Vivuli vya Kaya Bombo vyatanda kuelekea 2027 Jicho Pevu akidai kuambiwa ‘arudi Mandera’
WAKATI nchi inajiandaa kwa Uchaguzi Mkuu wa 2027, Kaunti za Mombasa na Kwale zitakuwa zikiadhimisha miaka 30 tangu ghasia za kikabila zilipotokea mwaka wa 1997.
Ghasia hizo za Kaya Bombo zilizochochewa kisiasa, zilisababisha vifo na maelfu ya Wakenya wakaachwa bila makazi.
Leo, suala hilo huzungumziwa kimyakimya miongoni mwa jamii zilizoathiriwa. Hata hivyo, wanasiasa wanaopanga kuwania ugavana Mombasa wamelifufua kupitia kwa lawama za siasa za kikabila katika kampeni zao za mapema.
Baadhi ya wanasiasa wanaonuia kumng’atua Gavana wa Mombasa Abdulswamad Nassir katika uchaguzi wa 2027 ni Mbunge wa Nyali Mohamed Ali, aliyekuwa Mbunge wa Kisauni Ali Mbogo na Katibu Mkuu wa UDA Hassan Omar.
Kiini cha mjadala wa siasa za kikabila ni msimamo wa Mbunge wa Nyali, anayedai wapinzani wake wanatumia asili yake ya kikabila dhidi yake.
“Kuna watu wameanza kusema Mohamed Ali si mwenyeji, kwamba arudi nyumbani. Ninaambiwa nirudi Mandera, mara Wajir, mara Isiolo…lakini nataka wajue siondoki. Mkenya yeyote ana haki ya kuwania ugavana wa Kaunti ya Mombasa,” alisema hivi majuzi.
Hata hivyo, wapinzani wake wanapinga kauli hizo wakisema matamshi yake ni ya kujitafutia huruma kwa wapigakura bila kujali yanaweza kuzamisha Mombasa kwa kipindi cha giza.
“Labda hakumbuki Kaya Bombo. Watu wa makabila tofauti wameishi pamoja Mombasa kwa miaka mingi na hatuwezi kuruhusu mtu yeyote kuleta siasa za kikabila,” alisema Bw Mbogo katika hafla ya umma, kauli inayoungwa mkono na wanasiasa wengine.
Katika mwaka wa 1997, mapigano ya Kaya Bombo yalianza katika kijiji cha Kaya Bombo, Kaunti ya Kwale, na kusambaa hadi sehemu za Mombasa, hasa Likoni.
Ghasia hizo zilichochewa kwa lengo la kuwazuia wakazi waliodhaniwa kuwa wafuasi wa upinzani kupiga kura dhidi ya chama tawala cha wakati huo, KANU.
Uchunguzi ulionyesha kuwa, mnamo Agosti 13, 1997, mwanasiasa wa eneo hilo aliwasafirisha vijana waliokuwa na mapanga na silaha nyingine hadi Kituo cha Polisi cha Likoni.
Walivamia kituo hicho usiku na kuiba bunduki na risasi.
Asubuhi ilipofika, walitumia bunduki hizo kuwashambulia wasiokuwa wenyeji, wakiua na kuwajeruhi wengine huku wakilazimisha wengi kuyahama makazi yao
Bw Peter Musyimi, aliyekuwa mwalimu mkuu wa Shule ya Msingi ya Mwakigwene iliyo Ukunda, anakumbuka mapigano ya risasi kati ya polisi na washambuliaji.
“Ninakumbuka nikiwaagiza watu wote shuleni, wakiwemo wanafunzi, walale chini ili kuepuka kupigwa na risasi zilizokuwa zikifyatuliwa pande zote. Mapigano yalichukua saa kadhaa kabla ya washambuliaji kushindwa nguvu na polisi,” alisema Mr Musyimi.
Baada ya hapo, wavamizi hao walikimbilia msituni ambako walijificha na kupanga mashambulizi zaidi.
