Mbinu za kusahau ex wako haraka
Baada ya kuachana na mpenzi, wengi hujikuta wakifanya jambo linalowaumiza zaidi: kuendelea kuangalia mitandao ya kijamii ya aliyekuwa mpenzi wao.
Ingawa inaweza kuonekana kama tabia isiyo na madhara, wataalamu wa afya ya akili wanasema inaweza kuchelewesha uponyaji wa kihisia na kukuacha kwenye mzunguko wa maumivu.
Kulingana na wanasaikolojia, hamu ya kufuatilia maisha ya aliyekuwa mpenzi wako ni ya kibinadamu, hasa pale maumivu ya kuachwa bado ni mapya.
Unapotafuta kuepuka mawazo mazito, kupata “ufafanuzi” au kuthibitisha kama mwenzako amepata mwingine, mitandao ya kijamii huwa mtego rahisi.
“Mara nyingi, kuangalia mitandao ya kijamii ya aliyekuwa mpenzi wako huchochea hisia zilezile za hofu au mshtuko kama unapokutana naye ghafla,” anasema mwanasaikolojia Roxy Zarrabi.
Anaongeza kuwa hata kama unatarajia kumuona mtandaoni, chapisho moja linaweza kukushtua, kukuumiza au kukuacha na maswali mengi zaidi.
“Hii huamsha hisia za mwili, na ndipo mzunguko hatari wa kuendelea kuchunguza mitandao yake huanza,” anafafanua.
Utafiti mmoja uliofanywa na kampuni ya Specops Soft unaonyesha ukubwa wa tatizo hili. Asilimia 27 ya washiriki 2,568 walikiri kuendelea kuingia kwenye akaunti za mitandao ya kijamii za waliokuwa wapenzi wao hata baada ya kuachana.
Wataalamu wanasema hali hii huongezeka zaidi unapokuwa na wasiwasi au huzuni, kwani mitandao ya kijamii huongeza tabia ya kujilinganisha na wengine, jambo linaloweza kuathiri vibaya hali ya moyo.
Hata hivyo, kuna njia za kujinasua. Roxy Zarrabi anashauri watu wanaopitia kipindi cha kuachana kuanza kwa hatua ndogo. “Badala ya kujaribu kuacha ghafla, jaribu kusubiri dakika tano kabla ya kuangalia akaunti ya aliyekuwa mtu wako,” anasema.
Anaeleza kuwa kuchelewesha tamaa hiyo kunasaidia kutenganisha msukumo na tendo lenyewe, na kadri unavyoendelea kufanya mazoezi, ndivyo utakavyoweza kuongeza muda huo hadi dakika 10 au 20, na hatimaye kuacha kabisa.
Pia anashauri mtu ajiulize maswali muhimu kabla ya kubonyeza simu: Unajaribu kuepuka hisia gani? Ni jambo gani muhimu unalikwepa kwa kuangalia mitandao yao? Ulihisiaje mara ya mwisho ulipofanya hivyo? Na kama ungekuwa unamshauri rafiki yako aliye katika hali kama yako, ungemwambia afanye nini?
Njia nyingine ni kutafuta shughuli mbadala. Badala ya kuangalia mitandao ya kijamii ya mpenzi wako wa zamani, unaweza kumpigia simu rafiki, kwenda matembezi mafupi, kuandika hisia zako au kutazama kwa dakika chache kipindi unachokipenda.
Kuwa na mpango tayari, kama vile kuandika: “Nikihisi hamu ya kuangalia akaunti ya aliyekuwa mchumba wangu, nitampigia fulani au nitafanya shughuli hii,” kunaweza kusaidia sana.
Zarrabi pia anashauri watu waache kuangalia uhusiano uliopita kwa miwani ya kumbukumbu nzuri pekee. “Wengi hujikita katika kumbukumbu za furaha pekee baada ya kuachana, jambo linaloongeza maumivu,” anasema.
Tafiti zinaonyesha kuwa kufikiria kwa makusudi sababu zilizofanya uhusiano kuvunjika, pamoja na kasoro za aliyekuwa mpenzi wako, kunaweza kupunguza hisia na kusaidia kupona.
Kuhusu hitaji la “kusahau”, mwanasaikolojia huyo anasema si lazima litoke kwa mpenzi wako wa zamani. Unaweza kufanya hivyo wewe mwenyewe kwa kuandika barua ya kumuaga, hata kama hutaituma, ili kutoa hisia zote ulizoshindwa kusema.
Hatimaye, asema Zarrabi, kuweka mipaka ya kidijitali ni muhimu. Ikiwa huwezi kumzuia aliyekuwa mpenzi wako moja kwa moja, unaweza kumnyamazia, kumzuia kwa muda au hata kuzima akaunti zako za mitandao ya kijamii kwa kipindi fulani.
Kwa jumla, aeleza, kuachana ni safari ya uponyaji. Kuendelea kuangalia maisha ya aliyekuwa mpenzi wako mtandaoni kunaweza kuifanya safari hiyo iwe ndefu na yenye maumivu zaidi.
Kupitia mikakati sahihi na kujipa muda, inawezekana kuachilia yaliyopita na kujielekeza kwenye maisha mapya yaliyo bora.