MAONI: Polisi hawana sababu zozote za kisheria kumpiga mtu
UTAKAPOSHIKWA na polisi nchini Kenya kisha uzabwe kofi – na nakuombea lisiwe la kukuua – jua mara moja kwamba maisha yako yamo hatarini.
Kisa na maana? Isipokuwa tu nia ya kujitoa hasira zake mwenyewe, kisheria, ofisa wa polisi nchini Kenya hana sababu yoyote ya kukupiga. Haafikii lengo lolote kwa kutumia nguvu dhidi yako. Pengine nia yake kukuadhibu kinyume cha sheria.
Zamani polisi wetu waliwapiga washukiwa ili kuwalazimisha kukiri makosa, lakini baadaye sheria zetu zilibadilika ikawa kwamba taarifa yoyote unayoandikisha kwa polisi, hasa ikiwa unakiri makosa, haiwezi kutumika dhidi yako mahakamani.
Mchakato wa mshukiwa kukiri makosa ambao unakubalika kisheria ni mmoja tu: mshukiwa akiri makosa mbele ya hakimu, wala si ofisa wa polisi, na taarifa hiyo ni lazima iandikwe na hakimu mwenyewe.
Polisi wakikukamata kisha wakulazimisha kukiri makosa yoyote wakidhani wanarahisisha kazi yao, ukifika mahakamani unaweza kuruka juu na kumwambia jaji au hakimu aitupilie mbali taarifa hiyo kwa kuwa hukuiandika kwa hiari yako.
Mazoea ya polisi wetu kuwapiga washukiwa yalipungua sheria ya jinai ilipofanyiwa marekebisho na kuwapokonya polisi jukumu la kumshurutisha mshtakiwa kukiri makosa wakati wa kuhojiwa kabla hajapandishwa kizimbani.
Ofisa wa polisi aliye na akili timamu, na ambaye kamwe hanuii kukuumiza, hana sababu yoyote wala hamu ya kukupiga hata kofi moja wala kukutishia.
Zamani, hasa enzi za marais Daniel Moi na Jomo Kenyatta, walioshikiliwa mahabusu kwa makosa ya jinai waliteswa hivi kwamba baadhi yao walifikishwa mahakamani kwa viti vya magurudumu au huku wamebebwa hobela-hobela.
Kuna maswali tunayopaswa kujiuliza wakati huu ambapo tunamlia Albert Ojwang, 31, aliyefia mikononi mwa polisi: Maofisa waliompiga, wakamvunja fuvu la kichwa, damu zikamtoka machoni na kinywani, walihamasishwa na nini? Nia yao ilikuwa kumpiga tu kwa raha zao?
Inawezekana kwamba marehemu alikuwa ametenda kosa ambalo hata angalishtakiwa mahakamani hangalipata adhabu kali kiasi ambacho walalamishi wangetaka?
Ikiwa kweli marehemu alikuwa amemtukana Naibu Spekta Mkuu wa Polisi, Bw Eliud Lagat, kama inavyodaiwa, inawezekana kwamba ofisa huyo alihofia huenda kijana angaliponyoka kisheria bila kulipia makosa yake?
Nimesalitika kuuliza swali hili la mwisho kwa sababu ipo sheria nyingine muhimu ambayo ilibadilika, kosa la kumtukana au kumchafulia mtu jina likawa si la jinai tena bali la madai tu, na mshtakiwa ana haki ya kupewa dhamana.
Zamani ungeshtakiwa kwa kumchafulia mtu jina, ulikuwa unachukuliwa kama mhalifu mwingine tu, mathalan mwizi wa kimabavu au muuaji, tena adhabu yako ilikuwa kali.
Leo hii, hata ukipatikana na hatia ya kumchafulia mtu jina, unaadhibiwa kwa faini tu, na si nono kama ilivyokuwa siku hizo. Ni kutokana na mabadiliko hayo ambapo siku hizi watu mashuhuri hawakimbii mahakamani kuyashtaki magazeti yanayofichua uozo wao.
Hata hivyo, kwa sababu bado kuna watu ambao wanaishi katika enzi ya zamani, au wasioelewa kwamba hawana jinsi ya kudhibiti midomo ya watu wanaotaka kuwatukana, inawawia vigumu kukuruhusu uponyoke bila kichapo baada ya kuwaudhi.
Nimeandika na kurudia mara nyingi hapa kwamba ukiwa mtumishi wa umma wa cheo cha juu au mwanasiasa, sharti uwe tayari kutukanwa, kudhihakiwa na kudharauliwa na wananchi.
Unapaswa kuelewa umefikia wadhifa huo kutokana na uzoefu wa kazi, imekadiriwa kwamba umetimiza ubora fulani ukilinganishwa na watu unaowaongoza, hivyo hata ustahimilivu wako unapaswa kuwa wa kiwango cha juu.
Hivi utakuwa kiongozi wa aina gani ikiwa utapandwa na hasira katika Kenya hii ambapo watu wamebanwa na maisha hivi kwamba wakikutukana leo, kesho hawakumbuki walikutukania nini?
Nchi ambapo mahakama haikubali taarifa za washtakiwa kukiri makosa inapaswa kuwaelimisha polisi wake ili wapate mbinu za kuwashawishi washukiwa wafunguke mioyo wakati wa kuhojiwa bila kutishiwa. Nchi haitahitaji makachero wa kutishia watu.
Hilo likifanyika, kazi ya upelelezi itakuwa rahisi. Na hatutakuwa na sababu za kuwakimbia makachero wala kuingia hofu tukiona magari ya ‘Subaru’ yanayoendeshwa na maofisa wa Kurugenzi ya Upelelezi wa Jinai (DCI).
Polisi nao wataheshimika kwa kutumia akili na maarifa badala ya nguvu za sulubu zinazomsababishia mtu majasho na kumpa mwonekano wa mpumbavu.