Mwenyekiti wa Shirika la Kijamii la Kaya Bombo (CBO), Bw Mohammed Mwalimu, alisema ingawa serikali hatimaye iliingilia kati, ilikuwa tayari imechelewa, kwani serikali hiyo hiyo ilikuwa na uwezo wa kuzuia mapigano hayo mapema.
Kulingana naye, watu 1,300 waliathirika moja kwa moja na sasa wanadai fidia kutoka kwa serikali ya kitaifa.
Kufuatia mashambulizi hayo, waathiriwa wanasema malori matatu yaliyobeba maafisa wa Polisi wa GSU yalipelekwa eneo hilo kwa zoezi la kuwanyang’anya raia silaha.
Katika hatua hiyo, raia wengi waliokuwa na silaha waliuawa.
Hata hivyo, operesheni hiyo ilizua malalamishi mengi, huku kukiwa na madai ya msako wa kiholela dhidi ya raia pamoja na ukiukaji wa haki za binadamu, ikiwemo kuwajeruhi raia wasio na hatia, ubakaji na mauaji.
Fatuma, 58, asema alipoteza biashara yake wakati wa ghasia hizo baada ya kukimbia eneo hilo. Asema akiwa njiani alikutana na maafisa watatu waliomtaka aandamane nao, ila alikataa na kujifungia ndani ya nyumba ya jirani yake.
“Walivunja mlango na kuingia kwa nguvu. Mwanangu, yale walinifanyia bado yananiumiza hadi leo. Walinibaka mmoja baada ya mwingine kisha wakanipiga, wakiniacha nikiwa karibu kufa. Walikuwa wakiniuliza tu kuhusu bunduki ambazo sikuwa najua chochote kuzihusu,” alisema.
Zoezi la kuwanyang’anya silaha lilichukua zaidi ya miezi mitatu. Baadhi ya waathiriwa bado wana majeraha ya kudumu na wanaishi kwa matumaini ya kupata haki.
Katika mwaka wa 1998, Moi aliunda Tume ya Uchunguzi kuhusu mapigano ya kikabila yaliyotokea Kenya tangu 1991, yakiwemo ya Kaya Bombo.
Tume hiyo iliyoongozwa na Jaji Akilano Akiwumi ilifanya vikao katika maeneo mbalimbali ya nchi, ikiwemo Mombasa na Kwale.
Matokeo ya uchunguzi huo, yaliyotolewa baada ya shinikizo la umma mwaka 2002, yalifichua jinsi wanasiasa waliokuwa wandani wa serikali walivyoshirikiana na baadhi ya maafisa wa polisi kupanga na kutekeleza ghasia za kikabila.
Ilibainika pia kuwa, operesheni ya usalama iliyolenga kuwafukuza washambuliaji ilihusisha wanajeshi, lakini wakati mmoja kikosi hicho kilizidiwa nguvu baada ya zaidi ya washambuliaji 300 waliokuwa na bunduki kujitokeza kutoka msituni.
Washambuliaji walichagua msitu wa Kaya Bombo kuwa ngome yao kwa sababu polisi waliogopa kuingia humo kutokana na imani za kishirikina.
Zaidi ya watu 3,000 waliokuwa wamekimbilia usalama katika Kanisa Katoliki la Likoni pia walishambuliwa, na wawili kati yao walipigwa risasi na kuuawa.
Ushahidi uliowasilishwa mbele ya tume hiyo ulionyesha kuwa, vijana hao walipokea mafunzo ya kijeshi kwa kiapo, na kwamba mashambulizi yalipangwa kwa umakini mkubwa, huku rekodi zikionyesha matumizi ya fedha kununua chakula na dawa.
Tume iliorodhesha majina ya wanasiasa, maafisa wa utawala wa serikali, polisi miongoni mwa wengine waliostahili kuchukuliwa hatua za kisheria.
Hata hivyo, hilo halikufanywa.