Makala

Mackenzie sasa ashtakiwa kwa vifo Kwa Bi Nzaro alivyohusishwa kupitia ‘ushahidi wa kisayansi’

Na BRIAN OCHARO February 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

MHUBIRI tata Paul Mackenzie na mwenzake Shallyne Anindo Temba wameshtakiwa kuhusiana na kile ambacho wachunguzi wanakirejelea kuwa awamu ya pili ya Shakahola, ambayo ni wimbi jipya la vifo vinavyohusishwa na dhehebu la kidini vilivyotokea katika msitu wa Kwa Bi Nzaro, Kaunti ya Kilifi.

Mackenzie na Temba walishtakiwa pamoja na Kahindi Kazungu Garama almaarufu Mlewa, Tom Ochieng Mkonwe almaarufu Thomas au Tomaso, Julius Tuva Luwali na Johnson Gona Richard.

Washtakiwa hao sita walifikishwa mbele ya Mahakama jijini Mombasa na wakakana mashtaka hayo, ambayo upande wa mashtaka unadai yalitendeka kati ya Januari na Julai 2025 katika eneo la Kwa Bi Nzaro.

Kulingana na hati ya mashtaka, washtakiwa hao, kwa kutekeleza mapatano ya kujiua kwa lengo la kusababisha vifo vyao na vya wengine wasio mbele ya mahakama, waliwaua kwa pamoja watu 29.

Katika shtaka la kwanza, upande wa mashtaka unadai kuwa walimuua Samuel Owino Owuoyo, aliyetambuliwa kama MLD BODY 19.07.2025.

Mashtaka yaliyosalia yanahusu vifo vya watu wengine 28, wengi wao wakielezewa katika hati ya mashtaka kama watu wasiojulikana wa jinsia isiyobainika na umri usiojulikana.

Baadhi ya miili hiyo imetambuliwa kupitia marejeleo ya kimaabara na ya eneo la tukio, yakiwemo BZRB G006 22.08.2025, BZRB G006 2,22.08.2025 na BZRB G018 28.08.2025, pamoja na nambari nyingine za ASN na BP zinazohusishwa na maeneo ya mazishi yaliyogunduliwa katika eneo la Kwa Bi Nzaro.

Katika kesi tofauti mbele ya Mahakama ya Shanzu, Mackenzie, Temba na washtakiwa wengine sita wanakabiliwa na mashtaka ya itikadi kali na makosa yanayohusiana na ugaidi yanayohusishwa na vifo vya angalau waumini 52 wa kanisa lililopigwa marufuku la Good News International Ministries.

Wengine ni Garama, Mkonwe, Luwali, Gona, Charles Mutua Musee almaarufu Mzee Mutua na James Kazungu Kahindi almaarufu Ponda au Baba Bura.

Kwa mujibu wa hati ya mashtaka, washtakiwa hao wanane wanakabiliwa kwa pamoja na makosa sita yanayohusiana na uhalifu uliopangwa na makosa ya kigaidi.

Upande wa mashtaka unadai kuwa kati ya Januari na Julai 2025, katika eneo la Kwa Bi Nzaro, washtakiwa walikuwa wanachama wa dhehebu la kidini lenye itikadi kali lililoelezewa kama kundi la kihalifu lililohatarisha maisha ya wafuasi wake na kusababisha vifo vya watu wasiopungua 52.

Temba na Garama pia wanadaiwa kusaidia upatikanaji wa shamba katika eneo la Kwa Bi Nzaro lililotumika kuandaa vitendo vilivyosababisha vifo hivyo.

Garama, Luwali na Gona nao wanadaiwa kusaidia kusafirisha waathiriwa kutoka Mji wa Malindi hadi Kwa Bi Nzaro.

Aidha, Temba, Garama, Mkonwe na Musee wanakabiliwa na shtaka la kupatikana na vifaa vinavyohusishwa na shughuli za kigaidi, ikiwa ni pamoja na diski za kumbukumbu na kadi za SD zilizo na mahubiri yaliyorekodiwa ambayo yanadaiwa kuwachochea wafuasi kufunga hadi kufa.

Walikana mashtaka hayo. Washtakiwa hao wanane pia waliwasilishwa mbele ya Mahakama Kuu jijini Mombasa kuhusiana na mashtaka 25 ya mauaji.

Hata hivyo, hawakutakiwa kujibu mashtaka hayo mara moja baada ya mahakama kuamuru wafanyiwe uchunguzi wa akili ili kubaini kama wanafaa kushtakiwa rasmi kwa makosa ya mauaji.

Upande wa mashtaka uliomba uchunguzi huo wa akili ufanywe kabla ya washtakiwa kujibu mashtaka, na ukaeleza kuwa utapinga ombi lolote la kuachiliwa kwao kwa dhamana, ukiomba siku nne kuwasilisha hati ya kiapo ya kupinga dhamana.

Kwa mujibu wa hati ya mashtaka, makosa ya mauaji yanahusu vifo vya watoto wa jinsia isiyojulikana wenye umri kati ya mwaka mmoja na miaka 11.

Musee na Kahindi, kwa nyakati tofauti, wanakabiliwa na shtaka la kusaidia wahalifu baada ya kutenda kosa la mauaji.

Serikali inadai kuwa walimpokea Luwali na kuwasaidia Temba, Garama na Mkonwe huku wakijua walikuwa wametenda kosa la mauaji, kwa lengo la kuwasaidia kukwepa mkono wa sheria.

Mackenzie amehusishwa na vifo vya Bi Nzaro kupitia ushahidi wa kisayansi unaodaiwa kuunganisha vifo hivyo na mafundisho pamoja na shughuli zake.

Ushahidi huo unajumuisha rekodi za mawasiliano ya simu, miamala ya MPesa pamoja na maelezo yaliyothibitishwa kutoka kwa washirika wanaodaiwa kuhusika katika matukio hayo.