni muhimu, lakini ni lazima tuweke utafiti katikati ya juhudi hizi. Tunahitaji kuzalisha data ya lugha na kuishirikisha katika mipaka mbalimbali. Bila data, Akili Unde haiwezi kujifunza Kiswahili ipasavyo,” alisema.
Profesa Kithaka Wa Mberia, mwanaisimu mashuhuri, alisisitiza umuhimu wa kurekodi lahaja, misimu na matumizi ya kisasa ya lugha ili kufanya zana za Akili Unde kuwa na ufanisi zaidi.
“Akili Unde inayoelewa Kiswahili cha vitabu pekee itafeli. Tunahitaji kuilisha lahaja kutoka Mombasa, Zanzibar na Dar es Salaam. Hivyo ndivyo tunavyoweza kuifanya iwe halisi kwa vijana,” alisema Profesa Mberia.
Profesa Clara Momanyi alisema ushirikiano kati ya serikali, vyuo vikuu na kampuni za teknolojia lazima uharakishwe ili kuunda zana zinazoweza kutumika kwa vitendo.
“Tunahitaji kamusi za mtandaoni zinazofanya kazi, programu sahihi za kutafsiri, istilahi zilizosawazishwa kote duniani na mifumo ya kutambua sauti na miundo ya Akili Unde iliyofundishwa kwa Kiswahili. Mustakabali wa lugha hii uko katika teknolojia. Ikiwa hatupo kwenye majukwaa ya kidijitali, basi hatupo katika mazingira ambako vijana hujifunza na kubuni,” alisema Momanyi.
Dkt. Juliet Jagero, mwenyekiti wa CHAKAM na mhadhiri mkuu katika Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Jaramogi Oginga Odinga (JOOUST), aliwataka watayarishaji wa maudhui ya kidijitali kuwajibika.
“Kadiri Kiswahili kinavyoenea mitandaoni, ni lazima tuhakikishe maudhui tunayozalisha yanakuza umoja, maadili na misingi inayojenga na kuimarisha jamii zetu,” alisema.
Aliwataka waandishi na wataalamu wa vyombo vya habari kuunda maudhui zaidi ya Kiswahili kwa ajili ya hadhira ya vijana kupitia podikasti, blogu, tovuti za elimu na mitandao ya kijamii.
“Hivyo ndivyo tunavyoweza kuhifadhi lugha na wakati huo huo kuunda ajira katika uchumi wa kidijitali,” alisema Dkt Jagero.
Majadiliano hayo yanafanyika wakati ambapo Kiswahili kinaendelea kupata umaarufu katika diplomasia, elimu na biashara za kuvuka mipaka. Taasisi za kikanda na mashirika ya kimataifa zinazidi kutumia lugha hiyo katika mawasiliano yao.
Hata hivyo, wataalamu wanakubaliana kwamba hatua inayofuata ni teknolojia. Kuanzia roboti za mazungumzo hadi wasaidizi wa sauti na programu za kujifunza zinazotumia Akili Unde, lugha zitakazotawala zitakuwa zile zilizo na miundombinu bora zaidi ya kidijitali.
Kwa Kenya na Ulimwengu mzima, mkutano wa Kisii uliashiria mwanzo wa kile ambacho wajumbe wanatumaini kuwa juhudi endelevu za kuhakikisha Kiswahili hakizungumzwi tu, bali pia kinaandikwa kwa misimbo ya kompyuta, kinatafsiriwa na kueleweka na mashine.