Makala

Majonzi, simanzi watoto wanne wa familia moja wakiangamia wakichota maji

Na DOMNIC OMBOK February 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WINGU la majonzi limetanda katika kijiji cha Kanyakwar, viungani mwa Kisumu baada ya watoto wanne kutoka familia moja kutumbukia kwenye timbo la mawe lililojaa maji na kufa papo hapo.

Tukio hilo la Jumapili jioni limemwacha Celine Akinyi na mumewe Felix Otieno na makovu, ambayo hawatayasahau daima dawamu baada ya kuwapoteza watoto wanne kwa wakati mmoja.

Bi Akinyi alisimulia kwa machungu jinsi alivyopokea simu kutoka kwa mumewe na kuangukiwa na uzito wa msiba uliotua bomani mwao.

“Aliniambia nije nyumbani mara moja na baada ya kuingiwa na wasiwasi, hakutaka kunizungumzia ndipo baadaye akaniambia watoto wetu wamezama majini,” akasema Bi Akinyi, ukiwa uliomvaa ukiwa dhahiri machoni pake.

“Nilipowasili niliwapata watoto wanne wameaga dunia na miili yao imelazwa kando kando. Walikuwa wameondolewa majini,” akasema huku machozi yakimtiririka.

Wavulana hao walioaga katika kisa hicho cha kuatua moyo na kuamsha hisia za maombolezo ni Wayne Otieno mwenye umri wa miaka 15, Kelly Otieno (12), Chris Brown Otieno (10) na Hillary Otieno (8).

Bi Akinyi aliondoka nyumbani mnamo Jumapili saa sita mchana na kuelekea kazini na aliwaacha wakisoma.

Naye mumewe Felix aliondoka nyumbani saa 10 kuenda kazini na akawaacha vijana hao wakitazama runinga.

Saa chache baadaye, wanne hao walikuwa wameangamia kwenye tukio ambalo ni la kushangaza mno.

Wayne alikuwa Gredi ya tisa na alitaka kuwa daktari, Kelly na Chris walizungumzia sana kuwa rubani naye Hillary, alikuwa Gredi ya 3.

“Nimesalia na mtoto mmoja ambaye hata hajafikisha umri wa mwaka mmoja,” akasema Bi Akinyi akiwa amelemewa na uzito wa tukio hilo.

Kwa mujibu wa jamaa na majirani, vijana hao walitoka nyumbani wakiwa wamebeba mitungi kuchota maji na timbo ambako walikufia ni mbali kidogo kutoka nyumbani kwao.

Timbo hilo lilikuwa limejazwa baada ya mchanga kuchimbwa miaka mingi. Lilijaa kutokana na maji ya mvua.

“Nilipigiwa simu na nilipofika nyumbani nilienda kwenye timbo na kupata mitungi imejaa maji na nguo pembeni. Wavulana wangu hawakuwa popote ndipo tukaanza kuwasaka,” akasema.

“Hili ni tukio ambalo limenishtua, bado nimeshangaa na siwezi amini wavulana wangu wameaga dunia,” akaongeza Bw Otieno.

Mashahidi walisimulia kuwa kijana mmoja aliangukia timbo hilo, kisha nduguye akajaribu kumwokoa ndipo wengine nao wakafuata.

“Huwa wanachota maji kwenye kisima cha karibu, sijui kipi kiliwafanya waende matimboni,” akaongeza.

Wakazi wamelalamika kuwepo kwa matimbo hayo wanayosema yalibakia wakati wa ujenzi wa barabara ya Kisumu-Kakamega na hayajajazwa.