Makala

Mvua kubwa na radi yatarajiwa kutwanga maeneo mengi Kenya Aprili nzima

Na BENSON MATHEKA April 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MVUA inayoendelea nchini inatarajiwa kunyesha katika maeneo mengi ya Kenya mwezi mzima wa Aprili, huku kiwango kikitarajiwa kuongezeka na kusababisha hatari ya mafuriko.

Hii ni kulingana na Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini.

Kwa mujibu wa utabiri huo, maeneo ya Bonde la Ufa, eneo la Ziwa Victoria na maeneo jirani yatapokea mvua kubwa mara kwa mara, huku radi zikitarajiwa katika baadhi ya maeneo, hasa karibu na mipaka ya Uganda na Sudan Kusini.

Kaunti za Nairobi, Nyandarua, Laikipia, Kiambu, Embu na maeneo mengine ya mashariki mwa Bonde la Ufa zinatarajiwa kupokea mvua zaidi ya wastani, ikiambatana na baridi wakati wa mchana na mawingu mazito.

Maeneo ya kaskazini mashariki kama Marsabit, Wajir na Mandera yanatarajiwa pia kupokea mvua zaidi ya wastani, huku baadhi ya sehemu za Turkana na Samburu zikitarajiwa kupata mvua ya wastani au chini ya wastani.

Kando na hayo, inatabiriwa kuwa maeneo ya Ukanda wa Pwani nao huenda yasipokee mvua sana ikilinganishwa na maeneo yaliyotajwa hapo juu.

Idara ya hali ya hewa imewaonya wakazi wa maeneo ya nyanda za juu mashariki na magharibi mwa Bonde la Ufa, pamoja na eneo la Ziwa Victoria na kaskazini magharibi mwa nchi, kujiandaa kwa mvu.

Wakulima wamehimizwa kuboresha mitaro ya maji mashambani, kufungua njia zilizoziba na kuepuka shughuli zinazobana udongo uliojaa maji ili kulinda mazao.

Idara imesema hali ya hewa itakuwa ya joto na unyevunyevu katika sehemu nyingi za nchi, huku halijoto za mchana zikitarajiwa kuwa kati ya nyuzi joto 20 hadi 32 kwa kiwango cha selsias.

Maeneo ya Pwani na kaskazini mashariki yatashuhudia joto la juu zaidi, huku Mandera ikitarajiwa kufikia nyuzi joto 38.

Nairobi itakuwa na hali ya wastani, joto likitarajiwa kuwa kati ya nyusi joto 14 na 27, huku Mombasa ikifikia hadi nyusi joto 32.

Idara ya hali ya hewa imeonya kuwa mafuriko yaliyoshuhudiwa mwezi Machi yanaweza kujirudia mwezi huu wa Aprili, hasa katika maeneo ambayo tayari yameathirika.

Mamlaka za usimamizi wa maji zimetakiwa kufuatilia kwa karibu viwango vya mito na kuhakikisha mabomba ya maji hayajaziba.

Aidha, mamlaka za barabara zimewekwa katika hali ya tahadhari kutokana na uwezekano wa mvua kuharibu miundombinu.

Maeneo ya Nyeri, Kirinyaga, Murang’a, Nyandarua, Meru, Embu, Tharaka Nithi na Laikipia yanatarajiwa kupokea mvua kubwa katika siku saba zijazo.

Kaunti za Bonde la Ufa Kusini kama Nakuru, Kericho, Narok, Bomet na Nandi pia zimetajwa miongoni mwa zitakazoathirika zaidi.

Wakazi wa eneo la Ziwa Victoria na Bonde la Ufa wanatarajiwa kushuhudia mvua za alasiri, radi na mvua za usiku huku maeneo ya kaskazini mashariki na kaskazini magharibi yakitarajiwa kupata mvua za hapa na pale siku nzima.