• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 9:50 AM
MAPOZI: Ethan, Vince & Brandon

MAPOZI: Ethan, Vince & Brandon

Na PAULINE ONGAJI

WANALETA msisimko mpya katika sekta ya RnB ambayo kidogo imesahaulika humu nchini Kenya huku utunzi wao ukihusisha muunganisho wa ladha mbalimbali za muziki tena kwa ustadi mkubwa.

Jukwaani wanafahamika kama Jadi, bendi iliyoundwa sio tu na waimbaji, bali pia watunzi, wacheza ala na hata washairi, suala ambalo limeongeza mvuto kwa kazi zao na kuzipa kina, na hivyo kuongeza hadhara.

Bendi hii ya wanachama watatu ambayo inajumuisha Edward’s Okoth Bryan al-maarufu Ethan, Vincent Mutuma al-maarufu Vince na Brandon Tumbo au kwa usahili Brandon, iko mbioni kuteka mioyo ya wapenzi wa muziki nchini.

Ethan ni mwimbaji, mwandishi wa nyimbo ambapo pia ana uwezo wa kutunga nyimbo za mitindo mbalimbali.

Yeye ndiye mwenye wajibu wa kuongeza lahani kwenye vibao vya kikundi hiki.

Msanii huyu alitambua kuwa angeimba akiwa na miaka sita pekee huku akipata chocheo kutoka kwa mamake ambaye alikuwa mwanachama wa kwaya ya kanisa.

Ili kuendeleza penzi lake la muziki aliamua kutumia kila fursa aliyopata ya uimbaji huku mara kwa mara akiwatumbuiza familia, jamaa na wageni nyumbani.

Ni kipaji kilichojitokeza hata zaidi aliposhiriki na hata kutwaa ushindi kwenye shindano la uimbaji wakati huo akiwa na miaka 12 pekee. Ushindi huu ulimpa ujasiri wa kufuata kwa uthabiti ndoto yake.

Kwa upande wake, Vince ambaye analeta mchango wa uimbaji, uandishi wa nyimbo na densi katika bendi hii, alianza kuimba akiwa angali mchanga, na hata kabla ya kujifunza kutembea alikuwa anaonyesha ishara ya kung’aa katika burudani.

Kama mtoto wa mhubiri, alikuwa na fursa nyingi za kutumbuiza tangu utotoni huku penzi lake katika densi likichochea uamuzi wake wa kujitosa katika muziki.

Vince aliingia katika ulimwengu wa burudani kupitia kikundi cha densi lakini akaamua kuondoka baada ya kutambua kwamba penzi lake katika uimbaji lilikuwa limepiku densi.

Na kwake Brandon ambaye ni muimbaji, mwandishi wa nyimbo, mcheza gitaa na mshairi, muziki umekolea kwenye mishipa ya damu hasa ikizingatiwa kwamba licha ya kuwa mwanafunzi wa ujarisiamali chuoni, bado anafuatilia ndoto yake ya kuwa mwanamuziki.

Bendi hii ilianzishwa Novemba 2018 na kampuni ya Kaka Empire huku muziki wao ukiunganisha mchanganyiko wa muziki wa RnB, Pop na Afro Soul katika kila kibao walichotunga.

Licha ya kwamba bado wabichi kimuziki, wanazidi kuteka wapenzi kwa sauti zao za kupendeza, vilevile vibao vyao vinavyotambulika kwa kunasa hisia za mashabiki.

Jibu

Wanasema kwamba wao ndio jibu kwa wapenzi wa aina zote za muziki nchini, huku wakitajwa kama nafuu ambayo sekta hii imekuwa ikisubiri.

Kinachowatenganisha na vikundi vingine vya kawaida nchini ni muunganisho thabiti kati yao, suala linalofanya iwe rahisi kwao kufanya kazi kwa pamoja.

Kwa sasa wanaendelea kupata umaarufu kupitia kibao chao Mimi na Wewe.

Ni sifa hizi zilizovutia jicho la Kaka Empire. Kulingana nao, kusajiliwa na kampuni hii kumewapa fursa ya kupanua hadhara yao na wanasisitiza kwamba hili litakuwa jukwaa la kuwaongezea umaarufu kimuziki.

Haina shaka kuwa kwa mashabiki wengi, Jadi wangali wachanga lakini kasi waliyojitosa nayo katika ulingo huu ni hakikisho la mwanzo wa ufanisi wao kimuziki.

Wajibu wao kwa sasa ni kudhihirisha iwapo wataendeleza msisimko huu na kudhihirishia ulimwengu kwamba mbio hizi sio mvuke tu!

You can share this post!

WAKILISHA: Rais wa shule yake anayekuza demokrasia

AUNTY POLLY: Ana mimba na siko tayari kuitwa ‘baba’

adminleo