Maoni

Madaraka Kenya ni kwa wachache walio na ushawishi

Na BENSON MATHEKA  June 2nd, 2025 Kusoma ni dakika: 1

Tangu 1963 Kenya ilipopata uhuru, ni watu wachache wanaofurahia manufaa ya kujitawala kiuchumi na kijamii na kufanya madaraka kupoteza maana yake halisi.
Kwa zaidi ya miongo sita, madaraka halisi yako mikononi mwa kundi dogo la watu wenye ushawishi mkubwa kisiasa, kiuchumi, na kijamii. Hali hii imezua maswali kuhusu usawa, haki, na maana halisi ya uhuru kwa Wakenya wa kawaida.
Kwa upande wa kisiasa, viongozi kutoka familia au jamii fulani wameendelea kushikilia nyadhifa kuu serikalini kwa miongo kadhaa.
Mzunguko wa uongozi mara nyingi huonekana kama urithi wa kifalme, hali inayofifisha matumaini ya viongozi wapya au wale kutoka jamii zisizo na ushawishi. Hii imechangia kukosekana kwa mabadiliko ya kweli katika maisha ya mwananchi wa kawaida.
Katika nyanja ya kiuchumi, mashirika makubwa na sekta muhimu za uchumi kama ardhi, benki, na viwanda vimeendelea kumilikiwa na wachache.
Rasilmali za taifa hutumika kwa faida ya watu wachache huku wengi wakisalia katika umaskini. Mchakato wa utoaji zabuni serikalini pia umejawa na upendeleo unaowanufaisha watu wenye uhusiano wa karibu na mamlaka.
Hali hii imeendeleza pengo kati ya matajiri na masikini, na kudhoofisha imani ya wananchi katika serikali.
Madaraka yanapaswa kuwa chombo cha maendeleo ya wote, si wachache. Ili kujenga taifa lenye usawa, ni muhimu kuwe na usimamizi bora wa rasilmali, uwazi katika uongozi, na ushirikishaji wa wananchi wote katika maamuzi ya kitaifa.
Madaraka ya kweli ni pale kila Mkenya anapoweza kufikia huduma za msingi, kushiriki kwenye maamuzi ya kitaifa, na kupata fursa sawa.
Hadi hapo, madaraka yataendelea kuwa kivuli cha matumaini kwa wengi, na ukweli mchungu wa upendeleo kwa wachache. Inasikitisha lakini ndio ukweli.