• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 8:50 AM
ULIMBWENDE: Epuka makosa haya wakati wa kuosha nywele zako

ULIMBWENDE: Epuka makosa haya wakati wa kuosha nywele zako

Na MARGARET MAINA

[email protected]

AGHALABU kila mmoja wetu anawajibika kuziosha nywele.

Wengi wetu tumekuwa tukifanya makosa kadhaa wakati wa kuosha nywele. Baadhi yetu hatutumii muda wa kutosha kusugua ngozi ya kichwa, hatuoshi vizuri au pia hatutumii conditioner.

Yafuatayo ni makosa makubwa matano ambayo watu wengi huyafanya wakiwa wanaosha nywele.

Kutozitia nywele maji vizuri

Watu wengi hawaloweshi nywele zao vizuri kabla ya kupaka shampoo. Ni muhimu kulowesha kila unywele kwa maji kabla ya kupaka shampoo ili kutakata vizuri.

Kutumia shampoo nyingi sana au kidogo sana

Sote tunafahamu kwamba kitu chochote kikizidi kina madhara au hakitaleta matokeo mazuri. Tunatakiwa kutumia kila kitu kwa kiasi. Si kwa wingi sana na si kwa uchache sana.

Kutumia shampoo nyingi kunaweza kukufanya usiweze kuipata nywele na kuisafisha vizuri kutokana na kuzidiwa na povu jingi sana. Na kutumia shampoo kidogo kutafanya nywele zako zisitakate vizuri. Pima shampoo kiganjani mwako, kiasi cha wastani – kulingana na ukubwa na wingi wa nywele zako – kwa kutumia vidole paka shampoo kwenye nywele zako ulizozigawanya kwenye makundi manne. Paka kuanzia kwenye ngozi ya kichwa – scalp – hadi kwenye ncha ya nywele.

Kutotilia maanani zaidi ngozi ya kichwa

Kama umeshawahi ‘kufanyiwa shampoo‘ kitaalam katika saluni, bila shaka unajua ni muda kiasi gani huwa wanautumia kwenye ngozi ya kichwa.

Kusugua ngozi ya kichwa ni hatua ya msingi zaidi kwenye mchakato wa kuosha nywele.

Watu wengi hawatumii muda wa kutosha kusugua ngozi zao za kichwa. Tunatakiwa kusugua ngozi zetu za kichwa kwa angalau dakika tatu.

Bila kujali urefu au aina ya nywele zako, unachotakiwa ni kusugua ngozi yako ya kichwa. Na unatakiwa kufanya hivyo kwa kutumia vidole na sio kucha kwa muda usiopungua dakika tatu.

Kutokuosha na kurudia “rinse & repeat”

Ni muhimu sana kuosha nywele na kurudia. Na hii ni muhimu zaidi kwa wale wenye nywele ndefu.

Kama una nywele fupi au ndogo kabisa, si lazima kwako kuosha na kurudia.

Baada ya kuwa umesugua ngozi ya kichwa kwa dakika tatu, ni muda wa kuosha nywele. Ukishaosha inafuata hatua ya pili ya uoshaji wa nywele.

Unatumia shampoo kama kawaida. Kwenye hatua hii utaweka msisitizo zaidi kwenye nywele zenyewe kwakuwa tayari ngozi ya kichwa ulishashughulika nayo awali.

Mara hii weka msisitizo zaidi kwenye kuosha nywele zako na hakikisha hakuna nywele inayoachwa bila kupata shampoo kuanzia kwenye mzizi mpaka kwenye ncha.

Kutokutoa shampoo vizuri kwenye nywele.

Baada ya kurudia kuosha nywele kwa mara ya pili kinachofuata ni kutoa shampoo kwenye nywele.

Watu wengi hawatoi shampoo vizuri kwenye nywele, na hii huzifanya nywele kubaki na shampoo ambayo husababisha nywele kubaki na vitu vyeupe vyeupe na nywele pia kutosafishika vizuri.

Hivyo inasisitizwa kutumia muda na maji ya kutosha kutoa shampoo na kuhakikisha imetoka kabisa kwenye nywele ili nywele zako ziwe zimesafishika vizuri.

You can share this post!

Wauguzi wakubali kurejea hospitalini

MAPISHI NA UOKAJI: Jinsi ya kuoka kuku kwenye ovena

adminleo