Sababu ya IEBC kutaka baadhi ya Wakenya kusajiliwa upya kupiga kura 2027
Mamilioni ya Wakenya waliosajiliwa kama wapiga kura kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2013 watahitajika kusajiliwa upya na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC).
Tume hiyo ilitangaza hayo katika taarifa iliyotoka Ijumaa, Aprili 2026.
Katika taarifa hiyo Mwenyekiti wa IEBC, Erastus Ethekon, alisema: “Kama ulisajiliwa kama mpiga kura kati ya 2012 na 2026, huna haja ya kusajiliwa upya.”
Tume ya uchaguzi imefafanua kuwa usajili mpya ni kuhakikisha wapiga kura waliosajiliwa mapema wanajumuishwa katika Sajili ya Kielektroniki ya Wapiga Kura (RoV) ya sasa.
IEBC inasema kuwa rejista ya sasa ya kibiometriki ilianzishwa mwaka 2012 kufuatia mabadiliko makuu ya kisera ya uchaguzi, na hivyo wapiga kura waliosajiliwa kabla ya wakati huo hawajajumuishwa kwenye rejista hii ya sasa.
“Kwa hivyo, watu waliokuwa wamesajiliwa kama wapiga kura kabla ya 2012 hawajajumuishwa kwenye RoV ya sasa isipokuwa kama walijisajili upya baadaye,” alisema Bw Ethekon.
Hii inamaanisha kuwa Wakenya wote waliosajiliwa kabla ya Novemba 2012, wakati orodha ilipofungwa kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa Agosti 2013, lazima wajumuishe taarifa zao za kibiometriki upya ili kuhakikisha majina yao yapo kwenye mfumo na waweze kupiga kura mwaka ujao.
“Matukio ya 2007/08 yalisababisha mageuzi katika sekta nyingi, ikiwemo mfumo wa uchaguzi. Wale waliosajiliwa kabla ya 2012 wanaweza kuhitajika kusajiliwa upya kuhakikisha majina yao yapo kwenye mfumo.”
Aliongeza: “Kama ulisajiliwa kati ya 2012 na 2026, huna haja ya kusajiliwa upya.”
Kulingana na Ethekon, orodha ya wapiga kura inayotumika sasa ilitengenezwa baada ya mchakato wa kuweka mipaka wa 2012, ukiambatana na mageuzi ya uchaguzi yaliyoanzisha usajili wa wapiga kura kibiometriki na kubadilisha jinsi Wakenya wanavyosajiliwa.
“Data ya kabla ya 2012 ilifutwa kisheria,” alisema, akiongeza kuwa katika zoezi la usajili wa 2012, tume ilisajili wapiga kura wapya wapatao milioni 14.5.
Orodha hiyo ilikua hadi 19.6 milioni mwaka 2017 na 22.1 milioni mwaka 2022 kadri Wakenya walivyosajiliwa zaidi.
“Tunatarajia kuongeza idadi hadi takriban milioni 28.8 kupitia zoezi hili linaloendelea,” Ethekon alisema.