Lugha, Fasihi na Elimu

Mwalimu anayepambana kuondoa wanafunzi mitandaoni, kuwarejesha vitabuni

Na RICHARD MAOSI February 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KIGEZO cha kupimia upevu wa mwalimu ni upana wa uelewa wake wa masuala yote yanayofungamana na mtaala.

Mwalimu bora anastahili kuwa na ufahamu unaozidi wa wanafunzi wake na adhihirishe ubunifu mkubwa kupitia matumizi ya nyenzo na mbinu tofauti za ufundishaji.

Anatakiwa pia kufanya utafiti wa mara kwa mara, awe mchangamfu na mwepesi wa kufanya somo lake kuwa la kusisimua na la kueleweka haraka.

Haya ni kwa mujibu wa Bi Pamela Nyaga ambaye sasa ni mwalimu katika Shule ya Upili ya Ikuu Boys iliyoko Chuka Kusini, Kaunti ya Tharaka Nithi.

“Mwalimu anastahili kuwa nadhifu, mcheshi na mwenye nidhamu. Ajitume kazini na atambue mahitaji ya wanafunzi wake pamoja na uwezo wa kila mmoja wao masomoni. Awaelekeze kwa utaratibu unaofaa, ateke saikolojia yao kwa wepesi na awatie moyo hata wasipofikia matarajio yake binafsi,” anasema.

Kwa mtazamo wa Bi Pamela, mwalimu hafai kuwa kiini cha wanafunzi wake kufeli wala kukata tamaa katika safari ya masomo inayohitaji subira, kujinyima kwingi na moyo wa kujitolea.

Anafaa kumsaidia mwanafunzi kutambua na kulea vipaji vyake huku akimtia motisha ya kupenda kusoma vitabu na kumshajiisha maishani.

“Vijana wa siku hizi wana mazoea ya kutumia muda mwingi kwenye mitandao ya kijamii badala ya kusoma vitabu. Mustakabali wa usomaji wa vitabu uko hatarini. Walimu hatuna budi kuubadilisha mkondo huu ili taifa lisiangamie,” anasisitiza Bi Pamela.

Pamela alilelewa katika kijiji cha Kimuchia kilichoko Chogoria, Maara, Tharaka Nithi. Alianza safari yake ya elimu katika Shule ya Msingi ya St Augustine Chogoria (2001-2006) kabla ya kujiunga na Shule ya Msingi ya Little Friends Academy, Makuri (2007-2008) kisha Shule ya Upili ya Chuka Girls, Tharaka Nithi (2009-2012).

Japo matamanio yake ya tangu utotoni yalikuwa kuwa tabibu au daktari, alihiari kusomea shahada ya ualimu (Kiingereza/Fasihi) katika Chuo Kikuu cha Kenyatta (2013-2017).

Aliyechochea zaidi kujitosa kwake katika taaluma ya ufundishaji ni mlezi wake, Bw James Nyaga, ambaye kwa sasa ni Mwalimu Mkuu katika shule moja ya upili iliyoko Tharaka Nithi.

Kabla ya kuhitimu chuoni, Bi Pamela alishiriki mafunzo ya nyanjani mnamo 2016 katika Shule ya Upili ya St John Chrysostom Muvandori, Kaunti ya Embu.

Alipata baadaye kibarua cha kufundisha katika Shule ya Upili ya Kieni iliyoko Chogoria (2017-2018) kabla ya kuhamia Ikuu Boys.

Ilikuwa hadi Januari 2020 alipoajiriwa na Tume ya Huduma kwa Walimu (TSC) na akadumishwa shuleni Ikuu Boys.

Pamoja na kuwa mwalimu wa darasa, amekuwa pia Mlezi wa Chama cha Midahalo shuleni humo kuanzia mwaka wa 2021.

Tangu wakati huo, amekuwa akishirikisha idadi kubwa ya wanafunzi wake kwenye ngazi, kategoria na viwango mbalimbali vya mashindano ya mijadala huku akiwahimiza zaidi kujikuza katika fani na sanaa zinazofungamana na masomo ya lugha.

Bi Pamela anajivunia kuwa kiini cha motisha inayotawala wanataaluma wengi chipukizi ambao hutangamana naye katika ngazi na viwango tofauti katika sekta ya elimu.

Kubwa zaidi katika maazimio yake kwa sasa ni kujiendeleza kitaaluma kwa kusomea shahada ya uzamili na uzamifu (PhD) ili kuweka hai ndoto ya kuwa mhadhiri wa kozi za fasihi katika vyuo vikuu.

Matamanio yake mengine ni kuwa mwandishi stadi wa kazi za kubuni, hasa mashairi na hadithi za watoto.