Makala

Sheria ya ICC sasa yatumika kuwaandama Pasta Mackenzie na ‘nabii’ Anindo Temba

March 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MSHUKIWA wa dhehebu la Shakahola, Paul Mackenzie, na mwanamke aliyejitambulisha kama nabii, Shallyne Anindo Temba, wameshtakiwa kwa makosa 23 ya mauaji chini ya sheria za uhalifu dhidi ya haki za binadamu, kuhusiana na vifo 52 vilivyotokea Kwa Bi Nzaro, Kaunti ya Kilifi mwaka uliopita.

Viongozi wa mashtaka walisema ushahidi uliokusanywa unafikia kiwango kinachohitajika kuthibitisha uhalifu huo chini ya sheria za Kenya na Mkataba wa Roma unaosimamia Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC).

Bw Mackenzie na Bi Temba wameshtakiwa kwa pamoja na Kahindi Kazungu Garama almaarufu Mlewa, Tom Ochieng Mkonwe almaarufu Thomas, Julius Thuva Luwali na Johnson Gona Richard.

Mahakama Kuu ya Mombasa ilielezwa kwamba washtakiwa hao sita walipanga mauaji kati ya Januari na Oktoba 2025, wakilenga wafuasi wa kanisa la Good News International.

Washukiwa wengine wawili, Charles Mutua Musee almaarufu Mzee Mutua na James Kazungu Kahindi almaarufu Ponda au Baba Bura, wanakabiliwa na mashtaka tofauti kama wasaidizi baada ya tukio la mauaji.

Katika shtaka la kwanza, Mackenzie, Temba, Garama, Mkonwe, Luwali na Johnson wanatuhumiwa kwa kosa la mauaji.

Hati ya mashtaka inasema kuwa, kwa kutekeleza itikadi ya kanisa la Good News International, walisababisha kifo kisicho halali cha mtoto asiyejulikana jinsia mwenye umri wa kati ya miaka 10 na 11.

Waendesha mashtaka wanadai kuwa washtakiwa walifanya vitendo kwa kufahamu kuwa vingesababisha kifo.

Mwathiriwa huyo, sawa na wengine waliotajwa katika hati ya mashtaka, ametambuliwa kupitia nambari ya kaburi ambako mwili wake ulifukuliwa.

Mashtaka ya pili hadi ya 23 yanafanana kwa muundo na maudhui na shtaka la kwanza.

Katika kila shtaka, washtakiwa hao sita wanatuhumiwa kwa mauaji kuhusu watoto tofauti wenye umri wa kati ya miezi sita na miaka 17.

Mbali na makosa 23 ya mauaji kama uhalifu dhidi ya haki za binadamu, washtakiwa hao pia wanakabiliwa na mashtaka mbadala 23 ya mauaji chini ya sheria za Kenya.

Katika shtaka mbadala la kwanza, upande wa mashtaka unadai kuwa, kwa pamoja waliua mtoto huyo huyo asiyejulikana mwenye umri wa kati ya miaka 10 na 11.

Mashtaka ya pili hadi ya 23 kwa njia mbadala yanarudia mashtaka makuu lakini yamewasilishwa kama makosa ya kawaida ya mauaji, huku waathiriwa wakiwa na umri wa kati ya miezi sita na miaka 17 wakitambuliwa kupitia nambari za makaburi.

Upande wa mashtaka unadai kuwa makosa hayo yalitendwa tarehe zisizojulikana kati ya Januari na Oktoba 2025 katika eneo la Kwa Bi Nzaro, Kata ya Chakama, Kaunti-ndogo ya Magarini, Kaunti ya Kilifi.

Bw Musee na Kahindi wameshtakiwa kando kwa kusaidia wahalifu baada ya kutenda mauaji.

Musee anatuhumiwa kumhifadhi Luwali nyumbani kwake katika kijiji cha Kanyaa, Kaunti-ndogo ya Mwingi, akijua kuwa Luwali alikuwa ametenda mauaji na hivyo kumsaidia kukwepa kukamatwa.

Bw Kahindi anadaiwa kuwasaidia Temba, Garama na Mkonwe kutoroka kukamatwa jijini Mombasa kati ya Julai 19 na 21, 2025. Washtakiwa wote walikana mashtaka walipofikishwa mbele ya Mahakama Kuu ya Mombasa.

Upande wa mashtaka umeashiria nia ya kuwaita mashahidi hadi 128 na umeahidi kutoa ushahidi wote kwa utetezi ndani ya wiki moja.

Pande zote mbili, mashtaka na utetezi, zilikubaliana kutofuatilia dhamana kwa sasa na badala yake kuharakisha kesi hiyo kwa usikilizwaji wa haraka.

Washtakiwa walishtakiwa baada ya uchunguzi wa kiakili kubaini kuwa wako timamu kujibu mashtaka mapya ya mauaji, yaliyotokea chini ya kilomita 30 kutoka Shakahola, ambako zaidi ya wafuasi 450 wa kanisa lililopigwa marufuku walifariki kwa kufunga kati ya mwaka 2021 na 2023.

Kesi za Kwa Bi Nzaro zimepangwa kutajwa Machi 17.