Makala

Watetezi wadai serikali inakimbiza fidia ya wahanga wa maandamano kwa hofu ya Juni 2026

Na FRIDAH OKACHI April 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WANAHARAKATI wanataka Tume ya Kutetea Haki za binadamu nchini (KNCHR) kuwa na uwazi katika mchakato wa fidia kwa waathiriwa wa maandamano ya Gen Z ya mwaka 2024 na 2025.

Pia, wamependekeza kuongezwa kwa siku za kukusanya data za waathiriwa kutoka siku sitini hadi tisini. Wanadai muda huo ni mchache na huenda ukasababisha baadhi ya waathiriwa halisi kukosa fidia hiyo.

Mkurugenzi wa kutetea haki za binadamu katika Shirika la Vocal Africa Bw Hussein Khalid alisema wamepokea taarifa kuwa Tume ya KNCHR itatumia muda wa siku 30 kuthibitisha waathiriwa halala na siku 30 za kutoa malipo hayo.

“Kwa kiwango cha chini kabisa, zilipaswa kuwa angalau siku 90 ili wapate muda wa kutosha. Tatizo la kuharakisha mchakato huu ni kwamba utaambatana na changamoto na makosa. Familia ziko katika hali ya dhiki, zina matarajio makubwa sana. Hivyo, ni jambo la busara kuruhusu muda zaidi ili mchakato huu ufanyike kwa haki, na kila mmoja apate nafasi ya kuwasilisha malalamiko yake na kuyafanyiwa kazi na tume,” alisema Bw Khalid.

“Maandamano hayo yalifanyika kwa zaidi ya kaunti 30. Na mashirika ya kutetea haki za binadamu utapata ni matano tu. Kwa hivyo watoe muda zaidi ili tufahamishe waathiriwa hao ni wapi watafikisha nakala zao za kuthibitisha uhalali,” aliongeza Bw Khalid.

Alionya Tume hiyo dhidi ya kuingiliwa na wanasiasa au serikali kuharakisha muda wa kutoa fidia hiyo. Alidai baadhi ya wanasiasa wanataka mchakato huo kuharakishwa ili kuzuia maandamano ya Juni 25 mwaka huu ambayo alidai kuwa huenda yakawa mabaya zaidi.

“Tuwe waangalifu na tufanye mambo kwa njia sahihi. Ni muhimu kuiruhusu tume ifanye kazi yake bila kuingiliwa. Isiwe na ushawishi kutoka kwa polisi au wanasiasa wakuu. Waachwe ili watekeleza jukumu lao kikamilifu.”

Kuhusu bajeti ya Sh2 bilioni, walisema hazitoshi. Kwa kuzingatia idadi ya kesi zinazohitaji fidia kutoka mwaka 2017, alidai pesa hizo zilizotengwa haziwezi kutosha.

“Hata hatujui kiwango cha fidia kinachopaswa kutolewa, kwa mfano kwa mtu aliyekamatwa tu. Bajeti hiyo inapaswa kuongezwa hadi Sh4 bilioni.”

Kwa upande wake Bi Mwanase Ahmed, Tume hiyo ya KNCHR haijafafanua ni waathiriwa wagani wanaofaa kulipwa.

“Kuna watu walioumia vibaya, waliouawa, kupigwa na hata kupata madhara ya kisaikolojia. Kuanza mchakato wa ukusanyaji wa data bila kuweka wazi aina ya majeraha au kesi zinazozingatiwa kunafanya iwe vigumu kwa familia kuelewa jinsi ya kushiriki,” alisema Bi Ahmed.

Baadhi ya wathiriwa wapo kwenye njia panda wasifahamu iwapo watapata fidia hiyo. Bi Mary Gititia, ni mwathiriwa ambaye kufikia sasa hajampata mwanawe aliyepotea June 25, mwaka 2024.

“Wangu alikuwa na miaka 26 alipotea wakati wa maandamano hayo hadi sasa hajawahi kupatikana. Ukipeleka makaratasi pale wanakuuliza uliripoti? Na hauna stakabadhi nyingine?… Wanasema wanataka wale waliuliwa ama wale walipigwa risasi. Na yule alipotea wakati wa maandamano akiandamana itakuwaje?” Alihoji.