Makala

Njaa, umaskini wafanya familia ziokote mahindi yaliyomwagika yakipakiwa mpakani Tanzania

Na LUCY MKANYIKA June 11th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

KWA miezi kadha sasa, Kenya imekumbwa na uhaba wa mahindi, hali iliyosababisha wafanyabiashara wa nafaka kuhamisha shughuli zao kutoka Magharibi na Bonde la Ufa hadi Taveta, Taita Taveta karibu na mpaka wa Tanzania.

Ingawa uhaba huu umewaathiri wauzaji na wasagaji wa mahindi pamoja na wakazi wa maeneo ya ukulima wa bidhaa hiyo, umekuwa tegemeo jipya kwa baadhi ya wakazi wa eneo la Taveta.

Katika siku za hivi majuzi, ardhi ya kiwanja cha ndege cha Taveta imegeuka kuwa kitovu cha shughuli za ukaushaji wa mahindi yanayoletwa kutoka nchi jirani ya Tanzania kupitia mpaka wa Taveta/Holili.

Mahindi hayo, yanapofika nchini, huwa na unyevunyevu wa takriban asilimia 16, hivyo lazima yakaushwe hadi kiwango kinachohitajika cha asilimia 13 au chini kabla ya kusafirishwa kwa viwanda vya kusaga unga.

Huku hayo yakiendelea, baadhi ya familia maskini za eneo la Taveta zimekuwa zikipata fursa ya kuokota punje zilizomwagika, hali inayowasaidia kujikimu kila siku.

Bw Peter Kamuti, 70, ni mmoja wa wakazi wanaotegemea mahindi yaliyoanguka ili kupata chakula cha kila siku.

Alisema kwa siku yeye hukusanya hadi kilo mbili za mahindi ambazo husaga na kupata unga wa ugali kinyume na awali ambapo alitegemea wahisani.

Wauzaji mahindi wapima kiwango cha unyevu kwa mahindi katika uwanja mdogo wa ndege wa Taveta Juni 9, 2025. Wafanyabiashara hao hununua mahindi kutoka Tanzania kufuatia uhaba unaoshuhudiwa nchini. Picha|Lucy Mkanyika

“Shida ndio hunifanya nije hapa kila siku. Sina chakula, na kwa sababu ya umri wangu, siwezi kufanya kazi za sulubu,” alisema Bw Kamuti.

Mkazi mwingine, Bi Eliza Kasua, mama wa watoto wanne, alisema uhaba wa vibarua umemlazimu kutafuta njia mbadala ya kupata chakula.

Alisema kuwa amekuwa akifanya vibarua vya kulima au kufua nguo lakini kwa sasa havipatikani.

“Naja hapa kila siku kwa sababu sitaki watoto wangu walale njaa. Maisha yamekuwa magumu sana na vibarua hakuna,” asema Bi Kasua.

Kwa Bw Wambua Mulwa, hali hii imekuwa njia pekee ya kujikimu yeye na familia yake.

“Hakuna kazi. Nikipata kazi, sitakuja hapa tena. Kila siku nakusanya hadi kilo kumi za mahindi,” asema Bw Mulwa.

Bw Khalid Ahmed, wakala wa mahindi wa kampuni ya Kitui Millers, alisema kuwa nchi ya Tanzania imekuwa tegemeo kubwa kwao.

Alisema kuwa mahindi yanapofika Taveta, unyevunyevu wake huwa karibu asilimia kubwa, hivyo kuwalazimu kuyakausha hadi kufikia kiwango kinachohitajika kabla ya kusafirishwa hadi Mombasa kwa kampuni za kusaga mahindi.

Kwa sasa, uhaba wa mahindi unatarajiwa kudumu hadi Oktoba, wakati mavuno mapya kutoka mashamba ya humu nchini yatakapokuwa tayari.

“Tunachukua mahindi kutoka soko ya Holili na kuyaleta Taveta ili yakauke. Tutaendelea hivi hadi mwezi wa Oktoba ambapo mahindi ya humu nchini yatakuwa tayari kuvunwa,” alisema Bw Ahmed.

Wakati huohuo, zaidi ya watu 1,000 kutoka Magharibi na Bonde la Ufa wamefuata wafanyibiashara hadi Taveta wakitafuta kazi za muda katika kiwanja hicho cha ukaushaji wa mahindi.

Bw John Wambula, mchukuzi kutoka Kitale, alisema kuwa wamehamia Taveta baada ya shughuli za uuzaji mahindi kusimamishwa kutokana na ukosefu wa bidhaa hiyo katika eneo hilo.

“Tumekuja Taveta kwa sababu ni lazima tutafute kazi. Kazi yetu ni kupakua, kukausha na kufunga magunia ya mahindi baada ya kukauka,” asema Bw Wambula.

Mbali na wafanyakazi hao wa muda, wachuuzi wa vyakula wa eneo hilo vilevile wamepata fursa ya kuuza kwa wanaofanya kazi katika uwanja huo.