Makala

Rais Ruto adharau mahakama kwa kuteua makamishna wa IEBC

Na CHARLES WASONGA June 11th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MVUTANO mwingine kati ya Serikali Kuu na Idara ya Mahakama unanukia baada ya Rais William Ruto kudharau agizo la Mahakama Kuu na kuteua rasmi mwenyekiti na makamishna wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC).

Kupitia tangazo kwenye toleo nambari 7724 la Gazeti Rasmi ya Serikali la Juni 10, 2025, Dkt Ruto alimteua rasmi Erustus Edung Ethekon kuwa mwenyekiti wa tume hiyo.

Aidha, Rais aliwateuwa Bi Ann Njeri Nderitu, Moses Alutalala Mukhwana, Hassan Noor Hassan, Francis Odhiambo Aduol na Bi Fahima Araphat Abdullah kuwa makamishna wa IEBC.

“Saba hao watahudumu katika tume hiyo kwa kipindi cha miaka sita,” Dkt Ruto akasema kwenye tangazo hilo.

Kiongozi wa taifa amechukua hatua hiyo siku moja baada ya Jaji Mkuu Martha Koome kuteua jopo la majaji watatu wa Mahakama Kuu kusikiza kesi inayopinga uhalali wa uteuzi watu hao saba kuongoza IEBC.

Mnamo Jumatatu wiki hii, Juni 9, 2025, majaji hao Roselyne Aburili, John Chigiti na Bahati Mwamuye walitenge Juni 23, 2025 kama siku ya kusikizwa kwa kesi hiyo iliyowasilishwa na wanaharakati Boniface Mwangi na Kelvin Omondi.

Mnamo Mei 29, 2025, Jaji wa Mahakama Kuu Lawrence Mugambi alitoa nafasi kwa Bunge kuwapiga msasa Bw Ethekon na wenzake sita, lakini akaamuru kuwa wasiteuliwe rasmi na kuapishwa kabla ya kesi hiyo kusikizwa na kuamuliwa.

Na mnamo Juni 4, 2025 Bunge la Kitaifa lilipitisha ripoti ya Kamati ya Haki na Masuala ya Kisheria (JLAC) iliyopendekeza kuteuliwa kwa saba hao.

Akiwasilisha ripoti kuhusu shughuli ya kuwapiga msasa wateule hao saba, iliyofanyika Jumamosi Mei 31, 2025, mwenyekiti wa JLAC George Murugara alisema kamati yake iliridhika na ufaa wa watu hao kushikilia nyadhifa hizo.

“Kwa hivyo, kwa mujibu wa mahitaji ya Kipengele cha 252 (b) cha Katiba, kamati hii inaidhinisha uteuzi wa Erastus Edung Ethekon  kuwa Mwenyekiti na Ann Njeri Nderitu, Moses Alutalala Mukhwana, Mary Karen Sorobit, Hassan Noor Hassan, Francis Odhiambo Oduol na Bi Fahima Arafat Abdallah kuwa wanachama wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC),” Bw Murugara, ambaye ni Mbunge wa Tharaka, akasema.

Wabunge waliidhinisha ripoti hiyo kwa kauli moja na kutoa nafasi kwa uteuzi wa Bw Ethekon na wenzake, lakini baada ya kesi iliyoko mahakamani kusikizwa na kuamuliwa.

Wadadisi wanasema huenda Jaji Mkuu Koome akadinda kuongoza sheria ya kuapishwa na Bw Ethekon na makamishna hao sita ikizingatiwa ndiye aliteua jopo la majaji watatu kuanza kusikiza kesi ya kupinga uhalali wa uteuzi huo.

“Bila shaka Rais Ruto kwa mara nyingine amedharau mahakama kwa kuteua makamishna wa IEBC kinyume na agizo lililotolewa na Jaji wa Mahakama Kuu Lawrence Mugambi. Huu ni ukiukaji Katiba na kuingilia uhuru wa mahakama na bila shaka Jaji Mkuu Koome hawezi kuwaapishwa Bw Ethekon na wenzake ili kupata kibali rasmi  cha kuanza kuchapa kazi,” anasema wakili Peter Mwamu.

Kulingana na mwanasheria huyo kudinda kwa Koome kutafufua uhasama mwingine kati ya matawi hayo mawili ya Serikali.

“Wasipoapishwa na Jaji Mkuu, Bw Ethekon na wenzake hawawezi kuanza kazi. Na wakiingia afisini, utendakazi wao hautatambuliwa kisheria na kikatiba,” Bw Mwamu akaongeza.