• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 10:08 PM
MAPOZI: Nick Mutuma

MAPOZI: Nick Mutuma

Na PAULINE ONGAJI

ANATAMBULIKA sio tu kutokana na ustadi wake kama muigizaji, bali pia kama mwanamuziki, mwanamitindo, mtangazaji na produsa miongoni mwa kazi zingine.

Hasa Nicholas Munene Mutuma au ukipenda Nick Mutuma, anatambulika kutokana na uigizaji katika baadhi ya vipindi maarufu sio tu humu nchini, bali katika bara lote la Afrika.

Baadhi ya vipindi maarufu nchini Kenya na kwingineko barani Afrika ambavyo ameshiriki ni pamoja na Changes, Shuga, State House, Skinny Girl in Transit na This Is It kutoka Nigeria.

Aidha, ameshiriki kwenye filamu Disconnect iliyozinduliwa nchini kote Aprili 2018 na ambayo ilifanya vyema.

Mzawa wa eneo la Meru, nchini Kenya, Nick Mutuma alilelewa jijini Dar es Salaam, Tanzania, ambapo alisomea katika shule ya kimataifa ya The International School of Tanganyika.

Baadaye alijiunga na shule ya kimataifa ya Braeside School jijini Nairobi, ambapo alikamlisha masomo ya upili.

Mwaka wa 2005, alijiunga na chuo kikuu cha United States International University (Nairobi), hadi 2010 huku akihitimu shahada ya Usimamizi wa Kibiashara wa Kimataifa.

Ustadi ulianza kujitokeza akiwa angali mchanga alipogundua penzi lake kwa sanaa ambapo mara kwa mara angeshiriki katika michezo ya drama shuleni.

Alipata mfichuo wa kwanza kwenye televisheni ya Kenya mwaka wa 2008, alipopata nafasi ya kuigiza kama Luka, kijana mdogo wa chuo cha masomo ya juu anayeishi maisha ya umaskini, hali iliyomsukuma kujihusisha na shuga mami. Nafasi hii iliibua maoni mbalimbali.

Aidha, mwaka huo huo alishiriki kwenye kipindi Changes kilichokuwa kikipeperushwa na kituo cha MNET, ambapo aliigiza kama Richard, kijana anayegundua kwamba alitekwa nyara hospitalini baada ya kuzaliwa, nafasi aliyoihifadhi kwa misimu mitatu, na hivyo kudhihirisa ukomavu wake kama mwigizaji.

Hata hivyo nyota yake iling’aa aliposhiriki kwenye kipindi Shuga (2008)ambapo alivunja rekodi kwa kuwa muigizaji aliyehifadhi nafasi yake kwenye kipindi hicho kwa misimu yote mitano. Kipindi hicho kiliangazia maisha ya vijana jijini Nairobi na tabia ya kushiriki ngono kiholela.

Aidha, kipindi hiki kilizindua taaluma za uigizaji za baadhi ya majina makuu ulingoni, ikiwa ni pamoja na mshindi wa tuzo ya Oscars, Lupita Nyong’o.

Mwaka wa 2014, Mutuma alishiriki kwenye kipindi State House, ambapo aliigiza nafasi ya mwana mkorofi wa rais, anayenaswa na penzi la binti ya mmojawapo wa wafanyakazi.

Miaka miwili baadaye, alijihifadhia nafasi ya kuigiza kama Tomide kwenye kipindi This Is It cha Nigeria.

Kutokana na umaarufu wa kipindi hiki, mwaka 2018 kiliteuliwa kama kipindi bora kwenye tuzo za AMVCA.

Mwaka 2018 pia alishiriki kwenye filamu Disconnect iliyofanya vyema miongoni mwa mashabiki.

Baadaye alishiriki kwenye msimu wa tano wa kipindi Skinny Girl in Transit.

Utangazaji

Kama mtangazaji, Mutuma amekuwa mshiriki mkuu katika vipindi mbalimbali kwenye redio na televisheni.

Aliwahi kujumuishwa mara kadha miongoni mwa waigizaji wa kiume wanaovutia zaidi.

Mwaka wa 2013, alitangazwa kama mwigizaji mwenye kipato kikubwa.

Kimuziki, hajaachwa nyuma huku akifahamika kwa nyimbo kama vile 254 Anthem, kibao alichoimba kwa ushirikiano na Lyra Aoko.

Wimbo huu ulikuwa ukizungumzia mambo mazuri kuhusu Kenya.

Septemba 2014, alizindua kibao kingine kwa jina That Life kwa ushirikiano na Cool Kid Taffie.

Katika masuala ya mitindo amehusika katika utangazaji wa bidhaa mbalimbali ikiwa ni pamoja na Nivea Fresh Active.

Kwa kawaida huwa vigumu kwa wasanii kujihusisha katika tasnia mbalimbali na kung’aa, lakini kwa Nick Mutuma, mambo ni tofauti huku akidhihirishia wenzake kwamba kwa kweli inawezekana.

You can share this post!

WAKILISHA: Uchoraji pato na jukwaa kulea vipaji

AUNTY POLLY…: Rafiki yangu ana matatizo ya kula

adminleo