Makala

Mwanamume mbunifu ajenga ‘nyumba’ ya taka za plastiki inayoelea baharini

Na KALUME KAZUNGU June 10th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MWANAMUME mbunifu kisiwani Lamu amewaacha wengi vinywa wazi alipoafikia kuishi ndani ya Bahari Hindi katika harakati za kuyatunza mazingira ya majini yasichafuliwe.

Hii ni baada ya mwanamume huyo kwa jina Mansoor Mzee Athman, 47, kuikamilisha nyumba yake aliyoijenga kwa kutumia taka za plastiki alizokusanya kutoka fukwe mbalimbali eneo hilo.

Nyumba hiyo inayoelea baharini imekuwa makazi rasmi ya Bw Mzee ambaye ndoto yake hasa ni kuhakikisha zogo la taka za plastiki zilizosheheni Lamu linamalizwa kabisa.

Kulingana na Bw Mzee, ambaye ni baba wa watoto watatu, harakati zake za kukabiliana na uchafuzi wa mazingira ya ufuoni zilianza tangu mwaka 2009.

Anasema kila wakati yeye huzurura kwenye fukwe kutafuta pkastiki ili kuzitumia kwa ujenzi wa nyumba yake ya kuelea pamoja na mashua.

Mansoor Mzee Athman, 47, akiwa ndani ya nyumba yake inayoelea baharini na aliyojenga kupitia taka za plastiki. Picha|Kalume Kazungu

Taifa Leo ilipotembelea nyumba hiyo ya kuelea ndani ya bahari, karibu na ofisi za misitu kisiwani Lamu, ilimpata Bw Mzee akiwa mwingi wa furaha huku akiwa amejilaza godoroni ndani ya nyumba yake.

Mbali na godoro, pia utapata mito, masufuria ya kupikia, jerikeni za maji na nguo ambacho ni kiashirio tosha kwamba mahali hapo ni makazi ya binadamu.

Anasema alitumia zaidi ya jerikeni na chupa za plastiki zisizopungua 1000 katika kutengeneza nyumba na mashua hiyo ya taka za plastiki.

“Nayafanya haya yote kupunguza kusheheni kwa taka za plastiki kwenye fuo zetu. Hofu yangu ni kuwa endapo watu wataendelea kutupa ovyo taka bila kuelimishwa, huenda kizazi kijacho kikakosa kuona samaki kwani wote watakuwa wameisha kwa sumu ya plastiki,” akasema Bw Mzee.

Anasema hatua yake ya kuishi baharini inatokana na mapenzi yake makuu kuihusu bahari na vyote viijazavyo.

Maamuzi yake pia yalitokana na kwamba kwake ni rahisi kukutana na kutangamana na watu mbalimbali baharini, ikiwemo wavuvi, wasafiri na wengineo, hivyo kupitisha ujumbe kuhusu umuhimu wa kuyatunza mazingira ya baharini.

“Mimi hapa ninawaelimisha waja kwamba waepuke kutupa plastiki baharini. Badala yake, waniletee hizo plastiki hapa kwangu ili niunde nyumba, mashua na vifaa vingine vyenye manufaa mbadala kwetu. Nashukuru kwamba kampeni yangu imeshuhudia ufanisi kwani taka kwenye fuo zetu zimepungua miaka ya hivi karibuni,” akasema Bw Mzee.

Anasema ubunifu wake wa kutengeneza nyumba na mashua za plastiki zinazoelea baharini hakujifunza kupitia elimu ya vyuo ama taasisi kwani yeye alikamilisha masomo ya darasa la nane pekee.

Mansoor Mzee Athman akipiga makasia ya boti alilotengeneza kwa plastiki. Picha|Kalume Kazungu

“Nilipomaliza darasa la nane sikuweza kusonga mbele kimasomo kutokana na umaskini wa familia yetu. Babangu alifariki nikiwa miaka saba pekee. Ila ninaamini maarifa niliyonayo yanafuata damu ya babangu. Alikuwa mhandisi katika meli hadi kufariki kwake mwaka 1990. Ninaamini kazi ya babangu ndiyo ilinipa motisha tangu nikiwa mdogo kabisa, hivyo kuibukia maarifa haya ya kutengeneza vyombo vya baharini,” akasema Bw Mzee.

Anaishukuru familia yake, ikiwemo mkewe, Bi Fatma Omar na wanawe watatu kwa kumpa ruhusa ya kujitosa kikamilifu katika masuala ya mazingira, ikiwemo kutumia muda mwingi akiwa mbali nao akitafuta plastiki, kutengeneza vyombo vya baharini na hata kuishi huko.

Si mara ya kwanza kwa Lamu kuibuka na ubunifu wa kuzikusanya taka za plastiki baharini na kutengeneza vifaa vya matumizi mbadala ili kupiga vita uchafu huo baharini.

Mnamo 2018, Lamu iligonga vichwa vya habari ilipozindua mashua ya kwanza kabisa ulimwenguni kutengenezwa kutumia taka za plastiki.

Mashua hiyo inajulikana kama Flip-Flopi.

Mwaka 2022,  kundi la wanawake wa kisiwa cha Mkokoni, Lamu Mashariki iliibuka na ubunifu wa kutumia taka za plastiki kuunda sehemu za kukaa kujivinjari na pia kutumia taka hizo kupambia nyumba zao.

Mwaka 2024, wakazi wa kisiwa cha Pate pia walitengeneza hoteli kutoka kwa taka za plastiki zilizokusanywa baharini.

Juhudi zote zinatajwa kusaidia kupunguza mrundiko wa taka kwenye mazingira ya baharini kwa kiwango cha karibu asilimia 70.