• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 7:53 PM
MAPOZI: Mary Oyaya

MAPOZI: Mary Oyaya

Na PAULINE ONGAJI

WASHIKADAU na mashabiki wengi wa filamu nchini watadhani kwamba ni Mkenya mmoja tu; Lupita Nyong’o, ambaye amewahi kujiundia jina kule Hollywood, Amerika.

Ukweli ni kwamba kuna waigizaji kibao kutoka humu nchini ambao licha ya kutoangaziwa sana na vyombo vya habari, wamefaulu kufika kwenye upeo wa jukwaa hilo.

Mmoja wao ni Mary Oyaya, mwigizaji ambaye ameshiriki katika baadhi ya filamu za haiba ya juu ulimwenguni.

Umaarufu wake hasa ulitokana na filamu ya Star Wars: Episode II – Attack of the Clones ambapo aliigiza nafasi yake Luminara Unduli.

Huu ulikuwa mwaka wa 2002, nafasi iliyomweka kwenye orodha moja na waigizaji maarufu ambao wamewahi kupamba makala tofauti ya filamu hiyo.

Baadhi yao ni Barriss Offee, Samuel L. Jackson, Ewan McGregor, Natalie Portman na Ian McDiarmid miongoni mwa wengine.

Fursa ya kuigiza nafasi hii ilitolewa na ajenti wake ila ili kuifanikisha, ilimbidi kufanyiwa majaribio katika Fox Studios ambapo aliwapiku washindani wengine wengi.

Ni fursa iliyomwezesha kushiriki katika baadhi ya tamasha kuu za filamu katika mataifa mbalimbali Amerika na Ulaya. Miongoni mwazo Celebration; hafla kubwa zaidi ya filamu za Star Wars.

Aidha, ameshiriki katika nafasi ndogo katika sinema mbalimbali kama vile Lost Souls, Down and Under na Farscape.

Na katika harakati hizo anajivunia kuingia kwenye jukwaa moja na baadhi ya maprodusa na waigizaji maarufu, miongoni mwao George Lucas, Wynona Ryder na Barriss Offee.

Mzaliwa wa mji wa Mombasa, Pwani ya Kenya, Mary Oyaya aliishi katika mataifa kadha ikiwa ni pamoja na Canada, Sweden na Australia. Safari yake katika masuala ya burudani na hasa uigizaji ilianza tokea utotoni.

Lakini mbali na uigizaji, yeye pia ni mwanamitindo, shughuli iliyochangia pakubwa kujihusisha kwake katika masuala ya uigizaji.

Taaluma yake kama mwanamitindo ilianza mwaka wa 1996 baada ya kukamilisha kozi ya uigizaji. Kama mwanamitindo ameshirikishwa kwenye majarida tofauti ya kimataifa ikiwa ni pamoja na CAT and S.

Kampuni za haiba ya juu

Pia, anajivunia kufanyia matangazo wasanifu mavazi magwiji, vilevile kampuni za haiba ya juu za kimataifa ikiwa ni pamoja na Salvatore Ferragamo, Gucci, Chanel, Jan Logan, Sergio Rossi.

Kando na hayo, ameshiriki katika matangazo kibao ya kibiashara ikiwa ni pamoja na Telstra Communications na Hewlett Packard.

Lakini licha ya kujihusisha na masuala ya burudani, kimasomo pia amejipiga msasa kwani ana shahada mbili za uzamili; katika Masuala ya mahusiano ya kimataifa na katika Masuala ya ustawi wa kijamii wa kimataifa.

Aidha, sawa na wazazi wake ambao waliwahi kuhudumu kama wanadiplomasia kwa miaka mingi, amewahi kufanya kazi katika shirika la Umoja wa Mataifa na mashirika mengine yasiyo ya kiserikali, huku pia akiwahi kufanya kazi na wakimbizi nchini Australia.

Wahenga walisema kwamba mcheza kwao hutuzwa, lakini kwa Oyaya, utambuzi wake kimataifa umepiku umaarufu wake hapa nyumbani.

Ukweli ni kwamba sio wengi wanaomfahamu sana, suala linalohuzunisha hasa ikizingatiwa kwamba yeye ni mmojawapo wa vigezo vikuu vinavyopaswa kuigwa.

You can share this post!

UKUMBI WA LUGHA NA FASIHI: Jinsi ya kufundisha darasa mseto

MIAMBA: Ureno yakanyaga Uholanzi na kutwaa taji la Uefa...

adminleo