Makala

Mamlaka yasema mikakati mipya inafaa kuwekwa kudhibiti mafuriko Nairobi

Na WINNIE ONYANDO March 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAMLAKA ya Kitaifa ya uhifadhi wa Maji (NWHSA) imetoa wito kwa serikali na wadau mbalimbali kuwekeza katika mikakati ya muda mrefu ya kuteka na kuhifadhi maji ili kudhibiti mafuriko yanayoendelea kuathiri Kaunti ya Nairobi kila msimu wa mvua.

Akizungumza na Taifa Leo Dijitali kufuatia mafuriko makubwa yaliyokumba jiji jana, Mkurugenzi Mkuu wa NWHSA, Julius Mugun, alisema janga hilo linaonyesha udhaifu mkubwa katika mifumo ya usimamizi wa maji mijini.

Alisema ingawa juhudi za dharura za uokoaji ni muhimu, hazitoshi kushughulikia chanzo kikuu cha mafuriko yanayojirudia kila mara.

“Mafuriko tunayoshuhudia sasa yanaonyesha wazi kuwa miundombinu yetu ya sasa haiwezi kumudu kiwango cha maji kinachotokana na mvua kubwa,” alisema Mugun.

Mvua kubwa iliyonyesha Ijumaa ilisababisha barabara kadhaa jijini Nairobi kufurika na kufanya usafiri kuwa mgumu kwa saa nyingi.

Baadhi ya barabara zilizoathirika ni pamoja na Mombasa Road, Kenyatta Avenue katikati ya jiji (CBD), Thika Road, Dunga Road na Enterprise Road.

Maeneo kadhaa ya makazi pia yalifurika maji, yakiwemo South C, Embakasi pamoja na baadhi ya mitaa ya mabanda na maeneo ya yaliyojengwa kando na mito.

Kulingana na Bw Mugun, kiwango kikubwa cha maji kinachotokana na mvua kubwa huzidi uwezo wa mifumo ya mifereji ya maji iliyopo sasa, ambayo nyingi zimepitwa na wakati au kuziba.

“Kiasi cha maji ya mvua tunachoshuhudia kinazidi uwezo wa miundombinu yetu ya sasa ambayo haikujengwa kuhimili kiwango hiki cha maji,” alisema.

Aliongeza kuwa mafuriko huathiri pia shughuli za kiuchumi katika jiji zima.

Bw Mugun alisema suluhu la kudumu linahitaji mbinu mbili kwa pamoja, kuboresha mifereji ya maji na kuimarisha utekaji wa maji ya mvua.

“Lazima tubadili mtazamo wetu kuhusu maji ya mvua. Badala ya kuyaona kama tatizo, tunaweza kuyageuza kuwa rasilimali muhimu kwa kuyateka na kuyahifadhi,” alisema.

Kulingana naye, kila kiasi cha maji kinachotekwa hupunguza uwezekano wa maji hayo kusababisha mafuriko katika makazi au barabara.

Alisema mamlaka hiyo iko tayari kushirikiana na serikali za kaunti, na wadau wengine kubuni miradi ya kudumu ya kuhifadhi maji, ikiwemo mabwawa makubwa, na mifumo ya utekaji wa maji katika makazi ya watu.

Idara ya Utabiri wa Hali ya Hewa imetahadharisha kuwa mvua huenda ikaendelea kunyesha katika siku zijazo.