Mamia wafurika Isiolo kupata matibabu ya bure
KUFIKA saa sita mchana, zaidi ya watu 700 tayari walikuwa wamefika kupokea matibabu ya bure katika Kaunti ya Isiolo.
Japo waandalizi wa mpango huo walitarajia kuwa idadi hiyo ingekuwa 400, watu walifika kwa wingi pindi tu walipopata habari kuwa matibabu yalikuwa yakitolewa bure.
Akizungumza katika Kanisa la St Eusebius Cathedral Kaunti ya Isiolo, Afisa Mkuu Mtendaji wa Chesire Disability Services Kenya, Bi Cecilia Mutava alibainisha kuwa kwa ushirikiano na Wizara ya Afya, Dayosisi ya Kikatoliki ya Isiolo na AIC Cure International waliweza kutoa huduma za matibabu kwa wakazi waliokuwa wakiugua magonjwa mbalimbali.
Aliongeza kuwa kauli mbiu ya mwaka huu ulikuwa kuondoa vikwazo katika sekta ya Afya na kutoa Huduma za Afya kwa Watu wanaoishi na ulemavu mbalimbali na kuiomba serikali kutenga fedha zaidi kwa wizara ya afya.
“Tunaomba serikali iingilie kati ili kuhakikisha kuwa kuna vifaa vya kutosha kuwezesha utoaji wa huduma kwa watu wanaoishi na ulemavu. Dawa ni ghali sana hasa kwa wale wanaotoka katika familia zisizojiweza. Tunatoa wito kwa wadau wote ikiwa ni pamoja na serikali kusimamia huduma za matibabu ili kusaidia watu wanaoishi na ulemavu hasa katika maeneo ya mashinani,” Bi Mutava alisema.
Dkt Karanja Njuguna Mark, daktari wa upasuaji wa mifupa katika Hospitali ya AIC Cure aliangazia matatizo ya clabfoot na ugonjwa wa kupooza kwa ubongo miongoni mwa wenyeji.
Wagonjwa wawili ambao walikuwa wamesafiri kilomita tano kupata huduma, Bi Akiru Ebeiyo, 77 na Bi Asukuru Losopiro, 85 waliambia Taifa Dijitali kwamba walifika Isiolo kutoka kaunti ya Turkana kutafuta huduma za matibabu bila malipo kwa vile SHA haifanyi kazi.
Masaibu yao ni moja tu kati ya Wakenya wengine ambao wanapitia changamoto katika kipindi cha mpito kutoka NHIF hadi SHA.
Wenyeji waliwapongeza waandalizi kwa kuwashughulikia wakisema kuwa kuna uhaba wa madaktari, wauguzi pamoja na kuadimika kwa madawa.
Pauline Kinyua, muuguzi aliyestaafu ambaye kwa sasa anafanya kazi na Kanisa Katoliki la Isiolo, alisema kuwa Isiolo ni mji unajumuisha makabila matano ambao hujishughulisha na maisha ya ufugaji wa mifugo.
“Kuna wale wanaoishi kilomita 300 kutoka hapa. Baadhi ya wale wanaohitaji msaada ni watoto wanaoishi na ulemavu ambao wanahangaika kwani SHA haiwasaidii watu kama hao. Wanahitaji kulazwa,” Muuguzi Kinyua alisema.