Serikali yazindua miradi ya kuchimba visima kukabili uhaba wa maji Kisumu Magharibi
WAKAZI wa eneo la Kisumu Magharibi wamepata afueni baada ya Mamlaka ya Kitaifa ya uhifadhi wa Maji (NWHSA) kuzindua miradi ya uchimbaji visima ili kukabiliana na uhaba wa maji safi.
Uzinduzi huo uliofanyika Jumatano ni sehemu ya mpango wa serikali wa Maji Mashinani unaolenga kuhakikisha wananchi wanapata maji safi karibu na makazi yao.
Kwa miaka mingi, wakazi wa eneo hilo wamekuwa wakilazimika kutegemea maji kutoka Ziwa Victoria, hali ambayo imewahatarisha kiafya na hata kuhatarisha maisha yao.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Afisa Mkuu Mtendaji wa NWHSA, Julius Mugun, alisema serikali imejizatiti kuhakikisha kila Mkenya anapata maji safi na salama bila ubaguzi.
Alisema wahandisi wataendelea kusimamia mradi huo hadi ukamilike na kusisitiza kuwa si mradi wa kisiasa bali ni suluhisho la kudumu kwa wananchi.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa NWHSA, Jane Mwikali, alieleza kuwa mradi huo ni mwanzo wa mabadiliko makubwa kwa jamii ambazo zimekuwa zikipuuzwa kwa muda mrefu.

Aliongeza kuwa ndani ya kipindi cha miezi mitatu, familia pamoja na wanafunzi watakuwa wanapata maji safi, hatua itakayochangia kuboresha afya na elimu katika eneo hilo.
Wakazi hawakuficha furaha yao, wakisema mradi huo utawaondolea mateso ya miaka mingi.
Bi Rose Awino kutoka eneo la Gongo alisimulia jinsi wakazi wamekuwa wakihatarisha maisha yao wakitafuta maji.
“Watu wamekuwa wakishambuliwa na mamba wanapochota maji kutoka ziwani. Huu mradi utabadilisha maisha yetu,” alisema.
Wakati huo huo, mwakilishi kutokaafisi ya Mbunge wa Kisumu Magharibi, Rose Buyu, alipongeza serikali kwa kuzingatia mahitaji ya eneo hilo.
Mbali na uchimbaji wa visima vipya, maafisa wa NWHSA pia walikagua miradi ya maji iliyokwama katika maeneo ya Orinde na Shule ya Msingi ya Lwala Kadawa na kuagiza ifanyiwe ukarabati mara moja.