• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 4:54 PM
Wanafunzi 25 waliokosa KCPE kujiunga na shule za upili

Wanafunzi 25 waliokosa KCPE kujiunga na shule za upili

NA GEORGE ODIWUOR

WANAFUNZI 25 waliokosa kufanya Mtihani wa Kitaifa wa Darasa la Nane (KCPE 2023) katika eneobunge la Homa Bay watajiunga na Kidato cha Kwanza, Wizara ya Elimu imetangaza.

Wanafunzi hao wataingizwa kwa shule mbalimbali za upili kulingana na alama walizokuwa wakifanya katika mitihani mbalimbali wakiwa katika shule za msingi.

Mkurugenzi wa Elimu wa Homa Bay Ziada Osano alisema maafisa katika ofisi yake watatafuta alama ambazo wanafunzi hao walikuwa wakipata kabla ya kuruhusiwa kujiunga na shule za upili.

“Wizara ya Elimu ilitoa agizo kutoa utaratibu wa kuwaruhusu waliokosa kufanya KCPE mwaka 2023 kujiunga na shule za upili. Watajiunga kwa shule hizo kulingana na mtindo wao wa matokeo walipokuwa katika shule za msingi,” akasema Bi Osano.

Aidha Bi Osano alisema watapekuwa kuhakikisha wanafunzi hao walikuwa wakifuatilia masomo ya mtaala wa hapa nchini Kenya.

Kwa mujibu wa agizo la wizara, wanafunzi hao wanatarajiwa kufanya mtihani mwingine watakapokuwa katika Kidato cha Tatu kabla ya kuingia Kidato cha Nne. Mtihani huo utapewa hadhi sawa na KCPE.

Msichana ambaye alihudhuria masomo yake mwaka mzima lakini akakosa kufanya KCPE ni miongoni mwa watakaojiunga na shule ya upili chini ya utaratibu huo wa kipekee.

Shule yake ilikuwa na watahiniwa 190 lakini jina lake lilikosekana kwenye orodha.

Shule ilisema wanafunzi wote waliambiwa kuthibitisha majina yao.

Mwanafunzi huyo alikuwa akijificha kwa choo wakati wenzake walifanya KCPE kwa siku tatu.

Babake msichana huyo alishangazwa mno.

“Binti yangu aliniambia hakufanya mtihani wakati matokeo yalitangazwa,” akasema mzazi wa mtoto huyo.

Bi Osano naye aliongeza kwamba farakano baina ya wazazi ilikuwa sababu nyingine ya wanafunzi wengine kukosa kufanya mtihani kwani walitoroka.

Pia alisema yuko mwanafunzi aliyekosa kufanya mtihani kwa sababu ya ugonjwa kumlemea katika kipindi hicho.

[email protected]

  • Tags

You can share this post!

Raila azuru Kilifi kukipa chama cha ODM mvuto mpya

NGUVU ZA HOJA: Tafsiri na ukalimani zijumuishwe katika...

T L