Akili MaliMakala

Ofisi mpya ya uwakilishi Dubai kuboresha soko la maparachichi

February 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

UFUNGUZI wa ofisi mpya ya uwakilishi ya Chama cha Kitaifa cha Biashara na Viwanda Kenya (KNCCI) Jijini Dubai, inatarajiwa kuimarisha kwa kiasi kikubwa biashara kati ya Kenya na nchi za Uarabuni za Mashariki ya Kati, hasa wanaouza bidhaa za kilimo na mifugo katika mataifa hayo.

Zao la avokado, pia parachichi, ambalo Kenya huuza sana nchi za Uarabuni wafanyabiashara na wakulima wanatarajia kunufaika pakubwa na ufunguzi huo.

Aidha, afisi hiyo inapaniwa kuangazia visa vya utapeli vinavyosakatwa katika nchi za Milki ya Uarabuni (UAE) kwa wauzaji wa bidhaa, ambao KNCCI inasema hushuhudia hasara ya kifedha.

Avokado tayari kuingia sokoni. Picha|Sammy Waweru

Chama hicho kinakadiria makontena yasiyopungua 156 ya mizigo hupotea kila mwaka, wafanyabiashara kutoka Kenya wanaoyauza humo wakikosa kulipwa na wengine kutapeliwa.

“Sekta ya Mifugo, bidhaa kati ya asilimia 25 hadi 30 zinazouzwa UAE na Saudi Arabia zimekosa kulipwa.

Tukifanya mahesabu, ni hasara ya Sh6 bilioni inayokadiriwa kila mwaka,” anasema Rais wa KNCCI Dkt Erick Rutto.

Hata hivyo, kulingana na Dkt Rutto, ufunguzi wa ofisi ya uwakilishi ya chama hicho itasaidia kuondoa mgogoro huo.

Wafanyakazi wakipakia avokado kwenye makatoni, tayari kupelekwa masoko ya nje. Chama cha Kitaifa cha Biashara na Viwanda Kenya (KNCCI) kimezindua ofisi mpya Dubai, hatua inayotarajiwa kukabiliana na visa vya utapeli. Picha|Sammy Waweru

“Umewadia wakati tuokoe wafanyabiashara na wakulima wetu,” anaelezea.

Ofisi hiyo, ilifunguliwa wiki iliyopita na hafla rasmi ya hatua hiyo ikaandaliwa jijini Nairobi.

KNCCI inasema hatua hiyo ni mojawapo ya mikakati kukuza uhusiano wa Kenya na UAE kibiashara – kwa mauzo ya nje ya nchi, na kwamba itatumika kama daraja la kibiashara kati ya wauzaji wa Kenya na wanunuzi katika eneo la Ghuba.

Itatoa msaada wa karibu kutatua migogoro, upatikanaji wa taarifa za masoko, urahisishaji wa biashara na uuzaji wa bidhaa za Kenya.

Dubai ni lango muhimu kuelekea Mashariki ya Kati na Asia, na kuifanya kuwa kitovu cha kimikakati kwa wauzaji wa Kenya wanaotaka kupanua masoko yao zaidi ya yale ya jadi.

Mfanyakazi wa Kakuzi PLC akionyesha maparachichi yaliyopakiwa tayari kuingia sokoni. Picha|Sammy Waweru

Muungano wa Washirika wa Avokado Kenya, ndio, Avocado Society of Kenya, umekaribisha hatua ya uzinduzi wa ofisi ya uwakilishi wa KNCCI Dubai, ukisema hilo limejiri wakati ufaao ikingatiwa kuwa sekta ya parachichi inakua kwa kasi.

“Kwa miaka mingi, wauzaji wa nje ya nchi wamekuwa wakipata hasara kubwa kutokana na kucheleweshwa kwa malipo na migogoro isiyotatuliwa na wanunuzi wa ng’ambo, hususan katika masoko ambako taasisi za Kenya hazikuwa na uwepo wa kutosha. Uzinduzi wa ofisi ya uwakilishi ya KNCCI utaletea sekta ya parachichi afueni,” Afisa Mkuu Mtendaji muungano huo, Ernest Muthomi, akaambia Akilimali kwenye mahojiano ya kipekee.

Muthomi alisema ukosefu wa kituo cha kuaminika cha mawasiliano katika masoko ya nje, aghalabu umewaacha wauzaji kwenye hatari baada ya kusafirisha mizigo yao, huku baadhi wakitapeliwa na wengine kukosa kulipwa na wanunuzi.

Kiwanda cha Kakuzi, Murang’a shughuli za upakiaji na ukaguzi wa avokado zikiendelea. Picha|Sammy Waweru

Alisifia hatua ya ufunguzi wa ofisi hiyo, akibainisha kuwa sasa itatoa mpangilio kwa wafanyabiashara kushirikiana na wanunuzi, jambo litakalosaidia kupunguza hasara, hatari na kuboresha uwajibikaji.

“Itakuwa na jukumu kuu katika kuwezesha malipo ya haraka, kuthibitisha uhalali wa wanunuzi na kuingilia kati pindi migogoro inapozuka kati ya wauzaji wa Kenya na waagizaji kutoka nje,” alieleza.

Hatua hiyo, Muthomi alisema, inatarajiwa kurejesha imani katika mchakato wa mauzo ya bidhaa nje ya nchi, hasa msimu wa mavuno wa maparachichi unapokaribia.

Jonathan Kipruto, meneja Kakuzi akifuatilia shughuli za upakiaji avokado kwenye makatoni. Picha|Sammy Waweru

Kenya ni miongoni mwa wauzaji wakuu wa avokado Barani Afrika, huku UAE ikijitokeza kama soko kubwa la bidhaa hiyo.

Hata hivyo, ushindani kutoka kwa nchi zinazozalisha maparachichi umeongezeka, na hivyo kuongeza shinikizo katika bei na viwango vya ubora.

Avokado Society of Kenya ina wanachama wasiopungua 160 – ambao ni kampuni na mashirika yanayouza maparachichi UAE, na Muthomi anaamini uzinduzi wa ofisi ya KNCCI Dubai utawaletea afueni kimapato.