• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 4:42 PM
NDIVYO SIVYO: ‘Makanga’ au ‘manamba’ hayafai katika miktadha rasmi

NDIVYO SIVYO: ‘Makanga’ au ‘manamba’ hayafai katika miktadha rasmi

Na ENOCK NYARIKI

Makanga na manamba ni maneno mawili yatumiwayo sana katika mazungumzo ya watu kuwarejelea wafanyakazi katika magari ya usafiri. Baadhi ya watu huyatumia maneno hayo kwa kutojua maneno mengine sanifu yanayoweza kutumiwa kuwarejelea wafanyakazi hao ambao huwa na majukumu tofauti.

Katika maeneo ya mjini, maneno hayo hutumiwa kwa uchangamano mno hivi kwamba mtu anaweza kudhani kuwa anayerejelewa ni mtu mmoja. Kwa watu wengine, ‘manamba’ na ‘makanga’ ni maneno yatumiwayo kuwabeza wafanyakazi hao wa matatu yamkini kutokana na tabia zao zilizochipuza katika mazingira yao magumu ya utendakazi.

Nimewahi kuliangazia neno manamba katika safu tofauti. Tulisema kuwa hili ni neno sanifu la Kiswahili ila matumizi yake ya kwanza hayakuhusiana na mfanyakazi katika chombo cha usafiri.

Lilitumiwa kuwarejelea wafanyakazi wa muda fulani katika mashamba makubwa. Hii ni fasili ya toleo la kwanza kabisa la Kamusi ya Kiswahili Sanifu iliyojulikana hadi mwanzomwanzo wa karne ya ishirini na moja.

Kamusi zilizoanza kuandikwa katika karne ya ishirini na moja zimeikumbatia maana ya pili ya neno hilo jinsi inavyotumiwa mtaani kurejelea wafanyakazi katika magari ya usafiri ambao kazi yao kubwa ni kuwaita watu waingie kwenye magari.

Yamkini ile hulka ya watu hao ya kuzitaja nambari za magari kila wanapowaita watu kuyaabiri ndiyo iliyowafanya kupewa jina hilo manamba. ‘Namba’ ni neno jingine ambalo limepata ukubalifu kwa maana ya nambari.

Nayo dhana ‘manamba’ ni lugha ya mtaani ya kuutajia wingi wa namba. Nadharia nyingine inayoweza kuelezea kubuniwa kwa neno hilo ni ile ya utaratibu maalumu unaofuatwa na watu hao katika kuyajaza magari.

Neno makanga halimo kwenye kamusi ingawa baadhi ya vyombo vya habari mpaka sasa hulitumia kwa maana ya mfanyakazi katika gari la abiria ambaye kazi yake ni kuwatoza watu nauli. Ijapokuwa neno kondakta ambalo hutumiwa kumrejelea mfanyakazi huyo si geni, watu wengi hupendelea kutumia makanga kutokana na mazoea.

Kanga ni ndege wa mwituni mwenye rangi nyingi afananaye na kuku. Je, kunao uwezekano kuwa asili ya neno makanga lilitokana na mvao wa wafanyakazi wenyewe hasa kabla ya kuibuliwa kwa sare ya makondakta?

Alhasili, anayepakia na kupakua mizigo kwenye chombo cha usafiri ni utingo au taniboi. Anayewatoza abiria nauli ni kondakta. Anayewaita watu waingie kwenye gari ni mpigadebe. Manamba na makanga hayajapata ukubalifu kamili kwa maana ya wafanyakazi wa matatu. Yasitumiwe katika miktadha rasmi.

You can share this post!

KAULI YA MATUNDURA: Mkangi aliandika Walenisi kwa mafumbo...

Chipu yabandua Madagascar kutinga fainali Namibia

adminleo