Mbinu ya kinaya katika riwaya ya ‘Nguu za Jadi’
LEO hii tutarejelea umuhimu wa matumizi ya kinaya kwa kuangazia swali la muktadha ufuatao:
“Nimechoka ati. Ndio maana sikutaka kushinda. Mnajua kazi ya mtemi ina kadhia nyingi…”
Eleza muktadha wa dondoo hili.
Msemaji – Mtemi Lesulia
Wasemewa – Wafuasi wake waliofika kumpa pole baada ya kushindwa katika uchaguzi.
Baada ya Lesulia kushindwa katika uchaguzi, alijifungia chumbani kwa siku mbili akisononeka na kulaani kila mtu.
Aliwakataza walioenda kumpa pole kwamba hakuwa amefiwa wala asingebaki kuwa mtemi wao siku zote za maisha yake.Ni nyumbani kwake Mtemi Lesulia.
Eleza umuhimu wa mbinu ya kimtindo iliyotumika katika dondoo hili ukirejelea riwaya nzima.
Mbinu iliyotumiwa ni kinaya. Kinaya ni tukio lililo kinyume cha matarajio ya msomaji au msikilizaji. Hoja zifuatazo zinadhihirisha namna mbinu hii ilivyotumiwa pamoja na umuhimu wake.
Ni kinaya kwamba Mangwasha anapomuombea mumewe atokomee kabisa ndipo wazo hilo linavyorejea kwa kasi na kuighasi nafsi yake.
Inadhihirisha kuwa Mangwasha ana mapenzi ya dhati kwa mumewe na mwenye utu.
Ni kinaya kuwa kila baya lililotokea katika nchi ya Matuo, lawama ilielekezwa kwa Waketwa (uk 6). Hii ni dhuluma dhidi ya Waketwa.
Ni kinaya kutothamini elimu inayotolewa kwa vijana.Hali hii inachangiwa na ukabila uliokithiri Matuo chini ya uongozi wa Mtemi Lesulia (uk 43).
Kuajiriwa kwa Wakule kwa taaluma ambazo hawakusomea kwa misingi ya kikabila ni kinaya (uk 44).
Ni kinaya kwa Mtemi Lesulia kushindwa kujiamini mwenyewe.Hali hii inasababisha madhila mengi kwa Waketwa wanaonyimwa nafasi za kuajiriwa (uongozi mbaya) uk 44).
Ni kinaya kwa wazazi kutojali maslahi ya wana wao na wengine kuwa katili kiasi cha kuangamiza makinda wao (ukatili) uk 47.
Askari wanapotekeleza maagizo ya Mtemi Lesulia bila kuzingatia usalama wao wenyewe wala wa wana wao ni kinaya (Ubarakala).
Mtemi Lesulia anahusika katika kuwatimua Waketwa kutoka kwa makao yao ya Matango ilhali ndiye kiongozi wao anayestahili kutetea haki za wote (uk96).
Kutimuliwa kwa jaji aliyesimamia haki ya Waketwa kuhusiana na umiliki wa Matango ni kinaya (matumizi mabaya ya mamlaka) uk96.
Ni kinaya kwa Mrima kufikiri kwamba utu hauna umuhimu tena (ubinafsi) uk107.
Sagilu kumwendea kinyume mwanawe, Mashauri, kinyume kwa kufanya mahusiano na Cheiya (utovu wa maadili) uk121.
Kushirikiana kwa Sagilu na Mrima ni kinaya kwani awali Mrima alimuambaa Sagilu kama tauni alipogundua kwamba alitamani kufanya usuhuba na Mangwasha (Mrima ni kigeugeu).
Chifu Mshabaha kuenda kumuomba msaada wa kifedha Mangwasha ni kinaya (umuhimu wa kutenda wema) uk154.
Mtemi Lesulia kudai kuwa hakutaka kushinda uchaguzi ni kinaya kwani alikuwa ametumia raslimali zake na za umma kuhakikisha anashinda katika uchaguzi (uk177).