Maoni

MAONI: Masaibu ya Tuju ni funzo kwa viongozi kuhusu mamlaka ya muda

Na MARY WANGARI March 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MASAIBU yanayomwandama waziri wa zamani, Raphael Tuju yanaibua mseto wa hisia ikiwemo masikitiko, mshangao na dhihaka kwa pamoja.

Masikitiko kwa sababu, baada ya kujituma kuanzia akiwa mwanahabari wa kawaida, akawa mwanasiasa mashuhuri, waziri na hatimaye mfanyabiashara na mwekezaji tajika, sasa anakabiliwa na tishio la kupoteza mali yote aliyotumia miaka mingi kuikusanya.

Mshangao ikizingatiwa kwamba, miaka michache tu iliyopita, Tuju alikuwa miongoni mwa wanasiasa mashuhuri zaidi waliokuwa na ushawishi mkubwa nchini na kimataifa kama mwandani wa rais mstaafu Uhuru Kenyatta.

Alihudumu kama katibu mkuu wa chama tawala cha Jubilee kati ya 2016 na 2022, kabla ya kujiuzulu na kutunukiwa hadhi ya waziri maalum ambapo licha ya kutokuwa na wizara yoyote mahsusi, alishiriki maamuzi yote ya baraza la mawaziri.

Mabadiliko haya kutoka kuwa miongoni mwa watu wenye mamlaka makubwa zaidi nchini na kutangamana kwa karibu na viongozi wa hadhi ya juu hadi kutiririkwa na machozi hadharani, ni ya kukanganya si haba.

Kwa mara nyingine, Wakenya waligeuzwa ghafla watazamaji wa filamu ya kupimana ubabe baina ya tabaka la juu, Tuju alipojitokeza nyumbani kwake siku moja tu baada ya kuripotiwa kutekwa nyara.

Hata kabla ya Wakenya kuelewa mgogoro unaomwandama Tuju na kiini cha masaibu yanayotishia kumpokonya mali ya mamilioni, waligutushwa na ripoti za kutoweka kwake na kujitokeza ghafla nyumbani kwake.

Kabla hajasimulia alikokuwa, polisi walimjia, wakambeba hobelahobela hadi korokoroni, akashtakiwa kwa kutoa habari za uongo kuhusu kutekwa nyara.

Dakika chache baadaye, aliripotiwa kuuguza majeraha aliyosababishiwa na polisi huku akionekana kuwa hali mahututi hospitalini na hivyo kukosa kuhudhuria kikao cha korti, haya yakifanyika chini ya saa 24!

Matukio yote haya yalifuata mpangilio wa sarakasi za awali ambazo zimeshuhudiwa kutoka kwa baadhi ya wanasiasa mashuhuri walipojipata pabaya baada ya kuhusishwa na sakata anuai, ikiwemo madai ya kutekwa nyara yaliyoishia kuwa uzushi.

Si ajabu kwamba, baadhi ya Wakenya wamejipata kwenye njiapanda wasijue jinsi ya kuhisi kuhusu masaibu yanayomwandama Tuju ambaye sasa amegeukia Wakenya Katika kipindi hiki kigumu,

Jinamizi linalomkabili Tuju na wapendwa wake linapasa kuwa funzo kwamba mamlaka huisha hivyo watumie nyadhifa zao kutetea haki za umma.