Raila apinga Ruto kukatiziwa muhula
KIONGOZI wa ODM Raila Odinga anataka Mahakama ya Juu kutupilia mbali kesi iliyowasilishwa na Wakenya watatu wanaotaka tafsiri ya Katiba na uamuzi kwamba Uchaguzi Mkuu ujao ufanyike Agosti 2026 badala ya 2027.
Wakati huo huo, Mwanasheria Mkuu Dorcas Oduor amesema ananuia kuwasilisha pingamizi dhidi ya kesi hiyo. Mwanasiasa wa upinzani ambaye pia ni mfanyabiashara, Jimmy Wanjigi, mmoja wa watu 10 waliowasilisha nia ya kushiriki kesi hiyo, pia amewasilisha stakabadhi mahakamani akiomba majaji wa Mahakama ya Juu kuendelea na kesi hiyo na kutoa uamuzi wa haraka kutokana na “mkanganyiko uliopo na hali ya wasiwasi inayoenea nchini.”
Walalamishi katika kesi hiyo,Dkt Owiso Owiso (wakili), Khelef Khalifa (mtetezi wa haki za binadamu), na Ashioya Biko (wakili) wanataka mJaji Mkuu Martha Koome na jopo lake kutoa uamuzi kuhusu tarehe halisi ya uchaguzi ujao wa urais.
Wanataka Mahakama iamue kuwa uchaguzi unapaswa kufanyika Agosti 2026, “ikiwa ni mwaka wa tano baada ya uchaguzi wa 2022,” na si mwaka wa 2027 kama ilivyopangwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC).
Kwa mujibu wao, kufanya uchaguzi tarehe yoyote tofauti na Jumanne ya pili ya Agosti katika mwaka wa tano baada ya Agosti 9, 2022, kutakuwa ni kuongeza muda wa utawala wa Rais William Ruto kinyume cha Katiba.
Hata hivyo, Bw Odinga, ambaye pia amejiunga katika kesi hiyo, ameomba Mahakama kutupilia mbali kesi hiyo akisema ni matumizi mabaya ya mchakato wa mahakama. Anaamini pia kuwa Mahakama ya Juu haina mamlaka ya kushughulikia suala hilo.
“Kesi hii ni matumizi mabaya ya mchakato wa mahakama na walalamishi hawajaonyesha mazingira ya kipekee yanayoweza kuhalalisha Mahakama hii kutumia mamlaka yake katika hatua hii,” alisema.
Anadai walalamishi walikimbilia Mahakama ya Juu mapema mno kwani Uchaguzi Mkuu hauhusiani na urais pekee bali pia unahusu nyadhifa zote zinazochaguliwa: Wabunge, Maseneta, Wawakilishi wa Wanawake, Magavana, na Wajumbe wa Kaunti.
Kupitia kwa wakili wake Paul Mwangi, Bw Odinga anasema suala la tarehe ya uchaguzi tayari lilishajadiliwa na kuamuliwa na Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufaa mara sita kupitia kesi zilizowasilishwa na Okiya Omtatah (Seneta wa Busia), Paul Njoroge (aliyekuwa Seneta aliyeteuliwa), na John Harun Mwau (aliyekuwa Mbunge wa Kilome), miongoni mwa wengine.
“Masuala yaliyoibuliwa katika kesi hii tayari yameamuliwa kwani suala ya tarehe ya uchaguzi mkuu na namna ya kuhesabu muda wake limesikilizwa na kuamuliwa na mahakama mbalimbali,” alisema wakili Mwangi.
Alinukuu uamuzi wa Mahakama ya Rufaa uliobainisha kuwa “tarehe thabiti na inayojulikana ya uchaguzi (‘Jumanne ya pili ya Agosti kila baada ya miaka mitano’) ilikusudiwa kukuza Kifungu cha 38 cha Katiba kinachohusu haki za kisiasa za wananchi.”
Kesi hiyo ilipotajwa mbele ya Naibu Msajili wa Mahakama ya Juu, Bernard Kasavuli, Mwanasheria Mkuu alipewa siku tatu kuwasilisha pingamizi lake na kukabidhi nakala pande zote. Jimmy Wanjigi, mwanasiasa wa upinzani, aliwasilisha hati ya kiapo akiunga mkono kesi ya walalamishi kwa hoja kuwa “masuala yaliyoibuliwa ni ya msingi kwa demokrasia ya kikatiba ya Kenya na yanahitaji uamuzi wa haraka na wa mwisho.”
Anasema Mahakama ya Juu inapaswa kutoa uamuzi haraka kuhusu suala hilo kwa kuwa kuna wasiwasi mkubwa na mkanganyiko..
“Mkanganyiko uliopo, wasiwasi mkubwa na hali ya kutokuwa na uhakika kuhusu tarehe ya uchaguzi wa urais ujao, bila shaka ni tishio kubwa na la dharura kwa utaratibu wa kikatiba na linaweza kuingiza nchi katika machafuko ya kisiasa yasiyo ya lazima,” alisema Bw Wanjigi.
Kupitia kwa wakili wake Willis Otieno, Bw Wanjigi anasema kuna utata unaosababisha uvumi na unaweza kudhoofisha imani ya umma katika mchakato wa uchaguzi, hivyo kuhatarisha uwiano wa kitaifa na uthabiti wa kiuchumi.
Anasisitiza kuwa Mahakama ya Juu ina mamlaka ya kusikiliza na kuamua kesi hiyo kwa kuwa ni mzozo wa kabla ya uchaguzi unaohusu tarehe ya uchaguzi wa urais, na hivyo uko ndani ya mamlaka ya Mahakama ya Juu.
Katika hoja zao, walalamishi wanasema kwa kuzingatia namna ya kuhesabu muda kikatiba, mwaka wa kwanza baada ya uchaguzi wa 2022 ulimalizika Agosti 8, 2023, mwaka wa pili Agosti 8, 2024, wa tatu Agosti 8, 2025, na wa nne Agosti 8, 2026.
Hivyo, mwaka wa tano utaanza Agosti 9, 2026 hadi Agosti 8, 2027. “Iwapo fomula hiyo ya kuhesabu muda ni sahihi, na walalamishi wanasisitiza kuwa ni sahihi, basi mwaka wa tano tangu uchaguzi wa Agosti 9, 2022, unaanza Agosti 9, 2026,” walisema.