Makala

Shinikizo zaidi Lagat ajiuzulu

Na WINNIE ONYANDO June 17th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

HATA baada ya Naibu Inspekta Jenerali Eliud Lagat kujiondoa kwa muda afisini ili kutoa nafasi kwa uchunguzi unaoendelea kuhusu kifo cha mwalimu-bloga Albert Ojwang, mamia Juni 17, 2025 walijitokeza wakishinikiza ajiuzulu.

Maandamano hayo yaliyoanza kwa amani mwendo wa saa nne yaligeuka kuwa ya vurugu n ahata kusababisha kifo cha mtu mmoja aliyepigwa risasi kichwani.

Maandamano hayo pia yalivurugwa na wahuni na magenge ya watu waliobeba visu na marungu wakipora watu hadharani.

Watu hao walikuwa wamebeba marungu na visu wakitishia watu na kuwaibia.

Haijulikana watu hao wanafadhiliwa na nani.

Akizungumza kuhusu maandamano hayo, mwanaharakati Francis Awino ambaye pia ni rais wa vuguvugu la Bunge la Mwananchi anasema kuwa maandamano hayo yanafaa kuendelea hadi Bw Lagat ajiuzulu.

“Kuna maafisa wengine ambao tayari wamekamatwa wakiwemo Afisa Mkuu wa Kituo cha Polisi cha Central (OCS) Samson Talaam na Konstabo James Mukhwana kuhusiana na kesi hiyo. Kwa hivyo, hakuna haja Bw Lagat kujiondoa kwa muda ofisini, anafaa kujiuzulu,” akasema Bw Awino.

Kulingana naye, kujiondoa kwake kwa muda ofisini haitoshi.

“Anafaa kujiuzulu hadi uchunguzi ukamilike na apatikane hana hatia kuhusiana na mauaji ya Ojwang,” akaongeza.

Kauli yake yanajiri siku moja tu baada ya Bw Lagat kwenye taarifa kusema kuwa amechukua hatua hiyo kwa kutambua wajibu wake kama Naibu Inspekta Jenerali katika Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS) na “kwa sababu ya uchunguzi unaoendelea kuhusu kifo cha kusikitisha cha Albert Ojwang”.

“Leo nimeamua kujiondoa katika afisi ya Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi hadi uchunguzi unaoendelea utakapokamilika,” taarifa hiyo ilisoma.

Bw Lagat aliahidi kutoa usaidizi wowote ambao wachunguzi watahitaji watakapokuwa wakiendesha kazi yao.

“Ninatoa risala za pole kwa familia ya Albert Ojwang’ kwa kupoteza mpendwa wao,” alisema.

Uchunguzi kuhusu kisa hicho unaendeshwa na Mamlaka Huru ya Kuchunguza Utendakazi wa Polisi (IPOA) na kufikia sasa maafisa wawili wa polisi wamekamatwa.

IPOA pia ilisema imewakamata wafungwa watatu, Gin Ammitoa Abwao, Collins Karani Ireri na Brian Mwaniki Njue, waliodaiwa kutumiwa na polisi kumdhulumu Ojwang’ ndani ya seli.

Jumla ya watu 23, baadhi yao wakiwa maafisa wa polisi, wamehojiwa kuhusiana na kifo cha mwalimu-bloga huyo.

Mwathiriwa huyo alikufa Juni 8, 2025 baada ya kudaiwa kudhulumiwa katika kituo cha polisi cha Central, Nairobi.

Kando na Nairobi, maandamano hayo pia yalifanyika katika kaunti mbalimbali huku waandamanaji wakitaka haki itendeke kwa mwendazake.

Rais William Ruto hapo awali aliahidi kuwa haki itatendeka kwa familia ya mwathiriwa na hata kutoa kitita cha Sh2 milioni kwa familia hiyo.

Kiongozi wa upinzani Raila Odinga pia aliifariji familia hiyo kwa kutoa mchango wa Sh1 milioni.