Makala

Maswali tele kuhusu wahuni waliovuruga maandamanao ya Jumanne

Na WINNIE ONYANDO June 18th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

DIWANI wa Nairobi Kusini, Waithera Chege, ameibua maswali kufuatia vurugu zilizotokea Jumanne Juni 17, 2025 wakati wa maandamano ya amani ya kudai haki kwa waathiriwa wa ukatili wa polisi.

Bi Chege amelaani vikali mashambulio hayo, akidai wahusika walikuwa wahuni waliolipwa, ambao walionekana kwenye video wakipiga kelele wakimuunga mkono Gavana Johnson Sakaja.

“Yaliyotokea yamevunja haki ya msingi ya maandamano ya amani. Ni jukumu la uongozi wa kaunti kuhakikisha usalama wa wananchi, si kushirikiana na makundi yanayowahangaisha waandamanaji,” alisema Bi Chege.

Katika video zilizosambaa, wahuni hao walionekana wakisema: “Sakaja twalinda Jiji,” hali inayozua maswali kuhusu ushirikiano wao wa moja kwa moja au wa kisiri wa Gavana Sakaja.

“Gavana Sakaja anapaswa kuwajibika kwa hali hii. Ikiwa hawezi kuhakikisha usalama wa wananchi, basi ni bora ajiuzulu,” aliongeza Bi. Chege.

Aidha, ametoa wito kwa serikali kuu kuhakikisha haki inapatikana kwa majeruhi na waathiriwa wote wa vurugu hizi.

“Ulinzi wa haki za kidemokrasia ni msingi wa taifa letu. Tusikubali giza la vurugu kufunika nuru ya mabadiliko tunayoyahitaji,” alihitimisha.

Haya yanajiri muda mchache baada ya gavana Sakaja kujitenga kabisa na madai kuwa serikali yake ina uhusiano na wahuni hao.

“Tunajitenga kabisa na magenge yoyote, wahuni, au vikundi vinavyofadhiliwa na wanasiasa ambavyo vinatumia vibaya maandamano kujihusisha na uhalifu,” Sakaja alisema.

 

“Tunalaani vikali uharibifu wa mali ya umma na ya kibinafsi ulioshuhudiwa wiki jana, unaofanywa na majambazi walioletwa kutoka nje ya Nairobi,” aliongeza.

Siku chache zilizopita, gavana huyo alisikika akisema kuwa hataruhusu waandamanaji kuharibu mali ya watu katikati kwa jiji la Nairobi.

Wahuni hao waliobeba visu na marungu Jumanne Juni 17, 2025 walivuruga maandamano huku wakitishia watu na kuwaibia.

Haya yanajiri siku chache tu baada ya makundi ya sungusungu kupiga doria katikati mwa jiji la Nairobi yakiwa na mawe na nyahunyo wakati wa maandamano ya kudai haki kwa mwalimu-bloga Albert Ojwang aliyeaga dunia mikononi mwa polisi.

Hali hii ilifanya baadhi ya wafanyabiashara kufunga maduka yao kwa hofu ya kuporwa kama ilivyotokea wiki jana wakati wa maandamano ya kutaka haki kwa mwalimu-bloga Ojwang.