Makala

Maelfu kupoteza kazi kampuni 1300 zikifutwa

Na BENSON MATHEKA April 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

Maelfu ya Wakenya wamo hatarini kupoteza ajira huku serikali ikifuta maelfu ya kampuni.Kampuni 1300 zimefungwa na kufutwa kutoka kwenye sajili rasmi ya kampuni, katika hatua kubwa inayolenga kusafisha mfumo na kuondoa kampuni zisizotekeleza wajibu wao kisheria.

Hatua hiyo ilitangazwa kupitia notisi za Gazeti la Serikali nambari 5212 hadi 5215, ambazo zilithibitisha kuwa kufutwa kwa kampuni hizo kulianza mara moja baada ya kuchapishwa kwa tangazo hilo. Hii ina maana kuwa kampuni zote zilizoathirika zimepoteza hadhi yao ya kisheria na haziwezi tena kuendesha shughuli zozote kwa jina lao.

“Kwa mujibu wa Kifungu cha 894 (5) cha Sheria ya Kampuni, umma unafahamishwa kuwa kampuni zifuatazo zimevunjwa na majina yao kuondolewa kwenye Sajili ya Kampuni kuanzia tarehe ya tangazo hili,” ilisema sehemu ya notisi hiyo.

Kampuni zilizofutwa zinahusisha sekta karibu zote za uchumi wa Kenya. Hizi ni pamoja na biashara za kilimo na ufugaji, kampuni za dawa, huduma za ubadilishaji fedha za kigeni, pamoja na kampuni za usafirishaji wa mizigo na teknolojia.

Sekta ya ujenzi imeathirika pakubwa, ikijumuisha wakandarasi, wastawishaji wa mali, wauzaji wa vifaa vya ujenzi na kampuni za mali isiyohamishika. Sekta ya usafiri pia imegongwa, huku kampuni za teksi, usafirishaji wa mizigo, huduma za usafirishaji wa vifurushi na hata usafiri wa baharini zikiorodheshwa.

Huduma za kifedha kama kampuni za bima, ushauri wa uwekezaji na uhasibu pia hazikuachwa nyuma. Kadhalika, hoteli, mikahawa, kampuni za usafiri wa watalii na biashara za kukodisha magari zimejumuishwa katika orodha hiyo pana ya kampuni zilizofutwa.

Mbali na kampuni hizo, notisi nyingine imetaja kampuni 289 ambazo zinakabiliwa na hatari ya kufutwa iwapo hazitachukua hatua ndani ya muda wa miezi mitatu tangu kuchapishwa kwa tangazo hilo.

“Kwa mujibu wa Kifungu cha 894 (3) cha Sheria ya Kampuni, baada ya miezi mitatu tangu tangazo hili, isipokuwa sababu itolewe kinyume, Msajili wa Kampuni ataondoa majina ya kampuni hizo kutoka sajili na hivyo zitafutwa,” ilieleza notisi hiyo.

Kampuni hizi 289 zinatoka sekta mbalimbali zikiwemo nishati ya jua, mafuta, utengenezaji wa saruji, maji na usafi, ushauri wa kitaalamu, masoko na udalali.

Wakurugenzi wa kampuni hizi wanatakiwa kuwasilisha pingamizi rasmi au uthibitisho kuwa kampuni zao bado zinafanya kazi ndani ya muda uliowekwa. Kushindwa kufanya hivyo kutasababisha kufutwa moja kwa moja bila notisi nyingine.

Hatua hii ina athari kubwa kwa wenyehisa, wakurugenzi na wafanyakazi wa kampuni husika, hasa pale ambapo kuna mikataba, mali au madeni ambayo bado hayajalipwa. Kufutwa kwa kampuni kunaweza kuathiri washirika wa kibiashara.

Kifungu cha 894 cha Sheria ya Kampuni kinampa Msajili mamlaka ya kufuta kampuni ambazo hazifanyi kazi au zimekuwa zikikiuka masharti ya kisheria mara kwa mara. Serikali imekuwa ikitumia kifungu hiki kuhakikisha sajili ya kampuni inabaki kuwa safi, sahihi na yenye kuaminika.

Hatua hii inajiri wakati ambapo Kenya inakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa ajira, hasa miongoni mwa vijana. Kwa mujibu wa takwimu za hivi karibuni, kiwango cha ukosefu wa ajira bado kiko juu, hali inayofanya kufutwa kwa kampuni nyingi kwa wakati mmoja kuwa suala linalozua mjadala mpana kuhusu athari zake kwa uchumi.