• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 9:50 AM
Wahudumu wa tuktuk Githurai wakarabati barabara mbovu iliyopuuzwa na viongozi

Wahudumu wa tuktuk Githurai wakarabati barabara mbovu iliyopuuzwa na viongozi

Na SAMMY WAWERU

JUMA hili limekuwa lenye shughuli chungu nzima kwa wahudumu wa tuktuk eneo la Githurai ambao wanakarabati barabara mbovu.

Chini ya muungano wa Tuktuk na magari madogo ya usafiri na uchukuzi aina ya Maruti, ndio GTMA, wahudumu hao wameikarabati barabara inayounganisha mtaa wa Githurai na Mwihoko, Kaunti ya Kiambu.

Baadhi ya sehemu katika barabara hiyo zimekuwa katika hali mbovu.

“Misongamano ya mara kwa mara na isiyoisha eneo hili na ambayo pia huathiri Thika Road, husababishwa na ubovu wa barabara hii,” Paul Kagiri msimamizi wa nidhamu GTMA ameambia Taifa Leo.

Imekuwa ratiba ya kila saa hasa eneo la Chuma Mbili, Kwa Nyanya na Kassmatt Jumbo, Githurai kushuhudia misongamano kutokana na mashimo yaliyoko katika barabara hiyo ya lami.

Wahudumu hao wamechukua jukumu la kukarabati barabara hiyo, baada ya kilio chao kwa viongozi waliochaguliwa kuwawakilisha serikalini kuonekana kupuuzwa.

“Tunawaona wakijishughulisha na Ripoti ya Maridhiano (BBI) badala ya kututatulia changamoto zinazotukumba na ambazo zilifanya tuwachague. Si mara moja, mbili au tatu tumewasilisha malalamishi yetu bila mafanikio,” akalalamika Joseph Ndung’u, mhudumu.

Kuwepo kwa mashimo, pia wanasema kunachangia kuharibika kwa tuktuk na magari mengine yanayotumia barabara hiyo.

“Isitoshe, misongamano inatupotezea wakati ambao tungekuwa tumejiendeleza kimapato na kukuza uchumi,” akasema mhudumu mwingine, akisema wakati wa mvua hali huwa mbaya zaidi.

Katika ukarabati huo, wanatumia raslimali zao kununua mawe ya kujaza kwenye mashimo, vifaa na pia kutumia magari yao kuyasafirisha.

Wahudumu wa tuktuk Githurai wakikarabati baadhi ya sehemu mbovu za barabara inayounganisha Githurai na Mwihoko, Kaunti ya Kiambu. Picha/ Sammy Waweru

Marekebisho hayo ni ya muda tu, na endapo serikali ya kaunti ya Kiambu na pia serikali kuu haitawajibika, huenda barabara ya Githurai – Mwihoko ikaharibika kupindukia.

Ni jambo la kushangaza ikizingatiwa kuwa barabara hiyo i machoni mwa viongozi waliochaguliwa eneo hilo, wakiongozwa na diwani, mbunge na pia gavana, ambao huitumia mara kwa mara.

You can share this post!

KCB yalenga kutikisa msimu mpya kuingia mashindano ya CAF

Kampeni za Diamond League msimu ujao kuanzia Rabat, Morocco