• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 2:00 PM
MAPOZI: Eddie Butita

MAPOZI: Eddie Butita

Na PAULINE ONGAJI

NI mmojawapo wa wachekeshaji wanaotamba nchini kwa sasa huku akijiundia jina kupitia kipindi cha Churchill Show na Churchill Raw.

Jina lake ni Edwin Butita, lakini jukwaani anafahamika kama Eddie Butita, mcheshi, mwigizaji, mwandishi wa miswada ya vipindi, mwelekezi wa thieta, produsa na mfawidhi, miongoni mwa mambo mengine mengi.

Lakini licha ya kujihusisha na mambo mengi, Butita hasa amenoa makali yake katika uvunjaji mbavu ambapo jitihada zake zimemfanya kuwa miongoni mwa wachekeshaji wanaothaminiwa sana katika kipindi cha Churchill Show.

Eddie Butita. Picha/ Maktaba

Mojawapo ya sifa zinazomtenganisha na wengine ni ustadi wake wa kutumia tashtiti hasa kuonyesha maisha ambayo wakazi wa vitongoji duni hukumbana nayo.

Ni suala ambalo kando na kuangazia uhalisia wa matatizo yanayowakumba wakazi wa maeneo haya, linawaacha mashabiki wakiangua vicheko.

Na ni uthabiti huu ambao umemuundia jina kiasi cha kumfanya kupata fursa za kutumbuiza katika shoo zingine zikiwemo Laugh Festival, Night of a Thousand Laughs, Kenya’s Biggest Laughs, The Hot Seat, Kenya Kona Comedy, The Trend, Crazy Monday Comedy Night, Nescafe Red Sensation Party, 3D Comedy na Kids Festival miongoni mwa zingine.

Lakini kando na masuala ya uchekeshaji, Eddie Butita amepanua himaya yake na kujiundia jina katika uandishi wa miswada na uelekezi wa vipindi, kiasi cha kuchangia katika baadhi ya vipindi vinavyotambulika kama vile Churchill Show, Churchill Raw na Eric Omondi Untamed miongoni mwa vingine.

Katika taaluma yake fupi kama chale, amechangia pakubwa katika kubuni mawazo na mikakati ambayo imeimarisha sekta ya burudani.

Ndiposa mwana burudani huyu ameenda hatua zaidi na kujihusisha katika ujasiriamali ambapo yeye ni mwanzilishi wa kampuni ya Stage Presence Media and Entertainment, inayohusika na maandalizi ya hafla na kusimamia vipaji.

Mzawa wa mtaa wa Kariobangi, jijini Nairobi, alianza kama mwanamuziki kabla ya kutambua kipaji chake cha ucheshi wakati huo akiwa katika shule ya upili, kipaji kilichochewa na wacheshi na waigizaji wa humu nchini na ng’ambo.

Baadhi ya watu waliompa msukumo wa kujitosa katika burudani ni pamoja na mchekeshaji Kevin Hart na mwigizaji Tyler Perry kutoka Amerika, vile vile mwana vichekesho Daniel ‘Churchill’ Ndambuki.

Ajitosa rasmi katika burudani

Mwaka wa 2010 baada ya kukamilisha elimu ya shule ya upili, aliamua kujitosa rasmi katika burudani baada ya kupata fursa ya kushiriki katika majaribio ya kipindi cha Churchill Live.

Ni hapa nyota yake iling’aa kwani katika shoo yake ya kwanza aliwashangaza wengi kwa kunasa macho ya mashabiki katika kipindi hicho licha ya kuwa limbukeni.

Na tangu wakati huo, ameendelea kusisimua mashabiki ambapo kwa sasa ni mmojawapo wa wachekeshaji wanaothaminiwa katika kipindi hicho, suala ambalo limempa fursa ya kushiriki katika vipindi vingine.

Huku akiongozwa na ndoto ya kuwa katika upeo wa ulimwengu wa burudani, swali ni ni iwapo ataepuka jinamizi ambalo limekuwa likiwaandama wengi katika fani hii; kung’aa kwa muda kisha kutoweka.

You can share this post!

Cofek yapinga benki kupewa uhuru wa kudhibiti viwango vya...

WAKILISHA: Anakuza vipaji vya uvumbuzi

adminleo