Maoni

MAONI: Kenya kurasimisha mkataba wa leba na Urusi ni sawa na kula meza moja na ibilisi

Na DOUGLAS MUTUA February 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

WATU wametania kwa muda sasa kuwa Kenya ni hospitali ya wendawazimu, anayepata nafuu huondoka na kwenda kuishi nje ya nchi. Yaani matatizo yaliyoko nchini yamekithiri hivi kwamba baadhi ya watu wanaamini kwingineko kokote kunawafaa kuliko huku.

Nadhani ni kwa mtizamo huu ambapo Wakenya wengi hawaoni ugumu kwenda kufanya kazi nje ya nchi hata ikiwa kazi yenyewe inahatarisha maisha yao moja kwa moja.

Tumeambiwa kwa muda sasa kuwa Wakenya wanaoibukia Urusi wakishiriki vita vya nchi hiyo dhidi ya Ukraine walijiunga na jeshi la Urusi ama kwa shuruti au hadaa, lakini pia tumewaona wengine kwenye video wakitetea uamuzi wao huo, eti wanazumbua riziki kwa hiari yao.

Ni vigumu kutambua ukweli ulipo, lakini inawezekana wapo walioingia kwa shuruti, na pia wengine walioamua kokote ni bora kuliko Kenya, afadhali kufia juani wakitafuta hela badala ya kufia kivulini wakisubiri serikali iwasaidie.

Ushahidi unaonyesha wapo Wakenya waliouawa vitani na miili yao haitawahi kuonekana, baadhi wako hospitalini wakitibiwa majeraha mabaya, na wengine wamekamatwa na Ukraine walipopatikana wakiisaidia Urusi vita, na sasa hatima yao haijulikani.

Serikali ya Kenya nayo haichelewi katika kudakia mambo! Sasa imejituma kikweli, inataka kuratibisha na kurasmisha uhusiano wa leba kati yake na Urusi ili Wakenya wakienda huko wasilazimishwe kujiunga na jeshi.

Taifa la Ukraine limeitahadharisha Kenya dhidi ya kuingia mkataba wowote wa leba na Urusi kwa kuwa huenda Wakenya wakaishia kutumiwa vibaya, ikiwa ni pamoja na kulazimishwa kupigana vita kwa niaba ya Urusi. Tayari ushahidi upo kwamba hilo linatendeka wakati huu.

Kwa taarifa yako, Serikali ya Kenya imekuwa ikilalamika kuwa Urusi inawasajili Wakenya jeshini bila kuihusisha. Hapo ndipo unapobaki na swali: Tatizo ni Serikali ya Kenya kutohusishwa, au ni hatari zinazohusiana na Wakenya kutumikia Urusi katika shughuli ya kufa na kupona?

Labda Kenya imetazama hitaji la Urusi la kuwapata wapiganaji wengi kutoka kokote kule, ikaamua hiyo pia ni fursa ya kuongeza kipato cha kigeni, ikaamua iwe wakala mkuu wa kuwezesha usajili wenyewe, ivune unono?

Hela zinazotumwa nyumbani na Wakenya wanaoishi ughaibuni, japo ni zaidi ya Sh1.6 trilioni kila mwaka, hazitoshi? Kwani Serikali yetu ina tumbo lisiloshiba?

Ikiwa tatizo ni Wakenya kuhadaiwa na Urusi na kupelekwa vitani badala ya kazi nyinginezo wanazodaiwa kuahidiwa, kwa nini Serikali ya Kenya isijiingilie kati na kushinikiza serikali za Mashariki ya Kati ambako wenzetu wengi wanaofanya kazi za nyumba wanateswa na hata kuuawa?

Kwani kuna kifo nafuu, yaani iwe si hoja ukiuliwa Uarabuni kwa kukataa kuosha mbwa kwani hiyo siyo kazi uliyoahidiwa ulipotoka Kenya, ila Mkenya mwenzako akifia vitani Urusi kwa kufumwa risasi iwe nongwa? Kwa nini msitetewe nyote?

Ikiwa Serikali ya Kenya inachukulia vita vya Urusi na Ukraine kama fursa, basi inapaswa kujiandaa kwa kuwa chochote kinaweza kutokea. Wanatamka wenzetu wa Afrika Magharibi kwamba ukitaka kula na ibilisi sharti utumie kijiko kirefu.

Kisa na maana lazima utaparurwa kwa makucha, utaishia kulia kwikwi, au, katika hali mbaya zaidi, mwenyewe utatandazwa mezani na kuliwa, tena kwa kunyofolewa, kwa raha za ibilisi mwenyewe.

Tuambizane ukweli: Kenya haina uwezo wowote wala utashi wa kisiasa wa kuikomesha Urusi ikiwa taifa hilo linaloongozwa na mkaidi Vladmir Putin litakiuka haki za Wakenya, kama vile kuwalazimisha vijana wetu kujiunga na jeshi.

Badala ya kukimbia kutangaza jinsi inavyonuia kurasmisha uhusiano wa leba na Urusi, Serikali yetu ingeweka masharti kadha, kuu zaidi likiwa kurejeshwa nchini kwa miili ya Wakenya waliouawa vitani. Urusi, kwa kiburi na dharau, haiwezi kutimiza sharti hilo hata baada ya miaka 100.

Na hilo ndilo taifa ambalo Serikali yetu inashinikiza iandikiane mkataba nalo kwa niaba ya Wakenya! Haifai hata kidogo. Huko ni kuhatarisha maisha ya watu, kushiriki kwa ujanja biashara ya watumwa ambapo Wakenya ndio bidhaa katika soko hilo.

Watetezi wa haki za kibinadamu wanapaswa kukimbia mahakamani kupinga jaribio hilo la Serikali yetu, na ikiwezekana wamwagike barabarani ili wakomeshe mpango huo kabla haujawa rasmi.

– Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika (mutua_muema@yahoo.com)