Majonzi mama akiibiwa mtoto mgonjwa alipofika hospitali kusaka matibabu
MAMA mmoja katika eneo la Voi, Kaunti ya Taita Taveta, ameeleza machungu yake baada ya mtoto wake mchanga kuibwa na mwanamke asiyejulikana.
Bi Luciana Eghwa, 19, alikuwa ametembelea Hospitali ya Rufaa ya Kaunti ya Moi mjini Voi, akitafuta matibabu ya mwanawe wa mwezi mmoja aliyekuwa mgonjwa alipokutana na mwanamke huyo.
Aliambiwa kuwa, mwanawe hangepata matibabu kwa vile hakuwa amesajiliwa kwa Bima ya Afya ya Kijamii (SHIF).
Bi Eghwa alishauriwa kumsajili au alipie huduma hizo kwa pesa taslimu lakini kutokana na changamoto za kifedha, hakuweza kupata matibabu.
Akiwa amekata tamaa, mwanamke aliyeonekana mwenye huruma alimkaribia na kujitolea kumsaidia mwanawe kupata matibabu katika kituo cha afya cha Ndovu, kilicho viungani mwa mji wa Voi.
Bi Eghwa alisema kuwa, mwanamke huyo alimshawishi kwenda huko na hata akalipia usafiri wao wa pikipiki.
“Nilikubali kwa kuwa sikumshuku. Aliniambia kuwa, pale Ndovu matibabu ni bure na nikakubali tukapanda pikipiki moja na yeye ndio alilipa nauli,” alieleza.
Walipowasili, Bi Eghwa aliingia ndani kutafuta huduma huku mgeni huyo akisubiri nje.
“Niliingia ndani na mtoto wangu. Nilipoambiwa kuwa lazima mtoto asajiliwe kwa bima ya SHA nilitoka nje nikaenda kumueleza huyo mwanamke nilichoambiwa. Lakini mimi ndio nilikuwa na mtoto,” alieleza.
Dakika chache baadaye, mwanamke huyo alimpa Bi Eghwa noti ya Sh200 na kumtuma akatafute chenji.
Bila kusita na kuuliza maswali, Bi Eghwa alimwachia mwanamke huyo mtoto na kwenda kwa maduka yaliyoko mita chache kutafuta chenji.
Aliporudi katika lango la kituo cha afya cha Ndovu alipokuwa amemwacha mwanamke huyo na mtoto, hakuwapata.
Akiwa na mshangao na hofu, alianza kuuliza waliokuwepo eneo hilo ikiwa walimuona mwanamke huyo akiondoka.
“Niliambiwa alipanda pikipiki kuelekea mjini. Nilipanda pikipiki kuwafwata lakini sikuwaona,” alisema.
Alirudi katika hospitali ya Moi lakini hakumuona na hivyo kuripoti katika kituo cha polisi cha Voi.
Baadaye, walielezwa kuwa mwanamke huyo alionekana akiwa na mtoto katika kituo cha magari cha Caltex na kupanda gari kuelekea Nairobi.
Mkuu wa polisi wa Voi Fredrick Kinaibei, alithibitisha kisa hicho na kusema uchunguzi ulishaanzishwa, huku picha ya mwanamke huyo ikisambazwa kwa vituo mbalimbali vya polisi.
Kamera za CCTV zilimnasa mshukiwa akiongea kwa simu katika wodi ya wajawazito katika hospitali ya Moi kabla ya kutekeleza uhalifu wake.
Bi Eghwa na familia yake wamekuwa wakizunguka katika maeneo tofauti wakijaribu kupata dalili zozote za mtoto wao huku polisi wakianza uchunguzi.
“Tuliambiwa kuwa alishukia Mtito Andei. Tunaomba msaada kutoka kwa wasamaria wema ili tuweze kupata mtoto wetu. Tukio hili limetusikitisha sana hata hatuwezi kula sababu ya huzuni kubwa tuliyopata,” alisema Bi Monica Msae, mamake Bi Eghwa.