UCHAMBUZI WA FASIHI: Vitushi katika hadithi fupi ‘Mapambazuko ya Machweo’
MZEE Makutwa na Mzee Makucha wanaishi mjini Kazakamba. Awali walikuwa marafiki ila sasa kinachowaunganisha ni umbuya wa kusalimiana tu.
Wote wamerejea nyumbani baada ya kuacha kazi.
Mzee Makutwa alistaafu baada ya kufikia wadhifa wa uwaziri serikalini naye Mzee Makucha aliachishwa kazi kutokana na sera ya serikali ya kupunguza idadi ya waajiriwa.
Maisha ya Mzee Makucha yaligeuka kuwa shubiri. Juhudi zake za kutaka kurejeshwa kazini hazikufaulu.
Kuzidisha, shirika la reli lililokuwa mwajiri wake lilisambaratika kabla ya kumlipa marupurupu yake.
Bintiye, Riziki, alitoroka nyumbani kwenda kuolewa ughaibuni baada ya kushindwa kuyahimili maisha haya mapya.
Mzee Makucha akaanza kujitafutia riziki kwa kuchuuuza vitafunwa kando ya barabara. Mkewe, Bi Macheo, alichangia pato la jamii kwa kuchuuza vitafunwa kwenye veranda ya nyumba yao.
Maisha ya Mzee Makutwa yalikuwa siri kwa jamii. Alionekana akiendesha gari lake mitaani akiwa na vijana waliokuwa umri wa wajukuwe.
Alimkebehi Mzee Makucha kila uchao akidai alijidunisha kwa kushiriki biashara ya kuchuuza bidhaa ndogondogo.
Alidai zile shughuli alizojipa za kushinda na vijana zilikuwa za kusaka pesa. Masimango yake na maswali aliyouliza Bi Macheo yalimpa ari Mzee Makucha kumchunguza Mzee Makutwa.
Siku moja Mzee Makucha alivizia mazungumzo baina ya vijana wawili, Dai na Sai, waliokuwa wakisubiri kuchukuliwa na gari la Mzee Makutwa.
Akaamua kuchukua teksi kuwafuata ili ategue kitendawili cha shughuli za Mzee Makutwa na vijana mle mtaani.
Safari yao iliwafikisha kwenye mgodi. Kulikuwa na umati wa vijana waliofanya kazi mbalimbali wakiwa chini ya ulinzi mkali wa wanyapara.
Ua wa stima ulizunguka sehemu hii na mabawabu wenye majibwa makubwa waliwazuia waliongia mle kutotoka.
Mzee Makucha alipenyeza hadi ndani ya pango walikofanyia kazi vijana wale. Hewa yenye joto ilifanya mja kupumua kwa shida. Vijana walichimba madongo ya mchanga na kuyatia kwenye mikokoteni.
Yalisafirishwa hadi kwenye uwanja ambako vijana wengine walipepeta mchanga huo na kuugawa katika mafungu. Kikundi kilichosalia cha watoto wadogo kilidondoa vijiwe vidogovidogo vyenye kung’aa.
Mzee Makucha aliporejea walikoegesha gari, alikabiliwa na walinzi na akajitambulisha kama rafikiye Mzee Makutwa, ambaye kwao walimfahamu kama Mzee Mamboleo.
Walipoondoka, walifululiza hadi kituo cha polisi kupiga ripoti. Kikosi cha polisi kilizuru sehemu hiyo na kumkamata Mzee Makutwa.
Walinzi na vijana walitoroka polisi walipokuwa wakimsaka Mzee Makutwa. Alitiwa korokoroni kwa kosa la jinai akisubiri kufunguliwa mashtaka.
Mzee Makucha alipokea tuzo kutoka kwa tajiri mmoja kwa ujasiri wake na kwa kuiokoa jamii kutokana na uhalifu ulioendelezwa dhidi ya jamii.